Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Oktoba 29, 2021.
 
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinalaani  tukio la Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma, kudaiwa kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi na wanafunzi wa kike chuoni hapo.
 
Taarifa iliyotolewa na Chuo hicho baada ya kusambaa kwa jumbe za uwepo wa tukio hilo chuoni hapo katika mitandao ya jamii,  imeeleza kuwa Mhadhiri huyo, Petrol Mswahili, amefanya vitendo hivyo kwa wanafunzi wa kike, jambo linalodhihirisha uwepo wa rushwa ya ngono. 
 
TAMWA ikiwa ni taasisi inayopinga unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake ikiwamo rushwa ya ngono, tunalaani  tukio hilo linalovunja maadili ya utumishi wa umma na zaidi hasa kudhalilisha watoto wa kike katika taasisi hii ya elimu ya juu.
 
Kadhalika, TAMWA tunasikitishwa na  vitendo hivyo ambavyo sio tu vimekuwa chanzo cha kuharibu mustakabali wa kitaaluma wa watoto wa kike, lakini pia ndicho chanzo cha magonjwa ya kuambukiza, sonona na kurudisha nyuma kundi hilo. 
 
Mwaka 2019 TAMWA ilifanya tathmini ya kuangazia ukubwa wa rushwa ya ngono kwenye vyumba vya habari, maeneo ya kazini na taasisi za elimu ya juu, na kubaini kuwa tatizo hilo lipo kwa ukubwa wake.
 
Kadhalika TAMWA ilibaini kuwa ukimya umetawala kwa wale waathirika wa rushwa ya ngono kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo woga wa kukosa vibarua, kufukuzwa shule au kufeli mitihani yao. 
 
Hivyo tunalaani vikali vitendo hivi huku tukiupongeza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kuchukua hatua za haraka dhidi ya mhadhiri huyo lakini pia tunaushauri uongozi wa chuo hicho kuweka mikakati itakayokomesha vitendo hivyo.
 
TAMWA inaomba pindi uchunguzi utakapokamilika basi sheria ichukue mkondo wake ili iwe funzo kwa wahadhiri wengine wanaoharibu watoto wa kike. Pia tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB) iendelee kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu rushwa ya ngono na udhalilishaji mwingine wa kijinsia. 
 
"Digrii bila rushwa ya ngono, ni digrii yenye tija"
 
Imetolewa na;
 
Mkurugenzi Mtendaji waTAMWA,
 
Dk Rose Reuben.
 

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 13, 2021. Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kuteua wanawake wawili katika Baraza la Mawaziri.
 
Uteuzi huo umefanyika jana ambapo Dkt Ashatu Kijaji ameteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na  Teknolojia ya Habari, wakati Dkt Stergomena Tax ameteuliwa kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
Uteuzi huu unafanya idadi ya mawaziri wanawake kufikia saba, kutoka watano walioteuliwa awali. 
 
TAMWA tunampongeza Rais Samia pia kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kumteua mwanamke kushika wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
"Uteuzi alioufanya Rais, wa kuongeza mawaziri wawili katika baraza unaonyesha dhahiri kuwa wanawake wanaaminika na wana uwezo wa kuleta mabadiliko katika Nyanja zote, kisiasa, kiuchumi na kijamii" Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA tunaamini kuwa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi ndiyo nguzo muhimu ya kuleta usawa na ndicho chanzo cha kuleta mabadiliko chanya katika jamii ambayo yataletwa katika usawa, haki na uwajibikaji. 
 
"Rais Samia, ameweza kuonyesha lile ambalo lilidhaniwa haliwezekani kwa kuwaweka mawaziri wanawake katika wizara nyeti  kama ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa, pia kwa kuendelea kuteua mawaziri wanawake, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala" amesema Dkt Reuben
 
Kadhalika tunampongeza Rais kwa ile kauli yake wakati akiwaapisha mawaziri hao aliposema: Nimeamua kuvunja taboo (mwiko), iliyoaminika kwamba wizara ya ulinzi lazima akae mwanaume mwenye misuli yake, kazi ya wizara ile si kupiga mizinga au kushika bunduki,  nimevunja taboo(mwiko) hiyo na kumteua dada yetu Tax kutokana na upeo wake mkubwa alioupata akiwa Jumuiya ya Nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara
 
“Hakika Rais amevunja dhana ya kuwa wanaume pekee ndiyo wenye uwezo wa kushika wizara hii, na kwa hili tunategemea Dkt Tax hatatuangusha, bali atasimamia vyema nafasi hiyo na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika masuala ya ulinzi na usalama,kwa kuwa ana uwezo na upeo" Dk Reuben 
Kadhalika TAMWA tunampongeza Rais Samia kwa kusikiliza kilio cha wanahabari na kuunganisha Wizara ya Habari, Mawasiliano na ile ya Teknolojia ya Mawasiliano, kuwa moja. 
Hatua hiyo itawafanya wadau wa habari kufanya kazi kwa ufanisi na wepesi zaidi kuliko hapo awali. 
TAMWA tunaamini kuwa Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi na katika ngazi za maamuzi ndicho chanzo cha haki, usawa na uwajibikaji na maendeleo  ya nchi. 
Wanawake Wanaweza! Kazi Iendelee!
Dkt Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

User Rating: 3 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Julai 20, 2021.
Leo Julai 20, gazeti la Jamhuri, linalotolewa kila wiki, katika ukurasa wake wa kwanza na kuendelea ukurasa wa tatu limeandika habari yenye kichwa  kinachosema: Mambo ya Nje haijamchukulia hatua Balozi".
Katika habari hiyo, inayomtuhumu Balozi wa Libya nchini Tanzania, Bwana Kamal Ramadan Krista kuhusika katika usafirishaji haramu wa wasichana na unyanyasaji wa kingono, Mkurugenzi wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Dk Rose Reuben amenukuliwa akisema kuwa: Sina maoni yoyote kwa sababu habari hii haikufanyiwa uchunguzi wa kutosha
Taarifa hiyo ikaeleza zaidi kuwa Dk Rose“Alipoelezwa kuwa suala hilo ni la kukiukwa kwa haki za watoto wa kike na kusafirishwa nje ya nchi kinyume na sheria huku TAMWA ikijipambanua kuwa watetezi wa haki za wanawake, alishauri watafutwe Polisi wa Kimataifa(Interpol) na Idara ya Uhamiaji. 
Aya ya mwisho ya habari hiyo imesema: Mkurugenzi huyo ameonyesha kutofurahishwa na gazeti la Jamhuri kuandika tuhuma dhidi ya mwanadiplomasia huyo.
Mkurugenzi wa TAMWA anakiri kupigiwa simu na kutembelewa na mwandishi wa Habari wa gazeti hilo Bwana Alex Kizenga tarehe 16 Julai mwaka huu majira ya mchana ambako alihitaji maoni dhidi ya Habari iliyochapishwa katika gazeti hilo wiki tatu nyuma iliyomtuhumu Balozi Krista kusafirisha wasichana wa kitanzania kwenda kufanya biashara ya ngono nchini mwake.   
Mbali na kukataa kutoa maoni kuhusu Habari hiyo kwa msimamo kuwa haikuwa na taarifa kutoka vyanzo vya msingi ama vilelezo. Mkurugenzi wa TAMWA hakukubali kutoa maoni wala kuzungumza maneno kama ilivyonukuliwa na gazeti hilo na  badala yake mhariri na mwandishi  wa Jamhuri Media ambao walidhamiria kumuandika katika taarifa hiyo wamemlisha maneno Mkurugenzi wa TAMWA Dk Rose Reuben.
Ifahamike kuwa chama hiki ni cha kihabari na hivyo kinafahamu misingi yote ya taaluma ya habari na mawasiliano na hivyo tunasikitishwa na mmonyonyoko huu wa maadili uliofanywa  na gazeti la Jamhuri.
Kwa unyenyekevu tunawataka waombe radhi katika gazeti hilo. 
Kadhalika, TAMWA inafanya kazi na wanahabari kila siku na imekuwa ikiruhusu mahojiano na Mkurugenzi Dk Rose Reuben bila kuweka vikwazo, lakini endapo chama hakijatoa ruhusa ya kunukuliwa, basi maombi hayo yaheshimiwe kama maadili ya kihabari yanavyofundisha. 
Kwa kuwa TAMWA ni sehemu ya wanahabari, tunapenda kutoa wito kwa wanahabari wote kufuata misingi na maadili ya habari pindi wanapotimiza majukumu yao. 
Dkt. Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji ~ TAMWA.

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Dar Es Salaam, October 11, 2021. Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinawakumbusha, wazazi, walezi, wadau, serikali na waandishi wa habari kuchukua hatua ili kuondoa aina mpya ya ukatili kwa njia ya mitandao ya kijamii.
 
Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike huadhimishwa duniani kote kila ifikapo Oktoba 11, ambapo kwa mwaka huu, kauli mbiu ya kitaifa na kimataifa ni: Kizazi cha Kidijitali, Kizazi Chetu!.
 
Kauli mbiu hii inalenga kuikumbusha jamii kutoa haki sawa kwa watoto wote kwenye teknolojia ya kidijitali ili waitumie  kwa Maendeleo na kwa usahihi.  
 
Zipo faida lukuki za matumizi ya mitandao ya kijamii, kama vile elimu kwa njia ya mitandao, taarifa muhimu za kitaifa na kimataifa lakini  bado watoto wa kike wameonekana kuachwa nyuma katika ulimwengu wa kidijitali kwa kukosa  fursa sawa hasa katika matumzi ya intanenti, kumiliki simu janja, na uhuru wa  kutumia mitandao ya kijamii kama ilivyo kwa watoto wa kiume. 
 
Ripoti ya Shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia masuala ya wanawake, (UN-Women) Julai mwaka huu, ilionyesha kuwa kuna ongezeko la ukatili wa kijinsia kupitia mitandao ya kijamii. 
 
Ripoti hiyo imeeleza: Upatikanaji  wa intaneti kwa watoto wa kike na wanawake, umesababisha kundi hilo kukumbana na udhalilishaji wa kingono zaidi, ukilinganisha na wanaume,
 
Kadhalika ripoti hiyo imeonyesha zaidi kuwa, watoto wa kike wamekuwa wakitishiwa kimwili, kutumiwa picha za ngono, na kupewa lugha dhalili katika mitandao ya kijamii.
 
Kwa hapa Tanzania, matukio kadhaa ya udhalilishaji wa kingono kwa njia ya mtandao yamewahi kuripotiwa ikiwamo kusambazwa kwa video za ngono zikiwaonyesha watoto wa kike, huku mwanaume akifichwa uso.
 
Aina nyingine ya ukatili wa kijinsia kwa njia ya mtandao ni kashfa na matamshi ya chuki, jina la akaunti kuibwa na  na kisha kutumiwa na watu kwa njia za utapeli au kurushwa kwa video za ngono. Hili limewakuta zaidi watoto wa kike wenye majina makubwa au maarufu katika jamii. 
 
Lakini pia, imekuwa ni tamaduni kwa watoto wa kike kurushiwa lugha dhalilishi kwa njia ya mtandao, ikiwamo zile zinazohusisha baadhi ya maungo yao ya mwili.
 
Picha za watoto wa kike zimekuwa zikisambazwa katika mitandao ya kijamii na kugeuzwa mjadala jambo ambalo limeonekana kuchangia kuongezeka kwa lugha dhalili dhidi yao.
 
Kutokana na kuongezeka kwa matukio haya yanayoendana na ongezeko la matumizi ya mitandao ya kijamii, hatuna budi kupunguza udhalilishaji huu na kuendelea kuhimiza matumizi sahihi, salama na yenye faida, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben.
 
Reuben ameomba  wazazi, walezi, serikali, asasi za kijinsia, asasi za kiraia, wapatanishi na wanahabari, kusimamia usalama wa watoto kike mitandaoni. 
 
Inawezekana tabia hizi zinaonekana kuwa ni za kawaida au kugeuzwa utamaduni lakini zimeleta madhara kwa watoto wa kike ikiwamo kukatisha masomo, kujiua, kutengwa na jamii na baadhi kuathirika kisaikolojia, Dkt, Reuben
 
TAMWA inaamini katika usawa wa kijinsia, haki za watoto na wanawake, hivyo katika kuadhimisha siku hii, tunaikumbusha serikali kutunga sheria zinazoendana na kasi ya teknolojia ili kuwabana wale watakaofanya ukatili wa kingono kwa njia ya mtandao.
 
Sheria isifumbe macho katika masuala haya, lakini si hayo tu, bado tunasisitiza hata ile sheria ya ndoa  ibadilishwe ili kumpa mtoto wa kike haki ya kusoma na kuolewa katika umri wa utu uzima Dkt. Reuben
 
TAMWA inapenda kutoa wito kwa jamii kuona umuhimu wa matumizi ya dijitali katika jamii yetu ili kuendana na uhalisia wa dunia, pia  kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kutoa na kuwezesha watoto wote kupata elimu ya masuala ya dijitali pia kurahisisha upatikanaji wa vifaa vya kidijitali  kwa kuzingatia jinsi zote bila ubaguzi.
 
TAMWA inaamini kuwa, maadhimisho ya mwaka huu, yataangazia  changamoto na fursa za kidijitali  kwa mtoto wa kike lakini bila kusahau, kuwa kumbe; malezi bora, elimu kwa mtoto wa kike ndicho chanzo cha leo kuwa na Rais wa kwanza mwanamke, ambaye ni Mama Samia Suluhu.
 
Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike ni siku ya kimataifa iliyotangazwa na Umoja wa Mataifa; pia inaitwa Siku ya Wasichana na Siku ya Kimataifa ya Wasichana. Siku hii huadhimishwa kila ifikapo Oktoba 11.
 
Umoja wa Mataifa ulianza kuadhimisha siku hii baada ya kuonekana kuna changamoto nyingi zinazomuandama mtoto wa kike ikiwamo kunyimwa fursa ya kupata elimu, ubakaji, ulawiti,  ndoa za mapema, mimba za mapema na kukosa haki nyingine ikiwamo ya kucheza na kushauri katika ngazi ya familia. 
 
Maadhimisho hayo pia yanaangalia  mafanikio ya watoto kike kidunia, ikiwamo Tanzania kama vile  kuongezeka kwa idadi ya watoto wa kike wanaopata elimu ya juu, watoto wa kike kuendelea kupata elimu ya afya ya uzazi na kufikiwa na taasisi mbalimbali zinazogusa maisha ya mtoto wa kike.
 
Kizazi cha Kidijitali, Kizazi Chetu!
 
Dkt Rose Reuben.
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 3, 2021. 
Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Siriel Mchembe kwa kusimamia kidete masuala ya ukatili wa kijinsia yanayotokea wilayani humo.
 Mchembe akitimiza majukumu yake ya kazi wilayani humo, ameweza kuibua ukatili unaofanywa na baadhi ya askari polisi wilayani humo, wanaodaiwa kuwashika sehemu za siri wasichana, kuwabaka, kuwapiga na kuwalazimisha kuwa na mahusiano ya kimapenzi. 
Mchembe ambaye pia kisheria ndiyo mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya, amenukuliwa akisema wazi katika mkutano huo kuwa; Mimi kama Mkuu wa wilaya, unyanyasaji wa kijinsia Handeni, Hapana.
Mkuu huyo wa Wilaya alichukua hatua za kuitisha mkutano baada ya kuwepo kwa madai ya  askari kuwapiga   na kuwajeruhi wasichana wawili katika ukumbi wa starehe wilayani humo kwa kile kinachodaiwa walikataa kuwa na mahusiano na askari hao. 
Katika mkutano huo walikuwepo wasichana ambao walitoa ushahidi wa wazi kuwa wanalazimishwa kuwa na mahusiano na askari na endapo wanawakataa basi wanawekwa mahabusu bila sababu ya msingi.
 Mashahidi wengine katika mkutano huo wamesema kuwa baadhi ya askari polisi huingia kwenye kumbi za starehe na kuwapiga wasichana bila sababu anuwai yenye mashiko.  
 Kadhalika, DC Mchembe alisimamia kidete tukio la mwezi Agosti mwaka huu, la mtoto wa miaka 10 kubakwa  mara kadhaa na kijana wa miaka 20 wilayani humo. 
TAMWA tunaamini kwamba utendaji kazi wa namna hii unaofanywa na Mheshimiwa Mchembe, utasaidia kupunguza matukio ya  ukatili wa kijinsia ambao umekuwa ukisababisha madhara makubwa ya kimwili na kiakili kwa watoto wa kike na wanawake. 
 Kadhalika, tunakemea vikali vitendo vya askari polisi kutumia madaraka yao vibaya  na kufanya ukatili wa kijinsi kama huu. 
Hakuna aliye juu ya sheria, na ndiyo maana askari wana dhamana ya kusimamia sheria hizi, lakini cha ajabu baadhi wamekuwa wa kwanza kuzivunja, Dkt Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA.
Dkt Reuben amesema ukatili wa namna hii sio tu unavunja haki za binadamu lakini pia ndicho chanzo cha madhara mengi ikiwamo mimba zisizotarajiwa, mimba za mapema, magonjwa ya kuambukiza na wakati mwingine madhara ya kimwili kama majeraha. 
Polisi wasimamie maadili yao ya kulinda raia na mali zao, wasiwe washika bendera wa kuendeleza ukatili wa kijinsia, hakuna aliye juu ya sheria, amesema Dkt Reuben. 
TAMWA tunaomba askari watakaobainika kufanya ukatili huo wachukuliwe hatua huku tukiendelea kumtia moyo Mheshimiwa Mchembe kulinda na kutetea haki za wanawake na watoto wilayani humo. 
Dkt Rose  Reuben
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Mhe. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Innocent Bashungwa;

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Iddi Hassan Kimata;

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari; Mhe.Eng. Kundo Andrea Mathew;

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk. Peter Mutuku Mathuki;

Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Anders Sjoberg;

Mwakilishi Mkazi wa Unesco nchini Tanzania, Mhe. Titso Dos Santos;

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Legal Service Facility, Lulu Ng’wanakilala;

Wawakilishi wa Jumuiya ya Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (MOAT);

Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika Tawi la Tanzania (MISA-Tan), Salome Kitomari;

Mwenyekiti wa Mtandao wa Radio za kijamii Tanzania (TADIO) Prosper Kwigize;

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa), Rose Reuben;

Wawakilishi wa Wakfu wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF)

Mwakilishi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT);

Wawakiliishi wa Umoja wa Club za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC)

Mwenyekiti wa Arusha Press Club, Claud Gwandu;

Wahariri na Waandishi wa habari;

Mabibi na Mabwana,

Mheshimiwa mgeni Rasmi, kwanza tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujalia uhai, na ni kwa neema zake kuwa leo tuko hapa kufanya shughuli hii muhimu ya kukumbushana utendaji wa vyombo vyabari nchini na duniani, ambapo hatimaye tutaimarisha ushirikiano kati ya dola, jamii na vyombo vya habari kwa masilahi mapana ya maendeleo ya taifa letu.

Nakushukuru kwa kukubali mwaliko wetu, kwani kwa kufanya hivi Mhe. Waziri unadhihirisha kwa matendo kauli ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati akiwaapisha makatibu wakuu kwamba serikali chini ya uongozi wake itaendelea kuenzi uhuru wa habari.

Search