Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Machi 8th 2022, Dar es Salaam. Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, kinalazimika kutupia jicho lake kwenye usalama wa wanahabari wanawake katika vyumba vya habari nchini Tanzania.
 
Ulazima huu umekuja baada ya kuwepo kwa mwendelezo wa matukio, ushahidi, na ripoti za kitafiti zinazoonyesha kuwa wanahabari wanawake siyo tu Tanzania bado wanapitia unyanyasaji wa kingono katika vyumba vya habari. 
 
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kwa mwaka huu, yamebebwa na Kauli mbiu isemayo; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu. Kauli hii inatupeleka zaidi kutaka kuweka usawa katika vyumba vya habari baada ya kubaini kuna mdudu anayetafuna tasnia ya habari kimya kimya. 
 
 Utafiti uliofanywa na Asasi ya Wanawake katika Habari Africa (WIN) mwaka 2022 ulibaini kuwa, asilimia 41 ya wanawake wanahabari waliwahi kufanyiwa unyanyasaji wa kingono wakiwa katika maeneo ya kazi. 
 
Hivyo basi wakati tukiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, TAMWA inahimiza Wamiliki wa vyombo vya habari, watunga sera, serikali na wanahabari wote kwa ujumla kutupia jicho unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa ndani ya vyumba vya habari.
 
Unyanyasaji wa kingono kwa wanahabari iwe ndani au nje ya vyumba vya habari, una madhara makubwa katika chombo cha habari, taaluma ya habari, aina ya habari zitakazoandikwa na hata katika maendeleo ya nchi yenyewe. Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk  Rose Reuben.
 
Udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari wanawake, unachagiza wanahabari wengi wa kike kuikimbia tasnia  na hilo limesababisha kupoteza vipaji lukuki ambavyo vingekuzwa iwapo kusingekuwa na bughudha hiyo.
 
 
Kadhalika udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari unashusha hadhi ya chombo cha habari, kwani pindi mwanahabari anapotoa shutuma kuwa mhariri au kiongozi wa chombo cha habari kamdhalilisha kingono, basi ni dhahiri chombo hicho hutazamwa vibaya. Kadhalika vivyo hivyo anapotoa taarifa kuwa amedhalilishwa na chanzo cha habari.
 
Kaika utafiti uliofanywa na TAMWA kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) mwaka 2021, kuhusu hali ya rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari, ilibainika kuwa wanahabari wanawake wamewahi kukutana na udhalilishaji huu, kimwili, kimaneno na hata baadhi walifukuzwa kazi. 
 
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyoiona TAMWA katika tafiti hizo ni ukimya. Wanahabari wengi wanawake hawataki kusema pindi wanapodhalilishwa, hivyo wanaishi katika msongo, maumivu, fedheha na wengine kuacha kabisa tasnia, kwa sababu ya udhalilishaji wa aina hii.  Dk Rose Reuben.
 
Utafiti wa TAMWA ulibaini kuwa wanafunzi wengi wa tasnia ya habari wa vyuo vikuu wanaokwenda kujifunza kwa vitendo  katika vyumba vya habari wamekutana na udhalilishaji huo na kujikuta wakiikimbia tasnia hiyo mara tu wanapomaliza masomo yao. 
 
Hata utafiti wa WIN uliofanyika Afrika nzima kuangalia ukubwa  wa tatizo hilo, ulibaini kuwa ni asilimia 4 tu ya wanahabari wanawake wanaopaza sauti zao pindi wanapofanyiwa ukatili huu.
 
Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, kwanza tunawaasa wanahabari kupaza sauti zao na kueleza bayana madhila wanayopitia katika kazi zao ikiwamo udhalilishaji wa kingono.
 
Imetosha sasa wanahabari kuwa kipaza sauti cha kusemea matatizo ya wengine  katika jamii, ilhali tatizo lao wamelinyamazia kimya, Dk Rose Reuben.
 
Kadhalika tunaviomba vyombo vya habari kuhakikisha vinaweka na ketekeleza sera ya jinsia ndani ya vyumba vya habari, na sera ya kupinga unyanyasaji na rushwa ya ngono na sera hizi zijulikane na wote ndani ya vyumba vya habari. 
 
Katika utafiti wa TAMWA tulibaini kuwa vyumba vingi vya habari havina sera ya jinsia wala sera za kupinga rushwa na unyanyasaji wa kingono, na vile vyenye sera hizi hazitumiki au hazijulikani na wanahabari/ wafanyakazi wengine, Dk Rose Reuben.
 
Lakini zaidi tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu sheria ya mwaka 2017 inayoangalia rushwa ya ngono mahala pa kazi. Hii itasaidia wanawake na wasichana kuifahamu  kujua kuwa uwepo wa sheria hii na namna ya kukusanya ushahidi wa madhila hayo. 
 
Lakini wakati huo huo serikali ione umuhimu wa kupeleka ajenda ya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu na hata mashuleni, ili kuwajengea uelewa watoto wa Tanzania uelewa na athari ya rushwa hii. 
 
Kwa mfano, hivi karibuni yamekuwapo matukio kadhaa ya wahadhiri kwa vyuo vikuu kuwadhalilisha kingono wanafunzi na huku video zao za utupu zikivuja. Haya na mengine mengi yapo pia katika vyombo vya habari na mahala pa kazi ikiwamo serikalini. 
 
Kwetu sisi TAMWA hili ni janga na ni muuaji wa kimya kimya wa utu wa wanawake,  endapo lisipochukuliwa hatua basi mabinti zetu vyuoni na wanataaluma katika uandishi watapoteza mwelekeo na hivyo tutapoteza vipaji na nguvu kazi, Dk Rose Reuben.
 
 
Kama kauli mbiu ya mwaka huu isemavyo, Haki Sawa kwa maendeleo Endelevu ndivyo tunavyotaka wanahabari wanawake waheshimiwe na wathaminiwe, watimize wajibu wao bila kulazimishwa au kurubuniwa kutoa rushwa ya ngono. 
 
Tunachoweza kusema TAMWA ni; Mwanahabari mwanamke anaweza kuripoti habari za uchunguzi kama mwanaume, anaweza kuripoti michezo kama mwanaume, anaweza kuripoti katika vita kama ilivyo kwa wanaume. Uanamke wake, hauondoi ujasiri, utimamu na umakini katika taaluma  yake. 
 
Kadhalika, Mwanahabari mwanamke hapimwi kwa sura wala sauti yake, bali ujuzi na kipaji katika taaluma yake ya uanahabari. 
 
TAMWA tunasisitiza kuwa hiki ni; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu kama kauli mbiu  ya mwaka huu isemavyo. 
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
 
Dk Rose Reuben
TAMWA
 

User Rating: 2 / 5

Star ActiveStar ActiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Novemba 25, 2021, Dar es Salaam. Leo Dunia inanza madhimisho ya  Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia. 
 
Maadhimisho haya  yanayobebwa na kauli mbiu isemayo; Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa yanakuja wakati ambapo takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kukithiri kwa matukio ya ukatili wa kijinsia, ikiwamo ubakaji hapa nchini.
 
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinasikitishwa na ongezeko la ukatili huu hasa kwa watoto na wanawake ambao ndio tegemeo katika mustakabali wa kimaendeleo nchini. 
 
Akiwa bungeni, Naibu Waziri wa Afya, Mwanaidi Ali Khamis alinukuliwa akisema, kati ya Januari hadi Septemba mwaka huu, watoto 6168 walifanyiwa ukatili wa kijinsia na kati yao, 3524 walibakwa. Wakati huo Naibu Waziri alisema, wanafunzi 1887 walipata ujauzito katika kipindi hicho hicho. 
 
Takwimu hizi zinaamanisha nini? Zinamaanisha kwamba, iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa basi katika kipindi cha mwaka mmoja, zaidi ya watoto 7000 watakuwa wamebakwa au watoto zaidi ya 12,000 watakuwa wamefanyiwa ukatili.
 
Takwimu hizi mpya zinaogofya na kutufanya TAMWA tuone pengine wadau, ikiwamo serikali, wazazi na walezi, tukubaliane na kutamka kuwa; Ubakaji sasa ni janga.
 
TAMWA tunaona ni wakati sahihi sasa, kwa wadau wa masuala ya ukatili wa kijinsia, kukaa pamoja na kupanga mikakati mipya na madhubuti zaidi ya kumaliza au kupunguza matukio haya kwani sheria na sera nzuri zipo lakini ukatili huo bado unaendelea katika jamii yetu. 
 
Hata hivyo tunaipongeza mahakama kwa kutoa hukumu na kufuatilia kwa ukaribu kesi hizi za ubakaji, kwani ipo mifano ya waliohukumiwa kwa kufanya matukio haya. Tunayapongeza madawati ya jinsia kwa kusimamia upelelezi na kutoa ushauri kuhusu matukio au kesi hizi za ubakaji na ukatili mwingine.  Hata hivyo bado matukio haya yanaendelea kuongezeka kila kukicha. Je tatizo lipo wapi? 
 
Ni muhimu kwa taifa, sasa kuendelea kubuni njia mbadala na mpya za kukabiliana na janga hili. Tunaliita janga kwa sababu, watoto 3524 kubakwa si lelemama, bali ni tatizo kubwa katika jamii yetu ambalo linaharibu kabisa mustakabali wa maisha ya kizazi kijacho.
 
Wakati huo huo, bado kinamama wanaendelea kupokea vipigo, kubakwa, kupewa lugha dhalilishi katika jamii yao hali inayowafanya kuwa kundi linaloomboleza na wakati mwingine kuichukia jinsia yao. 
 
"Ukatili huu, una madhara ya muda mfupi, muda mrefu, kiuchumi, kimwili na kisaikolojia kwa wanawake na wasichana na watoto wote kwa ujumla, kwani inawazuia kushiriki kikamilifu na kwa usawa katika jamii yao," Dk Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA. 
 
"Hakuna namna nyepesi ya kuelezea madhara haya ya ukatili wa kijinsia, tumewahi kuona, pengine tumesikia lakini bado jamii nzima haijajua madhara yake kwa kina labda kwa sababu, matukio haya hayatokei kwa wingi mara moja. Lakini tungewapata waathirika hawa na kuwakusanya pamoja, basi Tanzania ingelia," Dkt Reuben.
 
"Ubakaji huu wa watoto ni janga. Serikali itambue kuwa hili ni janga kwa sababu madhara yake yanaweza yasionekana kwa sasa lakini yataonekana baadaye wakati ambapo kizazi hiki cha sasa kitakapokuwa kimeshika usukani" Dkt Reuben.
 
TAMWA inaamini kuwa taifa salama ni lile linalojenga kizazi salama, ambacho waliopo wanawalinda watoto na kumlinda mwanamke. Hivyo basi, ili kuwa na jamii hiyo hatuna budi kuchagizana kwani; waswahili walisema; Kichango ni kuchagizana Kila mmoja ashiriki kwa namna yake kumaliza ukatili huu.
 
Kidunia hali ni kama hii, takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wanawake(UN-Women)zinaonyesha kuwa ukatili wa wanawake aghalabu hufanywa na mwenza, mume wa zamani au wa sasa. Inaelezwa kuwa wanawake zaidi ya milioni 640 wenye umri wa kuanzia miaka 15 na kuendelea waliwahi kufanyiwa ukatili na wenza.
 
Ukatili huu unatajwa kusababisha msongo wa mawazo, kihoro, mimba zisizotarajiwa, magonjwa ya zinaa ikiwamo UKIMWI na wakati mwingine waathirika kujiua. 
 
Takwimu hizo kadhalika zinaeleza kuwa, zaidi ya wanawake 87,000 duniani waliuawa na nusu yao, (50,000) waliuawa na mwenza au mwanafamilia. Zaidi ya thuluthi, waliuawa kwa makusudi na mwenza/mume wa sasa au wa zamani. 
 
TAMWA imeona zaidi kuwa unyanyasaji huu kwa hapa Tanzania umeendelea kujikita pia katika mashindano ya ulimbwende, vyuo vikuu, vyombo vya habari ikiwemo  mitandaonii pamoja na mahala pa kazi. Haya yote yasipofanyiwa kazi, basi tutakuwa na dunia isiyo salama kwa kundi hili.
 
"Tunampongeza Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ameonyesha wazi kuwa anasimamia vyema haki za wanawake na watoto, tumemuona na kumsikia akipinga lugha dhalilishi kwa wanawake na udunishwaji wa kundi hilo katika nafasi za siasa na uongozi. Kongole Rais wetu,"Dkt Rose Reuben
 
TAMWA hatutaacha kusimamia haki za wanawake, watoto na wanahabari, tutaendelea kupaza sauti hadi tutakapoona amani imetawala tukiendelea kusema "Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa”.
 
Kazi iendelee. 
 
Dk. Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
 

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Dar Es Salaam, October 11, 2021. Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinawakumbusha, wazazi, walezi, wadau, serikali na waandishi wa habari kuchukua hatua ili kuondoa aina mpya ya ukatili kwa njia ya mitandao ya kijamii.
 
Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike huadhimishwa duniani kote kila ifikapo Oktoba 11, ambapo kwa mwaka huu, kauli mbiu ya kitaifa na kimataifa ni: Kizazi cha Kidijitali, Kizazi Chetu!.
 
Kauli mbiu hii inalenga kuikumbusha jamii kutoa haki sawa kwa watoto wote kwenye teknolojia ya kidijitali ili waitumie  kwa Maendeleo na kwa usahihi.  
 
Zipo faida lukuki za matumizi ya mitandao ya kijamii, kama vile elimu kwa njia ya mitandao, taarifa muhimu za kitaifa na kimataifa lakini  bado watoto wa kike wameonekana kuachwa nyuma katika ulimwengu wa kidijitali kwa kukosa  fursa sawa hasa katika matumzi ya intanenti, kumiliki simu janja, na uhuru wa  kutumia mitandao ya kijamii kama ilivyo kwa watoto wa kiume. 
 
Ripoti ya Shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia masuala ya wanawake, (UN-Women) Julai mwaka huu, ilionyesha kuwa kuna ongezeko la ukatili wa kijinsia kupitia mitandao ya kijamii. 
 
Ripoti hiyo imeeleza: Upatikanaji  wa intaneti kwa watoto wa kike na wanawake, umesababisha kundi hilo kukumbana na udhalilishaji wa kingono zaidi, ukilinganisha na wanaume,
 
Kadhalika ripoti hiyo imeonyesha zaidi kuwa, watoto wa kike wamekuwa wakitishiwa kimwili, kutumiwa picha za ngono, na kupewa lugha dhalili katika mitandao ya kijamii.
 
Kwa hapa Tanzania, matukio kadhaa ya udhalilishaji wa kingono kwa njia ya mtandao yamewahi kuripotiwa ikiwamo kusambazwa kwa video za ngono zikiwaonyesha watoto wa kike, huku mwanaume akifichwa uso.
 
Aina nyingine ya ukatili wa kijinsia kwa njia ya mtandao ni kashfa na matamshi ya chuki, jina la akaunti kuibwa na  na kisha kutumiwa na watu kwa njia za utapeli au kurushwa kwa video za ngono. Hili limewakuta zaidi watoto wa kike wenye majina makubwa au maarufu katika jamii. 
 
Lakini pia, imekuwa ni tamaduni kwa watoto wa kike kurushiwa lugha dhalilishi kwa njia ya mtandao, ikiwamo zile zinazohusisha baadhi ya maungo yao ya mwili.
 
Picha za watoto wa kike zimekuwa zikisambazwa katika mitandao ya kijamii na kugeuzwa mjadala jambo ambalo limeonekana kuchangia kuongezeka kwa lugha dhalili dhidi yao.
 
Kutokana na kuongezeka kwa matukio haya yanayoendana na ongezeko la matumizi ya mitandao ya kijamii, hatuna budi kupunguza udhalilishaji huu na kuendelea kuhimiza matumizi sahihi, salama na yenye faida, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben.
 
Reuben ameomba  wazazi, walezi, serikali, asasi za kijinsia, asasi za kiraia, wapatanishi na wanahabari, kusimamia usalama wa watoto kike mitandaoni. 
 
Inawezekana tabia hizi zinaonekana kuwa ni za kawaida au kugeuzwa utamaduni lakini zimeleta madhara kwa watoto wa kike ikiwamo kukatisha masomo, kujiua, kutengwa na jamii na baadhi kuathirika kisaikolojia, Dkt, Reuben
 
TAMWA inaamini katika usawa wa kijinsia, haki za watoto na wanawake, hivyo katika kuadhimisha siku hii, tunaikumbusha serikali kutunga sheria zinazoendana na kasi ya teknolojia ili kuwabana wale watakaofanya ukatili wa kingono kwa njia ya mtandao.
 
Sheria isifumbe macho katika masuala haya, lakini si hayo tu, bado tunasisitiza hata ile sheria ya ndoa  ibadilishwe ili kumpa mtoto wa kike haki ya kusoma na kuolewa katika umri wa utu uzima Dkt. Reuben
 
TAMWA inapenda kutoa wito kwa jamii kuona umuhimu wa matumizi ya dijitali katika jamii yetu ili kuendana na uhalisia wa dunia, pia  kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kutoa na kuwezesha watoto wote kupata elimu ya masuala ya dijitali pia kurahisisha upatikanaji wa vifaa vya kidijitali  kwa kuzingatia jinsi zote bila ubaguzi.
 
TAMWA inaamini kuwa, maadhimisho ya mwaka huu, yataangazia  changamoto na fursa za kidijitali  kwa mtoto wa kike lakini bila kusahau, kuwa kumbe; malezi bora, elimu kwa mtoto wa kike ndicho chanzo cha leo kuwa na Rais wa kwanza mwanamke, ambaye ni Mama Samia Suluhu.
 
Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike ni siku ya kimataifa iliyotangazwa na Umoja wa Mataifa; pia inaitwa Siku ya Wasichana na Siku ya Kimataifa ya Wasichana. Siku hii huadhimishwa kila ifikapo Oktoba 11.
 
Umoja wa Mataifa ulianza kuadhimisha siku hii baada ya kuonekana kuna changamoto nyingi zinazomuandama mtoto wa kike ikiwamo kunyimwa fursa ya kupata elimu, ubakaji, ulawiti,  ndoa za mapema, mimba za mapema na kukosa haki nyingine ikiwamo ya kucheza na kushauri katika ngazi ya familia. 
 
Maadhimisho hayo pia yanaangalia  mafanikio ya watoto kike kidunia, ikiwamo Tanzania kama vile  kuongezeka kwa idadi ya watoto wa kike wanaopata elimu ya juu, watoto wa kike kuendelea kupata elimu ya afya ya uzazi na kufikiwa na taasisi mbalimbali zinazogusa maisha ya mtoto wa kike.
 
Kizazi cha Kidijitali, Kizazi Chetu!
 
Dkt Rose Reuben.
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Ndugu mgeni rasmi,
Wawakilishi wa FES,
Mkuu wa Dawati la Jinsia,
Mwakilishi wa Takukuru,
Wanahabari,
Nawasalimu kwa jina la JMT!
 
Dar Es Salaam, 2nd December, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Friedrich-Ebert-Stiftung (FES) Tanzania, wanaungana na watanzania wote kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.
 
Maadhimisho haya, hufanyika kila ifikapo Novemba 25 hadi Desemba 10 kila mwaka.  Kwa mwaka huu, maadhimisho haya yamepambwa na kauli mbiu isemayo: Pinga ukatili wa kijinsia Sasa 
 
Hata hivyo wakati maadhimisho haya yakiendelea, TAMWA pamoja na FES tumebaini kuwa tatizo la rushwa ya ngono mahala pa kazi linaendelea kushika mizizi katika jamii yetu. 
 
Hilo lilibainika hata wakati TAMWA ilipofanya mradi na Asasi ya Habari ya Internews mnamo mwaka 2019 na kuwashirikisha wanahabari kufanya habari za uchunguzi kuhusu rushwa ya ngono mahala pa kazi.
Makala za wanahabari hao, zilibainisha wazi, rushwa hiyo ipo lakini imegubikwa na ukimya hasa kutoka kwa waathirika. 
Kadhalika, mwaka 2021, TAMWA kwa kushirikiana na Women Fund Tanzania, (WFT) ilitekeleza mradi wa kuangazia rushwa ya ngono kwa wanahabari. TAMWA ilifanya utafiti na kubaini wanahabari wanakabiliwa kwa kiasi kikubwa na rushwa ya ngono na ukatili mwingine ndani ya vyumba vyao vya habari.
Utafiti  uliofanywa na asasi ya EBA nchini Tanzania mwaka 2020 ulibaini kuwa, suala la rushwa ya ngono linafahamika na limetanuka kuanzia katika sekta ya elimu na katika sekta ya ajira. 
 
Tatizo la rushwa ya ngono ni kubwa lakini limegubikwa na ukimya, wahanga wengi hawatoi taarifa wakiogopa kudhalilishwa zaidi, Dr Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA.
 
TAMWA tunasema, rushwa ya ngono vyuoni ndicho chanzo cha kuwa na wanafunzi wasio na tija katika sekta ya ajira, lakini pia ndicho chanzo cha kuzalisha wanaataluma wasio na sifa za kuajiriwa. 
 
Rushwa hii ya ngono mahala pa kazi na vyuoni, ndicho chanzo pia cha maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na magonjwa mengine ya zinaa, Dr Rose Reuben. 
Katika tafiti zetu, TAMWA tumegundua kuwa rushwa ya ngono hufanyika sio tu mahala pa kazi, bali wakati mwingine, hata katika kambi za wakimbizi, katika shule za sekondari.
Rushwa ya ngono hurudisha nyuma maendeleo ya mtu mmoja mmoja na nchi kwa sababu matokeo ya ukatili wa aina hii ni kurudisha nyuma ari ya utendaji kazi wa wanafunzi, wafanyakazi au waumini, Dr Rose Reuben
 TAMWA tumeona pia zipo changamoto katika kukabiliana na aina hii ya ukatili, kwanza ni ukimya. Wahanga wengi kushindwa au kuhofia kutoa ushahidi na kuzungumzia suala hili. Lakini pili, ukosefu wa takwimu zitakazowezesha wadau kufanyia kazi aina hii ya ukatili.
Ipo sheria ya makosa ya rushwa, inayogusa rushwa ya ngono, nayo ni sheria namba 11 ya mwaka 2007, kifungu cha 25. Dr Rose Reuben
 
Ukatili kwa njia ya mtandao
Wakati huo huo, tunakemea vikali ukatili kwa njia ya mtandao unaoendelea. Tumeona, tumesikia na wakati mwingine sisi ndiyo tumekuwa waanzilishi wa ukatili huu. Kutumia picha za wanawake vibaya, kutumia lugha dhalili kwa kundi Fulani mitandaoni, kutumia picha za watoto na kuweka maudhui yanayomdhalilisha. Haya ni baadhi tu ya matendo yanayochagiza ukatili wa kijinsia mitandaoni.
 
TAMWA ni wanahabari na wanahabari ni TAMWA, hivyo tunawaomba wadau wetu wa habari, mkatumie kalamu zenu kukemea rushwa ya ngono  ndani ya vyumba vyenu vya habari  na kuvaa joho la kupinga aina zote za ukatili wa kijinsia ikiwamo ule wa kwa  njia ya mtandao. 
 
Kadhalika, tunaipongeza serikali kwa kupitia wadau wake wakiwamo Takukuru, wamefanyia kazi suala la rushwa ya ngono kwa kufanya tafiti kadhaa lakini pia kwa kufanyia kazi makosa ya aina hii. Hongereni! lakini tunatamani  matokeo zaidi, kesi zaidi zipelekwe mahakamani, hukumu itolewe  ili kufanya mahala pa kazi pawe sehemu salama na penye tija. 
Pia tunampongeza  Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kuzindua mwongozo wa madawati ya rushwa ya ngono vyuoni. Tunaomba yakatumike kwa tija. 
Ewe Mwananchi, pinga ukatili wa kijinsia sasa,
 
#KaziIendelee
#ZuiaUkatiliMtandaoni
#ZuiaUkatili
 
Dr Rose Reuben
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Oktoba 29, 2021.
 
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinalaani  tukio la Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma, kudaiwa kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi na wanafunzi wa kike chuoni hapo.
 
Taarifa iliyotolewa na Chuo hicho baada ya kusambaa kwa jumbe za uwepo wa tukio hilo chuoni hapo katika mitandao ya jamii,  imeeleza kuwa Mhadhiri huyo, Petrol Mswahili, amefanya vitendo hivyo kwa wanafunzi wa kike, jambo linalodhihirisha uwepo wa rushwa ya ngono. 
 
TAMWA ikiwa ni taasisi inayopinga unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake ikiwamo rushwa ya ngono, tunalaani  tukio hilo linalovunja maadili ya utumishi wa umma na zaidi hasa kudhalilisha watoto wa kike katika taasisi hii ya elimu ya juu.
 
Kadhalika, TAMWA tunasikitishwa na  vitendo hivyo ambavyo sio tu vimekuwa chanzo cha kuharibu mustakabali wa kitaaluma wa watoto wa kike, lakini pia ndicho chanzo cha magonjwa ya kuambukiza, sonona na kurudisha nyuma kundi hilo. 
 
Mwaka 2019 TAMWA ilifanya tathmini ya kuangazia ukubwa wa rushwa ya ngono kwenye vyumba vya habari, maeneo ya kazini na taasisi za elimu ya juu, na kubaini kuwa tatizo hilo lipo kwa ukubwa wake.
 
Kadhalika TAMWA ilibaini kuwa ukimya umetawala kwa wale waathirika wa rushwa ya ngono kutokana na sababu mbalimbali ikiwamo woga wa kukosa vibarua, kufukuzwa shule au kufeli mitihani yao. 
 
Hivyo tunalaani vikali vitendo hivi huku tukiupongeza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kuchukua hatua za haraka dhidi ya mhadhiri huyo lakini pia tunaushauri uongozi wa chuo hicho kuweka mikakati itakayokomesha vitendo hivyo.
 
TAMWA inaomba pindi uchunguzi utakapokamilika basi sheria ichukue mkondo wake ili iwe funzo kwa wahadhiri wengine wanaoharibu watoto wa kike. Pia tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB) iendelee kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu rushwa ya ngono na udhalilishaji mwingine wa kijinsia. 
 
"Digrii bila rushwa ya ngono, ni digrii yenye tija"
 
Imetolewa na;
 
Mkurugenzi Mtendaji waTAMWA,
 
Dk Rose Reuben.
 

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 13, 2021. Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kuteua wanawake wawili katika Baraza la Mawaziri.
 
Uteuzi huo umefanyika jana ambapo Dkt Ashatu Kijaji ameteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na  Teknolojia ya Habari, wakati Dkt Stergomena Tax ameteuliwa kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
Uteuzi huu unafanya idadi ya mawaziri wanawake kufikia saba, kutoka watano walioteuliwa awali. 
 
TAMWA tunampongeza Rais Samia pia kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kumteua mwanamke kushika wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
"Uteuzi alioufanya Rais, wa kuongeza mawaziri wawili katika baraza unaonyesha dhahiri kuwa wanawake wanaaminika na wana uwezo wa kuleta mabadiliko katika Nyanja zote, kisiasa, kiuchumi na kijamii" Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA tunaamini kuwa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi ndiyo nguzo muhimu ya kuleta usawa na ndicho chanzo cha kuleta mabadiliko chanya katika jamii ambayo yataletwa katika usawa, haki na uwajibikaji. 
 
"Rais Samia, ameweza kuonyesha lile ambalo lilidhaniwa haliwezekani kwa kuwaweka mawaziri wanawake katika wizara nyeti  kama ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa, pia kwa kuendelea kuteua mawaziri wanawake, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala" amesema Dkt Reuben
 
Kadhalika tunampongeza Rais kwa ile kauli yake wakati akiwaapisha mawaziri hao aliposema: Nimeamua kuvunja taboo (mwiko), iliyoaminika kwamba wizara ya ulinzi lazima akae mwanaume mwenye misuli yake, kazi ya wizara ile si kupiga mizinga au kushika bunduki,  nimevunja taboo(mwiko) hiyo na kumteua dada yetu Tax kutokana na upeo wake mkubwa alioupata akiwa Jumuiya ya Nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara
 
“Hakika Rais amevunja dhana ya kuwa wanaume pekee ndiyo wenye uwezo wa kushika wizara hii, na kwa hili tunategemea Dkt Tax hatatuangusha, bali atasimamia vyema nafasi hiyo na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika masuala ya ulinzi na usalama,kwa kuwa ana uwezo na upeo" Dk Reuben 
Kadhalika TAMWA tunampongeza Rais Samia kwa kusikiliza kilio cha wanahabari na kuunganisha Wizara ya Habari, Mawasiliano na ile ya Teknolojia ya Mawasiliano, kuwa moja. 
Hatua hiyo itawafanya wadau wa habari kufanya kazi kwa ufanisi na wepesi zaidi kuliko hapo awali. 
TAMWA tunaamini kuwa Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi na katika ngazi za maamuzi ndicho chanzo cha haki, usawa na uwajibikaji na maendeleo  ya nchi. 
Wanawake Wanaweza! Kazi Iendelee!
Dkt Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

Search