Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 3, 2021. 
Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Siriel Mchembe kwa kusimamia kidete masuala ya ukatili wa kijinsia yanayotokea wilayani humo.
 Mchembe akitimiza majukumu yake ya kazi wilayani humo, ameweza kuibua ukatili unaofanywa na baadhi ya askari polisi wilayani humo, wanaodaiwa kuwashika sehemu za siri wasichana, kuwabaka, kuwapiga na kuwalazimisha kuwa na mahusiano ya kimapenzi. 
Mchembe ambaye pia kisheria ndiyo mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya, amenukuliwa akisema wazi katika mkutano huo kuwa; Mimi kama Mkuu wa wilaya, unyanyasaji wa kijinsia Handeni, Hapana.
Mkuu huyo wa Wilaya alichukua hatua za kuitisha mkutano baada ya kuwepo kwa madai ya  askari kuwapiga   na kuwajeruhi wasichana wawili katika ukumbi wa starehe wilayani humo kwa kile kinachodaiwa walikataa kuwa na mahusiano na askari hao. 
Katika mkutano huo walikuwepo wasichana ambao walitoa ushahidi wa wazi kuwa wanalazimishwa kuwa na mahusiano na askari na endapo wanawakataa basi wanawekwa mahabusu bila sababu ya msingi.
 Mashahidi wengine katika mkutano huo wamesema kuwa baadhi ya askari polisi huingia kwenye kumbi za starehe na kuwapiga wasichana bila sababu anuwai yenye mashiko.  
 Kadhalika, DC Mchembe alisimamia kidete tukio la mwezi Agosti mwaka huu, la mtoto wa miaka 10 kubakwa  mara kadhaa na kijana wa miaka 20 wilayani humo. 
TAMWA tunaamini kwamba utendaji kazi wa namna hii unaofanywa na Mheshimiwa Mchembe, utasaidia kupunguza matukio ya  ukatili wa kijinsia ambao umekuwa ukisababisha madhara makubwa ya kimwili na kiakili kwa watoto wa kike na wanawake. 
 Kadhalika, tunakemea vikali vitendo vya askari polisi kutumia madaraka yao vibaya  na kufanya ukatili wa kijinsi kama huu. 
Hakuna aliye juu ya sheria, na ndiyo maana askari wana dhamana ya kusimamia sheria hizi, lakini cha ajabu baadhi wamekuwa wa kwanza kuzivunja, Dkt Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA.
Dkt Reuben amesema ukatili wa namna hii sio tu unavunja haki za binadamu lakini pia ndicho chanzo cha madhara mengi ikiwamo mimba zisizotarajiwa, mimba za mapema, magonjwa ya kuambukiza na wakati mwingine madhara ya kimwili kama majeraha. 
Polisi wasimamie maadili yao ya kulinda raia na mali zao, wasiwe washika bendera wa kuendeleza ukatili wa kijinsia, hakuna aliye juu ya sheria, amesema Dkt Reuben. 
TAMWA tunaomba askari watakaobainika kufanya ukatili huo wachukuliwe hatua huku tukiendelea kumtia moyo Mheshimiwa Mchembe kulinda na kutetea haki za wanawake na watoto wilayani humo. 
Dkt Rose  Reuben
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Machi 8th 2022, Dar es Salaam. Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, kinalazimika kutupia jicho lake kwenye usalama wa wanahabari wanawake katika vyumba vya habari nchini Tanzania.
 
Ulazima huu umekuja baada ya kuwepo kwa mwendelezo wa matukio, ushahidi, na ripoti za kitafiti zinazoonyesha kuwa wanahabari wanawake siyo tu Tanzania bado wanapitia unyanyasaji wa kingono katika vyumba vya habari. 
 
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kwa mwaka huu, yamebebwa na Kauli mbiu isemayo; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu. Kauli hii inatupeleka zaidi kutaka kuweka usawa katika vyumba vya habari baada ya kubaini kuna mdudu anayetafuna tasnia ya habari kimya kimya. 
 
 Utafiti uliofanywa na Asasi ya Wanawake katika Habari Africa (WIN) mwaka 2022 ulibaini kuwa, asilimia 41 ya wanawake wanahabari waliwahi kufanyiwa unyanyasaji wa kingono wakiwa katika maeneo ya kazi. 
 
Hivyo basi wakati tukiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, TAMWA inahimiza Wamiliki wa vyombo vya habari, watunga sera, serikali na wanahabari wote kwa ujumla kutupia jicho unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa ndani ya vyumba vya habari.
 
Unyanyasaji wa kingono kwa wanahabari iwe ndani au nje ya vyumba vya habari, una madhara makubwa katika chombo cha habari, taaluma ya habari, aina ya habari zitakazoandikwa na hata katika maendeleo ya nchi yenyewe. Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk  Rose Reuben.
 
Udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari wanawake, unachagiza wanahabari wengi wa kike kuikimbia tasnia  na hilo limesababisha kupoteza vipaji lukuki ambavyo vingekuzwa iwapo kusingekuwa na bughudha hiyo.
 
 
Kadhalika udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari unashusha hadhi ya chombo cha habari, kwani pindi mwanahabari anapotoa shutuma kuwa mhariri au kiongozi wa chombo cha habari kamdhalilisha kingono, basi ni dhahiri chombo hicho hutazamwa vibaya. Kadhalika vivyo hivyo anapotoa taarifa kuwa amedhalilishwa na chanzo cha habari.
 
Kaika utafiti uliofanywa na TAMWA kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) mwaka 2021, kuhusu hali ya rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari, ilibainika kuwa wanahabari wanawake wamewahi kukutana na udhalilishaji huu, kimwili, kimaneno na hata baadhi walifukuzwa kazi. 
 
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyoiona TAMWA katika tafiti hizo ni ukimya. Wanahabari wengi wanawake hawataki kusema pindi wanapodhalilishwa, hivyo wanaishi katika msongo, maumivu, fedheha na wengine kuacha kabisa tasnia, kwa sababu ya udhalilishaji wa aina hii.  Dk Rose Reuben.
 
Utafiti wa TAMWA ulibaini kuwa wanafunzi wengi wa tasnia ya habari wa vyuo vikuu wanaokwenda kujifunza kwa vitendo  katika vyumba vya habari wamekutana na udhalilishaji huo na kujikuta wakiikimbia tasnia hiyo mara tu wanapomaliza masomo yao. 
 
Hata utafiti wa WIN uliofanyika Afrika nzima kuangalia ukubwa  wa tatizo hilo, ulibaini kuwa ni asilimia 4 tu ya wanahabari wanawake wanaopaza sauti zao pindi wanapofanyiwa ukatili huu.
 
Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, kwanza tunawaasa wanahabari kupaza sauti zao na kueleza bayana madhila wanayopitia katika kazi zao ikiwamo udhalilishaji wa kingono.
 
Imetosha sasa wanahabari kuwa kipaza sauti cha kusemea matatizo ya wengine  katika jamii, ilhali tatizo lao wamelinyamazia kimya, Dk Rose Reuben.
 
Kadhalika tunaviomba vyombo vya habari kuhakikisha vinaweka na ketekeleza sera ya jinsia ndani ya vyumba vya habari, na sera ya kupinga unyanyasaji na rushwa ya ngono na sera hizi zijulikane na wote ndani ya vyumba vya habari. 
 
Katika utafiti wa TAMWA tulibaini kuwa vyumba vingi vya habari havina sera ya jinsia wala sera za kupinga rushwa na unyanyasaji wa kingono, na vile vyenye sera hizi hazitumiki au hazijulikani na wanahabari/ wafanyakazi wengine, Dk Rose Reuben.
 
Lakini zaidi tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu sheria ya mwaka 2017 inayoangalia rushwa ya ngono mahala pa kazi. Hii itasaidia wanawake na wasichana kuifahamu  kujua kuwa uwepo wa sheria hii na namna ya kukusanya ushahidi wa madhila hayo. 
 
Lakini wakati huo huo serikali ione umuhimu wa kupeleka ajenda ya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu na hata mashuleni, ili kuwajengea uelewa watoto wa Tanzania uelewa na athari ya rushwa hii. 
 
Kwa mfano, hivi karibuni yamekuwapo matukio kadhaa ya wahadhiri kwa vyuo vikuu kuwadhalilisha kingono wanafunzi na huku video zao za utupu zikivuja. Haya na mengine mengi yapo pia katika vyombo vya habari na mahala pa kazi ikiwamo serikalini. 
 
Kwetu sisi TAMWA hili ni janga na ni muuaji wa kimya kimya wa utu wa wanawake,  endapo lisipochukuliwa hatua basi mabinti zetu vyuoni na wanataaluma katika uandishi watapoteza mwelekeo na hivyo tutapoteza vipaji na nguvu kazi, Dk Rose Reuben.
 
 
Kama kauli mbiu ya mwaka huu isemavyo, Haki Sawa kwa maendeleo Endelevu ndivyo tunavyotaka wanahabari wanawake waheshimiwe na wathaminiwe, watimize wajibu wao bila kulazimishwa au kurubuniwa kutoa rushwa ya ngono. 
 
Tunachoweza kusema TAMWA ni; Mwanahabari mwanamke anaweza kuripoti habari za uchunguzi kama mwanaume, anaweza kuripoti michezo kama mwanaume, anaweza kuripoti katika vita kama ilivyo kwa wanaume. Uanamke wake, hauondoi ujasiri, utimamu na umakini katika taaluma  yake. 
 
Kadhalika, Mwanahabari mwanamke hapimwi kwa sura wala sauti yake, bali ujuzi na kipaji katika taaluma yake ya uanahabari. 
 
TAMWA tunasisitiza kuwa hiki ni; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu kama kauli mbiu  ya mwaka huu isemavyo. 
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
 
Dk Rose Reuben
TAMWA
 

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam Agost 12, 2020. Wakati macho na masikio ya Watanzania yakiisubiri kwa hamu Oktoba 28 ambayo ni siku ya uchaguzi mkuu nchini, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF) pamoja na Global Peace Foundation (GPF) tunaoa mapendekezo kwa  vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi, kuondoa changamoto zote zinazochagiza ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
Uchaguzi Mkuu unafanyika wakati ambapo kati ya wagombea 16 waliochukua fomu kugombea urais, wapo wanawake wawili mpaka sasa ambao ni Queen Cathbert Sendinga wa Chama cha ADC, na Cecilia Augustino wa Demokrasia Makini walioteuliwa na vyama vyao kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi huo. Kadhalika, wapo wanawake watano wanaowania umakamu wa Rais, katika mchakato huu wa uchaguzi. 
Lakini TAMWA, WiLDAF  na GPF  taasisi ambazo malengo yake ni kuwepo kwa jamii yenye amani, inayoheshimu haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia, na amani zimeona ni vyema kuikumbusha jamii, wadau wa masuala ya siasa na ya jinsia  kuzifanyia kazi changamoto zinazochangia ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
 TAMWA WiLDAF  na GPF  chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake Afrika, (AWDF) kupitia mradi wa ‘Wanawake Sasa’ imeendesha midahalo mbalimbali ya wanawake kutoka  vyama vya siasa ,wakiwamo wanawake wanasiasa, viongozi wa dini na kubaini kuwa bado kuna changamoto  zinazopelekea ushiriki mdogo wa wanawake katika siasa.
Midahalo tuliyofanya  katika  kanda za Dodoma, Arusha, Zanzibar na Dar es Salaam, iliibua changamoto zinazowakabili wanawake katika siasa ikiwamo lugha dhalilishi  zinazowavunja moyo wanawake  wanaogombea au walio katika nafasi za uongozi pamoja na familia zao kuwania nafasi mbali mbali za uongozi.
Wanawake wanaogombea nafasi za uongozi, hukutana na changamoto  ya lugha dhalilishi wakati wa kampeni, na hata wakati wa utendaji wao wa kazi ili tu kuwakatisha tamaa na kuwarudisha nyuma. Kama tunataka uchaguzi wa haki na wa kidemokrasia, ni muhimu kwa tume ya uchaguzi na vyombo vya usalama kupiga marufuku na kutoa adhabu kali kwa wanasiasa watakaotoa lugha hizi dhidi ya wanawake, Rose Reuben, Mkurugenzi TAMWA.
Katika midahalo hiyo, TAMWA , WiLDAF  na GPF  tumebaini kuwepo kwa rushwa ya kifedha katika shughuli za kawaida za siasa na hasa wakati wa chaguzi mbali mbali za ndani ya vyama, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu. Hii ni pamoja na tabia za wajumbe wanaotegemewa kupiga kura kuwa na hulka ya kudai au kujenga mazingira ya kupewa kitu kidogo ili waweze kutoa ushirikiano kwa mgombea. Hii inaathiri  wanawake ambao wengi wao hawana kipato cha kutosha hasa wanawake vijana. 
 
Pia tumebaini uwepo wa vitendo vya kuomba au kutengeneza mazingira ya rushwa ya ngono kwa baadhi ya wanaume wenye dhamana za kusimamia michakato ya chaguzi au mamlaka ndani ya vyama vya siasa.Changamoto hiyo husababisha wanawake kudhalilishwa na kuharibiwa ndoto zao za kisiasa na wakati mwingine familia au wenzi wao kuwazuia kushiriki katika siasa. 
Hayo na mengine mengi, yanachangia wanawake, kuvunjika moyo na hivyo kutoshiriki shughuli za siasa au kukosa nafasi za uongozi pale wanapokuwa na msimamo wa kutotoa rushwa.
Katika hili tunapenda kutoa rai kwa wanawake wenzetu kukataa kabisa kudhalilishwa na kutojihusisha na vitendo vya rushwa ya fedha au ngono na pia tunashauri jumuiya za wanawake ndani ya vyama vya sisasa kuvunja ukimya na kuhakikisha hoja za rushwa katika siasa inazungumzwa katika kila vikao vya jumuiya na vikao vingine muhimu. 
Pia tunaviomba vyama vya siasa viweke utaratibu madhubuti na wa siri wa kutoa taarifa za vitendo hivi na kuwe na kamati huru ndani ya vyama zisizofungamana na yeyote zitakazoratibu upokeaji, ufuatiliaji na utoaji adhabu kwa wale ambao bado wanaendekeza vitendo hivi vya kuwadhalilisha wanawake.   
Changamoto nyingine zilizoibuliwa katika midahalo hiyo,  ni Ilani za vyama vya siasa ambazo hazitoi nafasi kwa wanawake kuwa viongozi na kupata nafasi ya kugombea katika majimbo. Tumebaini wanawake wengi wanashindwa kushiriki uchaguzi kwa kutopata baraka hii kuanzia ndani ya vyama.
Wakati huo huo tunavitaka, vyama hivyo viwachague wanawake wenye uwezo wa kisiasa na wa uongozi.
Tunapenda kuvipongeza vyama vya siasa ambavyo vimetoa nafasi za wanawake kugombea nafasi za udiwani na ubunge na hata urais katika kura za maoni. 
“Mwaka huu wanawake wengi wamejitokeza. Tungependa kuviomba vyama vya siasa kuhakikisha kuwa wale wanawake wenye uwezo wasimamishwe kugombea nafasi hizo na tunawaomba wananchi wote kuwachagua wanawake waliosimamishwa kugombea nafasi za ubunge na udiwani, na wengine wapewe nafasi za teuzi mbalimbali Mkurugenzi wa GPF , Martha Nghambi. 
Tunavikumbusha vyama kuendelea kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake ambao hawakupata nafasi mwaka huu ili waweze kusimama na kugombea chaguzi zijazo ndani ya vyama vyao, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
Kadhalika tunapenda kuwaasa wanawake kuepuka kugawanywa na zile kauli kuwa, hawapendani badala yake waendelee kushirikiana na kupeana fursa mbalimbali za kisiasa, kiuchumi na masuala ya kijamii.
Kauli hizi za kuwa wanawake hatupendani si za kweli bali zimekuwa zikitumika katika jamii kuwagawa wanawake kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, Reuben 
Tunatarajia kuwa serikali, wadau wa siasa, vyombo vya usalama vitazingatia kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DK John   Pombe Magufuli ya kuwepo kwa mazingira wezeshi kwa wanawake katika uchaguzi mkuu na katika nafasi za uongozi na maamuzi. Pia tunampongeza kwa kuendelea kumchagua Mama Samia Suluhu kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao. 
 
Tungependa kumalizia kwa kusisitiza kauli zilizotolewa na Rais, viongozi wa vyama mbali mbali na tume ya taifa ya uchaguzi kuwa uchaguzi wa mwaka huu utakuwa ni  huru, haki na wa amani. 
Tunawakumbusha wagombea wote kuhakikisha kuwa hawatoi kauli zozote za uvunjifu wa Amani, kuchochea vurugu, kuwagawa watu kwa dini au makabila yao au matusi na udhalilishaji wa kijinsia kwa wagombea wengine. 
Wakati huo, TAMWA, WiLDAF na GPF  inaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuendelea kuhimiza uchaguzi huru, wa haki na usawa na kutengenezwa kwa mazingira sawa ya ushindani kwa wagombea wote.
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ubariki Uchaguzi Mkuu wa Octoba 2020. 
 
Rose Reuben Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
Anna Kulaya Mkurugenzi - WILDAF
Martha Nghambi Mkurugenzi - GPF

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Abeda Rashid Abdallah.....
Ndugu wadau wa masuala ya jinsia.
Viongozi wa serikali,
Wanahabari, 
Itifaki imezingatiwa!
 
Zanzibar, February 4, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kina furaha kubwa kupata fursa hii adhimu,  leo Februari 4th, 2021, ya kukutana tena na wadau wake muhimu walioshiriki katika utekelezaji wa mradi wa Wanawake Sasa’ uliofadhiliwa na taasisi ya kimataifa ya African Women, Development Fund (AWDF).
 
Mradi wa ‘Wanawake Sasa’ umehitimishwa kwa mafanikio makubwa na kamwe mafanikio hayo yasingepatikana bila nyinyi wadau muhimu ambao mlishiriki katika kuhimiza Amani, ushirikiano  katika chaguzi na ushiriki wa wanawake katika siasa, uongozi na maamuzi.
 
Kutokana na ushirikiano wenu, tumeona namna ambavyo Rais, John Maguuli ameendelea kuteua viongozi wanawake, na hilo limethibitishwa katika kauli yake aliyoitoa Novemba, 2020 mara baada ya uchaguzi kuwa; ataendelea kuwaamini wanawake. 
Kwa msingi huo napenda nitumie fursa hii kuahidi kuwa, serikali ninayoiongoza itaendelea kuwaamini wanawake katika kushika nafasi mbalimbali za uongozi, alisema Rais JPM.
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
Si hayo tu, tumeona kivitendo, ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi na tumeshuhudia idadi ya wanawake zaidi ya 230 katika bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwamo mawaziri wanawake.
Kwa upande wa Zanzibar, tuliona uthubutu wa kinamama wawili, waliojitokeza na kuchukua fomu za kuwania urais. 
 
Ndugu mgeni rasmi,
TAMWA inaishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) na ile ya bara kwa kushiriki katika matukio ya utekelezaji wa mradi huu katika maeneo manne, ikiwamo Zanzibar, Arusha, Dar es Salaam na Dodoma. 
 
Viongozi wa Serikali wameshiriki kwa kiasi kikubwa katika kufungua, kutoa nasaha na kutoa ushauri kwa TAMWA katika ajenda hii ya ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi, Amani na mshikamano. Tunawashukuru!
 
Ndugu Mgeni Rasmi
Kupitia midahalo ya wanawake wanasiasa iliyofanywa katika maeneo yetu manne ya mradi, wanawake wanasiasa zaidi ya 150 kutoka vyama mbalimbali vya siasa nchini,  walipata fursa ya kujifunza umuhimu wa kutumia vyombo vya habari kueneza ajenda zao za kisiasa.
 
Pia kupitia midahalo hiyo, waliweza kujifuza changamoto za kila mmoja hasa katika mrengo wa ukatili wa kijinsia, ikiwamo rushwa ya ngono na kujua namna ya kukabiliana na changamoto za aina hiyo.
Wanawake wanasiasa waliopata mafunzo waliteuliwa kuanzia ngazi ya kanda hadi kitaifa. 
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
TAMWA iliwaleta pamoja viongozi wa dini 50 kutoka maeneo hayo manne ambao walishiriki kikamilifu kueneza Amani wakati wa uchaguzi na kusisitiza ushiriki wa wanawake katika siasa, uongozi na maamuzi. Haya kwetu ni mafanikio kwani, nafasi ya viongozi wa dini katika kuhubiri Amani na kuwaleta watu pamoja, vilisaidia katika kufanyika kwa uchaguzi wa Amani, huru na wa haki. 
 
Ndugu mgeni rasmi, 
Kama ujuavyo TAMWA inatumia silaha yake kuu, ambayo ni vyombo vya habari katika kufikisha ajenda kwa jamii, na hivyo iliwapa mafunzo wanahabari zaidi ya 70 kutoka katika maeneo hayo manne. Wanahabari hao walifundishwa na kupata ujuzi kuhusu umuhimu wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi.
 
Wanahabari hao baada ya mafunzo walifanikisha kuchapishwa kwa Makala za magazeti 40, vipindi vya redio  na televisheni, talk show na kuongeza wigo wa  idadi ya wanahabari tuliofanya nao kazi awali na kuwafikia wa wanahabri zaidi kutoka Zanzibar, Arusha hadi  Dodoma ambao waliandaa Makala za kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi. 
 
Ndugu mgeni rasmi, 
TAMWA na wanahabari kupitia kazi zao, walishirikiana na kuwafikia wanawake ambao awali waliogopa kushiriki katika siasa na uongozi. Hii iliongeza idadi ya wanawake waliojitokeza kuwania nafasi za uongozi kuanzia ngazi za chini hadi nafasi za ubunge. 
 
Taarifa fupi ya mradi Wanawake Sasa
Wanawake Sasa ni mradi uliotekelezwa kwa ushirikiano wa asasi tatu, TAMWA, WiLDAF na GPF Tanzania, chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake wa Afrika (AWDF).
Mradi huu ulikuwa na malengo makuu matatu, kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za uongozi na maamuzi, kwa kuwahamasisha na kuwawezesha wanawake, wanawake wenye ulemavu na vijana kuwa viongozi.
 
Lengo la pili, ni kuwahamasisha na kuwawezesha wanawake katika vyama vya siasa kuwania nafasi za uongozi katika vyama vyao. 
Lengo la tatu ni, kukuza wanawake kisiasa, kuhamasisha Amani katika chaguzi kupitia vyombo vya habari kwa kuishirikisha jamii. Mradi huu wa mwaka mmoja, ulianza kutekelezwa Januari Novemba 2020 na utekelezaji wake ulivihusisha vyama vitano vya siasa (CCM,ACT WAZALENDO,CUF,CHADEMA NA NCCR-MAGEUZI) katika kanda nne Arusha, Dar es Salaam, Dodoma na Zanzibar.
 
Mkurugenzi Mtendaji,
 
Rose Reuben.
 
TAMWA.

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Ndugu mgeni rasmi,
Wawakilishi wa FES,
Mkuu wa Dawati la Jinsia,
Mwakilishi wa Takukuru,
Wanahabari,
Nawasalimu kwa jina la JMT!
 
Dar Es Salaam, 2nd December, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Friedrich-Ebert-Stiftung (FES) Tanzania, wanaungana na watanzania wote kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.
 
Maadhimisho haya, hufanyika kila ifikapo Novemba 25 hadi Desemba 10 kila mwaka.  Kwa mwaka huu, maadhimisho haya yamepambwa na kauli mbiu isemayo: Pinga ukatili wa kijinsia Sasa 
 
Hata hivyo wakati maadhimisho haya yakiendelea, TAMWA pamoja na FES tumebaini kuwa tatizo la rushwa ya ngono mahala pa kazi linaendelea kushika mizizi katika jamii yetu. 
 
Hilo lilibainika hata wakati TAMWA ilipofanya mradi na Asasi ya Habari ya Internews mnamo mwaka 2019 na kuwashirikisha wanahabari kufanya habari za uchunguzi kuhusu rushwa ya ngono mahala pa kazi.
Makala za wanahabari hao, zilibainisha wazi, rushwa hiyo ipo lakini imegubikwa na ukimya hasa kutoka kwa waathirika. 
Kadhalika, mwaka 2021, TAMWA kwa kushirikiana na Women Fund Tanzania, (WFT) ilitekeleza mradi wa kuangazia rushwa ya ngono kwa wanahabari. TAMWA ilifanya utafiti na kubaini wanahabari wanakabiliwa kwa kiasi kikubwa na rushwa ya ngono na ukatili mwingine ndani ya vyumba vyao vya habari.
Utafiti  uliofanywa na asasi ya EBA nchini Tanzania mwaka 2020 ulibaini kuwa, suala la rushwa ya ngono linafahamika na limetanuka kuanzia katika sekta ya elimu na katika sekta ya ajira. 
 
Tatizo la rushwa ya ngono ni kubwa lakini limegubikwa na ukimya, wahanga wengi hawatoi taarifa wakiogopa kudhalilishwa zaidi, Dr Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA.
 
TAMWA tunasema, rushwa ya ngono vyuoni ndicho chanzo cha kuwa na wanafunzi wasio na tija katika sekta ya ajira, lakini pia ndicho chanzo cha kuzalisha wanaataluma wasio na sifa za kuajiriwa. 
 
Rushwa hii ya ngono mahala pa kazi na vyuoni, ndicho chanzo pia cha maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na magonjwa mengine ya zinaa, Dr Rose Reuben. 
Katika tafiti zetu, TAMWA tumegundua kuwa rushwa ya ngono hufanyika sio tu mahala pa kazi, bali wakati mwingine, hata katika kambi za wakimbizi, katika shule za sekondari.
Rushwa ya ngono hurudisha nyuma maendeleo ya mtu mmoja mmoja na nchi kwa sababu matokeo ya ukatili wa aina hii ni kurudisha nyuma ari ya utendaji kazi wa wanafunzi, wafanyakazi au waumini, Dr Rose Reuben
 TAMWA tumeona pia zipo changamoto katika kukabiliana na aina hii ya ukatili, kwanza ni ukimya. Wahanga wengi kushindwa au kuhofia kutoa ushahidi na kuzungumzia suala hili. Lakini pili, ukosefu wa takwimu zitakazowezesha wadau kufanyia kazi aina hii ya ukatili.
Ipo sheria ya makosa ya rushwa, inayogusa rushwa ya ngono, nayo ni sheria namba 11 ya mwaka 2007, kifungu cha 25. Dr Rose Reuben
 
Ukatili kwa njia ya mtandao
Wakati huo huo, tunakemea vikali ukatili kwa njia ya mtandao unaoendelea. Tumeona, tumesikia na wakati mwingine sisi ndiyo tumekuwa waanzilishi wa ukatili huu. Kutumia picha za wanawake vibaya, kutumia lugha dhalili kwa kundi Fulani mitandaoni, kutumia picha za watoto na kuweka maudhui yanayomdhalilisha. Haya ni baadhi tu ya matendo yanayochagiza ukatili wa kijinsia mitandaoni.
 
TAMWA ni wanahabari na wanahabari ni TAMWA, hivyo tunawaomba wadau wetu wa habari, mkatumie kalamu zenu kukemea rushwa ya ngono  ndani ya vyumba vyenu vya habari  na kuvaa joho la kupinga aina zote za ukatili wa kijinsia ikiwamo ule wa kwa  njia ya mtandao. 
 
Kadhalika, tunaipongeza serikali kwa kupitia wadau wake wakiwamo Takukuru, wamefanyia kazi suala la rushwa ya ngono kwa kufanya tafiti kadhaa lakini pia kwa kufanyia kazi makosa ya aina hii. Hongereni! lakini tunatamani  matokeo zaidi, kesi zaidi zipelekwe mahakamani, hukumu itolewe  ili kufanya mahala pa kazi pawe sehemu salama na penye tija. 
Pia tunampongeza  Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kuzindua mwongozo wa madawati ya rushwa ya ngono vyuoni. Tunaomba yakatumike kwa tija. 
Ewe Mwananchi, pinga ukatili wa kijinsia sasa,
 
#KaziIendelee
#ZuiaUkatiliMtandaoni
#ZuiaUkatili
 
Dr Rose Reuben
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
WAJIBIKA KULINDA UTU WA MWANAMKE UPATE KURA YAKE
01/09/2020
Wanamtandao wa Katiba, Uchaguzi na Uongozi ambao ni watetezi wa haki za wanawake na wasichana, yakiwemo masuala ya kukuza ushiriki wao katika uongozi wa kisiasa,    na pia tukiwa ni  wadau wakuu wa uchaguzi kama wapiga kura na wagombea katika nafasi mbalimbali za uchaguzi. Tumekuwa  tukifuatilia  kwa ukaribu mkubwa sana mchakato mzima wa uchaguzi tangu ulipoanza na matukio mbalimbali ambayo tayari yameshajitokeza ikiwemo utumiaji wa lugha za matusi na kauli mbaya za udhalilishaji dhidi ya wanawake wanaogombea na wafuasi wa vyama kwa ujumla. Kwa mfano, kumekuwepo na lugha za kutukana Wanawake wagombea wakiitwa “Malaya”, n.k 
 
Ni vema tutambue kwamba kasumba hii mbali na kwamba ni kinyume na haki za binadamu na ni kosa kisheria, inarudisha nyuma jitihada za serikali katika kufikia usawa wa kijinsia na kurudisha nyuma ari ya wanawake wengi kugombea nafasi za uongozi kwa sababu ya kuogopa kudhalilishwa. Halikadhalika,  inanyamazisha sauti za wanawake ambao ni zaidi ya nusu ya watanzania wote ambao ni wapiga kura wakuu na ambao wanahaki ya ushirki salama katika masuala ya kisiasa, suala ambalo halina tija kwa taifa letu. Kutokana na hali hii, tunaona umuhimu wa vyombo na mamlaka zinavyohusika kuwawajibisha kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi kwa wote wanaotumia matusi na lugha za kudhalilisha wanawake.
 
 Sisi, Wanamtandao watetezi wa haki za wanawake nchini, tunachukulia matukio haya kama kuvunjwa kwa Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977), inayokataza ubaguzi wa aina yoyote, na  tunaikumbusha jamii  kwamba Kanuni ya Makosa ya Adhabu, Sura ya 16, kifungu cha 89 kinataja kutumia lugha chafu dhidi ya mtu mwingine kuwa ni kosa la jinai. 
 
Tunaomba Umma wa Watanzania na Vyombo mbalimbali vinavyosimamia uchaguzi wa taifa hili utambua kwamba, ushiriki wa wanawake katika michakato ya uchaguzi ni haki yao ya kikatiba, na zimebainishwa katika sheria mbalimbali za nchi. 
 
Tume ya Taifa ya Uchaguzi huweka  wazi Kanuni mbalimbali za uchaguzi na Maadili ya vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi kwa  lengo la kuweka mazingira wezeshi kwa Watanzania wote, wakike na wakiume, kushiriki katika mchakato huu wa uchaguzi na kutoa mchango wao, kwa uhuru, uwazi na amani. Vile vile, Sheria ya Vyama vya Siasa, iliyorekebishwa mwaka 2018, katika kifungu chake cha 9, inakataza viongozi na wanachama wake kutamka au kutumia lugha za matusi, maneno ya kudhalilisha, uchochezi, au alama ambazo zinaweza kusababisha au kuhatarisha amani na ukosefu wa umoja wa kitaifa.
 
 Vilevile  Kanuni za  maadili ya Uchaguzi zilizotolewa katika Gazeti la Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania la tarehe 5/06/2020 zimebainisha mambo yaliyokatazwa kufanywa na vyama vya siasa kifungu ca 2.2 (b)  kinakataza kutumia lugha ya matusi, kashfa, kejeli, udhalilishaji na vitisho au lugha inayochochea uvunjfu wa amani au kuashiria ubaguzi wa jinsia, ulemavu, rangi au maumbile kwenye mikutano na kwenye shughuli zote za kampeni.
 
Kwa kuzingatia hili katazo, na kwa kuzingatia haki zetu za kikatiba na sheria za nchi, Sisi kama watetezi wa  haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa nchini, tunataka yafuatayo yazingatiwe ili kutokomeza udhalilishaji wa wanawake hasa kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi mkuu: 
Tunazitaka mamlaka zinazohusika (Tume ya Uchaguzi, Msajili wa Vyama Vya Siasa, na Taasisi nyingine husika kuwachukulia hatua kali kwa wagombea, pamoja na wapambe wao, wanaotoa lugha za kudhallisha na kutukana wanawake kwenye kampeni au mahali popote wakati huu wa uchaguzi m
Tunawataka viongozi wa taasisi mbalimbali zikiwemo za dini, na hasa vyama vya siasa, Asasi za Kiaraia, na Jamii yote kwa ujumla ya Tanzania kukemea vikali tabia hizi za kudhalilisha wanawake hasa kipindi hiki cha uchaguzi.
 
Vyama vya Siasa vitambue kwamba vina wajibu wa kulinda, kutetea na kudumisha haki na usawa wa Wanawake ndani ya vyama vyao na katika jamii kwa ujumla, kwa kuwa Wanawake ndiyo kundi kubwa la wapiga kura Tanzania. Kwahiyo lazima viheshimu UTU wa mwanamke  na kutoa fursa na kuweka mazingira yaliyo ya wazi na wezeshi ili wanawake wengi washiriki kikamilifu katika kutimiza haki yao ya kikatiba kama wagombea  na wapiga kura.
 
Mwisho na siyo kwa daraja, sisi wanawake wote kwa ujumla wetu, bila kujali Imani za kiitikadi, tukemee, tukatae na kuwajibisha wale wote wenye kutudhalilisha kwa njia yoyote ile, ikiwa ni pamoja na kututukana  
 
Tunawataka wanahabari na vyombo vya Habari kutumia taaluma yao vizuri kutetea UTU, HAKI ya mwanamke na hususani kipindi hiki cha uchaguzi. Vyombo vya Habari visishiriki katika kusambaza taarifa zenye lugha za matusi na udahlili zilizodhamiria katika kumdalilisha mwanamke wa Taifa hili.
 
 
Tamko hili la kukemea lugha za matusi dhidi ya wanawake ni mwendelezo wa matamko ambayo Wanamtandao tumeshayatoa tangu uchaguzi huu uanze. TUNALAANI NA KUKEMEA KWA NGUVU ZOTE MATUMIZI YA LUGHA ZA MATUSI, LUGHA ZA KEJELI, UDHALILISHAJI,  KATIKA KIPINDI CHOTE CHA UCHAGUZI
 
 
Imetolewa leo Septemba 1, 2020
Mtandao wa Wanawake Katiba Uchaguzi na Uongozi.

Search