Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Dar es Salaam, Novemba 12, 2020. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinalaani vikali, matukio ya ukatili wa kijinsia yanayoendelea hapa nchini katika kipindi cha miezi miwili.

Hivi karibuni, vyombo vya habari vimeripoti matukio kadhaa ya ukatili wa kijinsia hasa ubakaji wa watoto yanayoashiria kuwa bado vitendo hivi vinaendelea licha ya kuwepo sheria, matamko na sera zinazopinga vikali matukio hayo.

Miongoni mwa matukio hayo ni pamoja na lile la Novemba 11, mwaka huu, ambapo  Mwenyekiti wa Kijiji cha Ijinga, Wilaya ya Magu, Badri  Masengo (40) anayedaiwa kumpa ujauzito mwanafunzi wa darasa la sita,Shule ya Msingi Ijinga mwenye umri wa miaka 15 .

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam Agost 12, 2020. Wakati macho na masikio ya Watanzania yakiisubiri kwa hamu Oktoba 28 ambayo ni siku ya uchaguzi mkuu nchini, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF) pamoja na Global Peace Foundation (GPF) tunaoa mapendekezo kwa  vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi, kuondoa changamoto zote zinazochagiza ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
Uchaguzi Mkuu unafanyika wakati ambapo kati ya wagombea 16 waliochukua fomu kugombea urais, wapo wanawake wawili mpaka sasa ambao ni Queen Cathbert Sendinga wa Chama cha ADC, na Cecilia Augustino wa Demokrasia Makini walioteuliwa na vyama vyao kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi huo. Kadhalika, wapo wanawake watano wanaowania umakamu wa Rais, katika mchakato huu wa uchaguzi. 
Lakini TAMWA, WiLDAF  na GPF  taasisi ambazo malengo yake ni kuwepo kwa jamii yenye amani, inayoheshimu haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia, na amani zimeona ni vyema kuikumbusha jamii, wadau wa masuala ya siasa na ya jinsia  kuzifanyia kazi changamoto zinazochangia ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
 TAMWA WiLDAF  na GPF  chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake Afrika, (AWDF) kupitia mradi wa ‘Wanawake Sasa’ imeendesha midahalo mbalimbali ya wanawake kutoka  vyama vya siasa ,wakiwamo wanawake wanasiasa, viongozi wa dini na kubaini kuwa bado kuna changamoto  zinazopelekea ushiriki mdogo wa wanawake katika siasa.
Midahalo tuliyofanya  katika  kanda za Dodoma, Arusha, Zanzibar na Dar es Salaam, iliibua changamoto zinazowakabili wanawake katika siasa ikiwamo lugha dhalilishi  zinazowavunja moyo wanawake  wanaogombea au walio katika nafasi za uongozi pamoja na familia zao kuwania nafasi mbali mbali za uongozi.
Wanawake wanaogombea nafasi za uongozi, hukutana na changamoto  ya lugha dhalilishi wakati wa kampeni, na hata wakati wa utendaji wao wa kazi ili tu kuwakatisha tamaa na kuwarudisha nyuma. Kama tunataka uchaguzi wa haki na wa kidemokrasia, ni muhimu kwa tume ya uchaguzi na vyombo vya usalama kupiga marufuku na kutoa adhabu kali kwa wanasiasa watakaotoa lugha hizi dhidi ya wanawake, Rose Reuben, Mkurugenzi TAMWA.
Katika midahalo hiyo, TAMWA , WiLDAF  na GPF  tumebaini kuwepo kwa rushwa ya kifedha katika shughuli za kawaida za siasa na hasa wakati wa chaguzi mbali mbali za ndani ya vyama, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu. Hii ni pamoja na tabia za wajumbe wanaotegemewa kupiga kura kuwa na hulka ya kudai au kujenga mazingira ya kupewa kitu kidogo ili waweze kutoa ushirikiano kwa mgombea. Hii inaathiri  wanawake ambao wengi wao hawana kipato cha kutosha hasa wanawake vijana. 
 
Pia tumebaini uwepo wa vitendo vya kuomba au kutengeneza mazingira ya rushwa ya ngono kwa baadhi ya wanaume wenye dhamana za kusimamia michakato ya chaguzi au mamlaka ndani ya vyama vya siasa.Changamoto hiyo husababisha wanawake kudhalilishwa na kuharibiwa ndoto zao za kisiasa na wakati mwingine familia au wenzi wao kuwazuia kushiriki katika siasa. 
Hayo na mengine mengi, yanachangia wanawake, kuvunjika moyo na hivyo kutoshiriki shughuli za siasa au kukosa nafasi za uongozi pale wanapokuwa na msimamo wa kutotoa rushwa.
Katika hili tunapenda kutoa rai kwa wanawake wenzetu kukataa kabisa kudhalilishwa na kutojihusisha na vitendo vya rushwa ya fedha au ngono na pia tunashauri jumuiya za wanawake ndani ya vyama vya sisasa kuvunja ukimya na kuhakikisha hoja za rushwa katika siasa inazungumzwa katika kila vikao vya jumuiya na vikao vingine muhimu. 
Pia tunaviomba vyama vya siasa viweke utaratibu madhubuti na wa siri wa kutoa taarifa za vitendo hivi na kuwe na kamati huru ndani ya vyama zisizofungamana na yeyote zitakazoratibu upokeaji, ufuatiliaji na utoaji adhabu kwa wale ambao bado wanaendekeza vitendo hivi vya kuwadhalilisha wanawake.   
Changamoto nyingine zilizoibuliwa katika midahalo hiyo,  ni Ilani za vyama vya siasa ambazo hazitoi nafasi kwa wanawake kuwa viongozi na kupata nafasi ya kugombea katika majimbo. Tumebaini wanawake wengi wanashindwa kushiriki uchaguzi kwa kutopata baraka hii kuanzia ndani ya vyama.
Wakati huo huo tunavitaka, vyama hivyo viwachague wanawake wenye uwezo wa kisiasa na wa uongozi.
Tunapenda kuvipongeza vyama vya siasa ambavyo vimetoa nafasi za wanawake kugombea nafasi za udiwani na ubunge na hata urais katika kura za maoni. 
“Mwaka huu wanawake wengi wamejitokeza. Tungependa kuviomba vyama vya siasa kuhakikisha kuwa wale wanawake wenye uwezo wasimamishwe kugombea nafasi hizo na tunawaomba wananchi wote kuwachagua wanawake waliosimamishwa kugombea nafasi za ubunge na udiwani, na wengine wapewe nafasi za teuzi mbalimbali Mkurugenzi wa GPF , Martha Nghambi. 
Tunavikumbusha vyama kuendelea kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake ambao hawakupata nafasi mwaka huu ili waweze kusimama na kugombea chaguzi zijazo ndani ya vyama vyao, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
Kadhalika tunapenda kuwaasa wanawake kuepuka kugawanywa na zile kauli kuwa, hawapendani badala yake waendelee kushirikiana na kupeana fursa mbalimbali za kisiasa, kiuchumi na masuala ya kijamii.
Kauli hizi za kuwa wanawake hatupendani si za kweli bali zimekuwa zikitumika katika jamii kuwagawa wanawake kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, Reuben 
Tunatarajia kuwa serikali, wadau wa siasa, vyombo vya usalama vitazingatia kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DK John   Pombe Magufuli ya kuwepo kwa mazingira wezeshi kwa wanawake katika uchaguzi mkuu na katika nafasi za uongozi na maamuzi. Pia tunampongeza kwa kuendelea kumchagua Mama Samia Suluhu kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao. 
 
Tungependa kumalizia kwa kusisitiza kauli zilizotolewa na Rais, viongozi wa vyama mbali mbali na tume ya taifa ya uchaguzi kuwa uchaguzi wa mwaka huu utakuwa ni  huru, haki na wa amani. 
Tunawakumbusha wagombea wote kuhakikisha kuwa hawatoi kauli zozote za uvunjifu wa Amani, kuchochea vurugu, kuwagawa watu kwa dini au makabila yao au matusi na udhalilishaji wa kijinsia kwa wagombea wengine. 
Wakati huo, TAMWA, WiLDAF na GPF  inaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuendelea kuhimiza uchaguzi huru, wa haki na usawa na kutengenezwa kwa mazingira sawa ya ushindani kwa wagombea wote.
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ubariki Uchaguzi Mkuu wa Octoba 2020. 
 
Rose Reuben Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
Anna Kulaya Mkurugenzi - WILDAF
Martha Nghambi Mkurugenzi - GPF

User Rating: 2 / 5

Star ActiveStar ActiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Novemba 25, 2021, Dar es Salaam. Leo Dunia inanza madhimisho ya  Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia. 
 
Maadhimisho haya  yanayobebwa na kauli mbiu isemayo; Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa yanakuja wakati ambapo takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kukithiri kwa matukio ya ukatili wa kijinsia, ikiwamo ubakaji hapa nchini.
 
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinasikitishwa na ongezeko la ukatili huu hasa kwa watoto na wanawake ambao ndio tegemeo katika mustakabali wa kimaendeleo nchini. 
 
Akiwa bungeni, Naibu Waziri wa Afya, Mwanaidi Ali Khamis alinukuliwa akisema, kati ya Januari hadi Septemba mwaka huu, watoto 6168 walifanyiwa ukatili wa kijinsia na kati yao, 3524 walibakwa. Wakati huo Naibu Waziri alisema, wanafunzi 1887 walipata ujauzito katika kipindi hicho hicho. 
 
Takwimu hizi zinaamanisha nini? Zinamaanisha kwamba, iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa basi katika kipindi cha mwaka mmoja, zaidi ya watoto 7000 watakuwa wamebakwa au watoto zaidi ya 12,000 watakuwa wamefanyiwa ukatili.
 
Takwimu hizi mpya zinaogofya na kutufanya TAMWA tuone pengine wadau, ikiwamo serikali, wazazi na walezi, tukubaliane na kutamka kuwa; Ubakaji sasa ni janga.
 
TAMWA tunaona ni wakati sahihi sasa, kwa wadau wa masuala ya ukatili wa kijinsia, kukaa pamoja na kupanga mikakati mipya na madhubuti zaidi ya kumaliza au kupunguza matukio haya kwani sheria na sera nzuri zipo lakini ukatili huo bado unaendelea katika jamii yetu. 
 
Hata hivyo tunaipongeza mahakama kwa kutoa hukumu na kufuatilia kwa ukaribu kesi hizi za ubakaji, kwani ipo mifano ya waliohukumiwa kwa kufanya matukio haya. Tunayapongeza madawati ya jinsia kwa kusimamia upelelezi na kutoa ushauri kuhusu matukio au kesi hizi za ubakaji na ukatili mwingine.  Hata hivyo bado matukio haya yanaendelea kuongezeka kila kukicha. Je tatizo lipo wapi? 
 
Ni muhimu kwa taifa, sasa kuendelea kubuni njia mbadala na mpya za kukabiliana na janga hili. Tunaliita janga kwa sababu, watoto 3524 kubakwa si lelemama, bali ni tatizo kubwa katika jamii yetu ambalo linaharibu kabisa mustakabali wa maisha ya kizazi kijacho.
 
Wakati huo huo, bado kinamama wanaendelea kupokea vipigo, kubakwa, kupewa lugha dhalilishi katika jamii yao hali inayowafanya kuwa kundi linaloomboleza na wakati mwingine kuichukia jinsia yao. 
 
"Ukatili huu, una madhara ya muda mfupi, muda mrefu, kiuchumi, kimwili na kisaikolojia kwa wanawake na wasichana na watoto wote kwa ujumla, kwani inawazuia kushiriki kikamilifu na kwa usawa katika jamii yao," Dk Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA. 
 
"Hakuna namna nyepesi ya kuelezea madhara haya ya ukatili wa kijinsia, tumewahi kuona, pengine tumesikia lakini bado jamii nzima haijajua madhara yake kwa kina labda kwa sababu, matukio haya hayatokei kwa wingi mara moja. Lakini tungewapata waathirika hawa na kuwakusanya pamoja, basi Tanzania ingelia," Dkt Reuben.
 
"Ubakaji huu wa watoto ni janga. Serikali itambue kuwa hili ni janga kwa sababu madhara yake yanaweza yasionekana kwa sasa lakini yataonekana baadaye wakati ambapo kizazi hiki cha sasa kitakapokuwa kimeshika usukani" Dkt Reuben.
 
TAMWA inaamini kuwa taifa salama ni lile linalojenga kizazi salama, ambacho waliopo wanawalinda watoto na kumlinda mwanamke. Hivyo basi, ili kuwa na jamii hiyo hatuna budi kuchagizana kwani; waswahili walisema; Kichango ni kuchagizana Kila mmoja ashiriki kwa namna yake kumaliza ukatili huu.
 
Kidunia hali ni kama hii, takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wanawake(UN-Women)zinaonyesha kuwa ukatili wa wanawake aghalabu hufanywa na mwenza, mume wa zamani au wa sasa. Inaelezwa kuwa wanawake zaidi ya milioni 640 wenye umri wa kuanzia miaka 15 na kuendelea waliwahi kufanyiwa ukatili na wenza.
 
Ukatili huu unatajwa kusababisha msongo wa mawazo, kihoro, mimba zisizotarajiwa, magonjwa ya zinaa ikiwamo UKIMWI na wakati mwingine waathirika kujiua. 
 
Takwimu hizo kadhalika zinaeleza kuwa, zaidi ya wanawake 87,000 duniani waliuawa na nusu yao, (50,000) waliuawa na mwenza au mwanafamilia. Zaidi ya thuluthi, waliuawa kwa makusudi na mwenza/mume wa sasa au wa zamani. 
 
TAMWA imeona zaidi kuwa unyanyasaji huu kwa hapa Tanzania umeendelea kujikita pia katika mashindano ya ulimbwende, vyuo vikuu, vyombo vya habari ikiwemo  mitandaonii pamoja na mahala pa kazi. Haya yote yasipofanyiwa kazi, basi tutakuwa na dunia isiyo salama kwa kundi hili.
 
"Tunampongeza Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ameonyesha wazi kuwa anasimamia vyema haki za wanawake na watoto, tumemuona na kumsikia akipinga lugha dhalilishi kwa wanawake na udunishwaji wa kundi hilo katika nafasi za siasa na uongozi. Kongole Rais wetu,"Dkt Rose Reuben
 
TAMWA hatutaacha kusimamia haki za wanawake, watoto na wanahabari, tutaendelea kupaza sauti hadi tutakapoona amani imetawala tukiendelea kusema "Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa”.
 
Kazi iendelee. 
 
Dk. Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
 

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Abeda Rashid Abdallah.....
Ndugu wadau wa masuala ya jinsia.
Viongozi wa serikali,
Wanahabari, 
Itifaki imezingatiwa!
 
Zanzibar, February 4, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kina furaha kubwa kupata fursa hii adhimu,  leo Februari 4th, 2021, ya kukutana tena na wadau wake muhimu walioshiriki katika utekelezaji wa mradi wa Wanawake Sasa’ uliofadhiliwa na taasisi ya kimataifa ya African Women, Development Fund (AWDF).
 
Mradi wa ‘Wanawake Sasa’ umehitimishwa kwa mafanikio makubwa na kamwe mafanikio hayo yasingepatikana bila nyinyi wadau muhimu ambao mlishiriki katika kuhimiza Amani, ushirikiano  katika chaguzi na ushiriki wa wanawake katika siasa, uongozi na maamuzi.
 
Kutokana na ushirikiano wenu, tumeona namna ambavyo Rais, John Maguuli ameendelea kuteua viongozi wanawake, na hilo limethibitishwa katika kauli yake aliyoitoa Novemba, 2020 mara baada ya uchaguzi kuwa; ataendelea kuwaamini wanawake. 
Kwa msingi huo napenda nitumie fursa hii kuahidi kuwa, serikali ninayoiongoza itaendelea kuwaamini wanawake katika kushika nafasi mbalimbali za uongozi, alisema Rais JPM.
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
Si hayo tu, tumeona kivitendo, ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi na tumeshuhudia idadi ya wanawake zaidi ya 230 katika bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwamo mawaziri wanawake.
Kwa upande wa Zanzibar, tuliona uthubutu wa kinamama wawili, waliojitokeza na kuchukua fomu za kuwania urais. 
 
Ndugu mgeni rasmi,
TAMWA inaishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) na ile ya bara kwa kushiriki katika matukio ya utekelezaji wa mradi huu katika maeneo manne, ikiwamo Zanzibar, Arusha, Dar es Salaam na Dodoma. 
 
Viongozi wa Serikali wameshiriki kwa kiasi kikubwa katika kufungua, kutoa nasaha na kutoa ushauri kwa TAMWA katika ajenda hii ya ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi, Amani na mshikamano. Tunawashukuru!
 
Ndugu Mgeni Rasmi
Kupitia midahalo ya wanawake wanasiasa iliyofanywa katika maeneo yetu manne ya mradi, wanawake wanasiasa zaidi ya 150 kutoka vyama mbalimbali vya siasa nchini,  walipata fursa ya kujifunza umuhimu wa kutumia vyombo vya habari kueneza ajenda zao za kisiasa.
 
Pia kupitia midahalo hiyo, waliweza kujifuza changamoto za kila mmoja hasa katika mrengo wa ukatili wa kijinsia, ikiwamo rushwa ya ngono na kujua namna ya kukabiliana na changamoto za aina hiyo.
Wanawake wanasiasa waliopata mafunzo waliteuliwa kuanzia ngazi ya kanda hadi kitaifa. 
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
TAMWA iliwaleta pamoja viongozi wa dini 50 kutoka maeneo hayo manne ambao walishiriki kikamilifu kueneza Amani wakati wa uchaguzi na kusisitiza ushiriki wa wanawake katika siasa, uongozi na maamuzi. Haya kwetu ni mafanikio kwani, nafasi ya viongozi wa dini katika kuhubiri Amani na kuwaleta watu pamoja, vilisaidia katika kufanyika kwa uchaguzi wa Amani, huru na wa haki. 
 
Ndugu mgeni rasmi, 
Kama ujuavyo TAMWA inatumia silaha yake kuu, ambayo ni vyombo vya habari katika kufikisha ajenda kwa jamii, na hivyo iliwapa mafunzo wanahabari zaidi ya 70 kutoka katika maeneo hayo manne. Wanahabari hao walifundishwa na kupata ujuzi kuhusu umuhimu wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi.
 
Wanahabari hao baada ya mafunzo walifanikisha kuchapishwa kwa Makala za magazeti 40, vipindi vya redio  na televisheni, talk show na kuongeza wigo wa  idadi ya wanahabari tuliofanya nao kazi awali na kuwafikia wa wanahabri zaidi kutoka Zanzibar, Arusha hadi  Dodoma ambao waliandaa Makala za kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi. 
 
Ndugu mgeni rasmi, 
TAMWA na wanahabari kupitia kazi zao, walishirikiana na kuwafikia wanawake ambao awali waliogopa kushiriki katika siasa na uongozi. Hii iliongeza idadi ya wanawake waliojitokeza kuwania nafasi za uongozi kuanzia ngazi za chini hadi nafasi za ubunge. 
 
Taarifa fupi ya mradi Wanawake Sasa
Wanawake Sasa ni mradi uliotekelezwa kwa ushirikiano wa asasi tatu, TAMWA, WiLDAF na GPF Tanzania, chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake wa Afrika (AWDF).
Mradi huu ulikuwa na malengo makuu matatu, kuongeza idadi ya wanawake katika nafasi za uongozi na maamuzi, kwa kuwahamasisha na kuwawezesha wanawake, wanawake wenye ulemavu na vijana kuwa viongozi.
 
Lengo la pili, ni kuwahamasisha na kuwawezesha wanawake katika vyama vya siasa kuwania nafasi za uongozi katika vyama vyao. 
Lengo la tatu ni, kukuza wanawake kisiasa, kuhamasisha Amani katika chaguzi kupitia vyombo vya habari kwa kuishirikisha jamii. Mradi huu wa mwaka mmoja, ulianza kutekelezwa Januari Novemba 2020 na utekelezaji wake ulivihusisha vyama vitano vya siasa (CCM,ACT WAZALENDO,CUF,CHADEMA NA NCCR-MAGEUZI) katika kanda nne Arusha, Dar es Salaam, Dodoma na Zanzibar.
 
Mkurugenzi Mtendaji,
 
Rose Reuben.
 
TAMWA.

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Ndugu mgeni rasmi,
Wawakilishi wa FES,
Mkuu wa Dawati la Jinsia,
Mwakilishi wa Takukuru,
Wanahabari,
Nawasalimu kwa jina la JMT!
 
Dar Es Salaam, 2nd December, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Friedrich-Ebert-Stiftung (FES) Tanzania, wanaungana na watanzania wote kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.
 
Maadhimisho haya, hufanyika kila ifikapo Novemba 25 hadi Desemba 10 kila mwaka.  Kwa mwaka huu, maadhimisho haya yamepambwa na kauli mbiu isemayo: Pinga ukatili wa kijinsia Sasa 
 
Hata hivyo wakati maadhimisho haya yakiendelea, TAMWA pamoja na FES tumebaini kuwa tatizo la rushwa ya ngono mahala pa kazi linaendelea kushika mizizi katika jamii yetu. 
 
Hilo lilibainika hata wakati TAMWA ilipofanya mradi na Asasi ya Habari ya Internews mnamo mwaka 2019 na kuwashirikisha wanahabari kufanya habari za uchunguzi kuhusu rushwa ya ngono mahala pa kazi.
Makala za wanahabari hao, zilibainisha wazi, rushwa hiyo ipo lakini imegubikwa na ukimya hasa kutoka kwa waathirika. 
Kadhalika, mwaka 2021, TAMWA kwa kushirikiana na Women Fund Tanzania, (WFT) ilitekeleza mradi wa kuangazia rushwa ya ngono kwa wanahabari. TAMWA ilifanya utafiti na kubaini wanahabari wanakabiliwa kwa kiasi kikubwa na rushwa ya ngono na ukatili mwingine ndani ya vyumba vyao vya habari.
Utafiti  uliofanywa na asasi ya EBA nchini Tanzania mwaka 2020 ulibaini kuwa, suala la rushwa ya ngono linafahamika na limetanuka kuanzia katika sekta ya elimu na katika sekta ya ajira. 
 
Tatizo la rushwa ya ngono ni kubwa lakini limegubikwa na ukimya, wahanga wengi hawatoi taarifa wakiogopa kudhalilishwa zaidi, Dr Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA.
 
TAMWA tunasema, rushwa ya ngono vyuoni ndicho chanzo cha kuwa na wanafunzi wasio na tija katika sekta ya ajira, lakini pia ndicho chanzo cha kuzalisha wanaataluma wasio na sifa za kuajiriwa. 
 
Rushwa hii ya ngono mahala pa kazi na vyuoni, ndicho chanzo pia cha maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na magonjwa mengine ya zinaa, Dr Rose Reuben. 
Katika tafiti zetu, TAMWA tumegundua kuwa rushwa ya ngono hufanyika sio tu mahala pa kazi, bali wakati mwingine, hata katika kambi za wakimbizi, katika shule za sekondari.
Rushwa ya ngono hurudisha nyuma maendeleo ya mtu mmoja mmoja na nchi kwa sababu matokeo ya ukatili wa aina hii ni kurudisha nyuma ari ya utendaji kazi wa wanafunzi, wafanyakazi au waumini, Dr Rose Reuben
 TAMWA tumeona pia zipo changamoto katika kukabiliana na aina hii ya ukatili, kwanza ni ukimya. Wahanga wengi kushindwa au kuhofia kutoa ushahidi na kuzungumzia suala hili. Lakini pili, ukosefu wa takwimu zitakazowezesha wadau kufanyia kazi aina hii ya ukatili.
Ipo sheria ya makosa ya rushwa, inayogusa rushwa ya ngono, nayo ni sheria namba 11 ya mwaka 2007, kifungu cha 25. Dr Rose Reuben
 
Ukatili kwa njia ya mtandao
Wakati huo huo, tunakemea vikali ukatili kwa njia ya mtandao unaoendelea. Tumeona, tumesikia na wakati mwingine sisi ndiyo tumekuwa waanzilishi wa ukatili huu. Kutumia picha za wanawake vibaya, kutumia lugha dhalili kwa kundi Fulani mitandaoni, kutumia picha za watoto na kuweka maudhui yanayomdhalilisha. Haya ni baadhi tu ya matendo yanayochagiza ukatili wa kijinsia mitandaoni.
 
TAMWA ni wanahabari na wanahabari ni TAMWA, hivyo tunawaomba wadau wetu wa habari, mkatumie kalamu zenu kukemea rushwa ya ngono  ndani ya vyumba vyenu vya habari  na kuvaa joho la kupinga aina zote za ukatili wa kijinsia ikiwamo ule wa kwa  njia ya mtandao. 
 
Kadhalika, tunaipongeza serikali kwa kupitia wadau wake wakiwamo Takukuru, wamefanyia kazi suala la rushwa ya ngono kwa kufanya tafiti kadhaa lakini pia kwa kufanyia kazi makosa ya aina hii. Hongereni! lakini tunatamani  matokeo zaidi, kesi zaidi zipelekwe mahakamani, hukumu itolewe  ili kufanya mahala pa kazi pawe sehemu salama na penye tija. 
Pia tunampongeza  Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kuzindua mwongozo wa madawati ya rushwa ya ngono vyuoni. Tunaomba yakatumike kwa tija. 
Ewe Mwananchi, pinga ukatili wa kijinsia sasa,
 
#KaziIendelee
#ZuiaUkatiliMtandaoni
#ZuiaUkatili
 
Dr Rose Reuben
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
WAJIBIKA KULINDA UTU WA MWANAMKE UPATE KURA YAKE
01/09/2020
Wanamtandao wa Katiba, Uchaguzi na Uongozi ambao ni watetezi wa haki za wanawake na wasichana, yakiwemo masuala ya kukuza ushiriki wao katika uongozi wa kisiasa,    na pia tukiwa ni  wadau wakuu wa uchaguzi kama wapiga kura na wagombea katika nafasi mbalimbali za uchaguzi. Tumekuwa  tukifuatilia  kwa ukaribu mkubwa sana mchakato mzima wa uchaguzi tangu ulipoanza na matukio mbalimbali ambayo tayari yameshajitokeza ikiwemo utumiaji wa lugha za matusi na kauli mbaya za udhalilishaji dhidi ya wanawake wanaogombea na wafuasi wa vyama kwa ujumla. Kwa mfano, kumekuwepo na lugha za kutukana Wanawake wagombea wakiitwa “Malaya”, n.k 
 
Ni vema tutambue kwamba kasumba hii mbali na kwamba ni kinyume na haki za binadamu na ni kosa kisheria, inarudisha nyuma jitihada za serikali katika kufikia usawa wa kijinsia na kurudisha nyuma ari ya wanawake wengi kugombea nafasi za uongozi kwa sababu ya kuogopa kudhalilishwa. Halikadhalika,  inanyamazisha sauti za wanawake ambao ni zaidi ya nusu ya watanzania wote ambao ni wapiga kura wakuu na ambao wanahaki ya ushirki salama katika masuala ya kisiasa, suala ambalo halina tija kwa taifa letu. Kutokana na hali hii, tunaona umuhimu wa vyombo na mamlaka zinavyohusika kuwawajibisha kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi kwa wote wanaotumia matusi na lugha za kudhalilisha wanawake.
 
 Sisi, Wanamtandao watetezi wa haki za wanawake nchini, tunachukulia matukio haya kama kuvunjwa kwa Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977), inayokataza ubaguzi wa aina yoyote, na  tunaikumbusha jamii  kwamba Kanuni ya Makosa ya Adhabu, Sura ya 16, kifungu cha 89 kinataja kutumia lugha chafu dhidi ya mtu mwingine kuwa ni kosa la jinai. 
 
Tunaomba Umma wa Watanzania na Vyombo mbalimbali vinavyosimamia uchaguzi wa taifa hili utambua kwamba, ushiriki wa wanawake katika michakato ya uchaguzi ni haki yao ya kikatiba, na zimebainishwa katika sheria mbalimbali za nchi. 
 
Tume ya Taifa ya Uchaguzi huweka  wazi Kanuni mbalimbali za uchaguzi na Maadili ya vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi kwa  lengo la kuweka mazingira wezeshi kwa Watanzania wote, wakike na wakiume, kushiriki katika mchakato huu wa uchaguzi na kutoa mchango wao, kwa uhuru, uwazi na amani. Vile vile, Sheria ya Vyama vya Siasa, iliyorekebishwa mwaka 2018, katika kifungu chake cha 9, inakataza viongozi na wanachama wake kutamka au kutumia lugha za matusi, maneno ya kudhalilisha, uchochezi, au alama ambazo zinaweza kusababisha au kuhatarisha amani na ukosefu wa umoja wa kitaifa.
 
 Vilevile  Kanuni za  maadili ya Uchaguzi zilizotolewa katika Gazeti la Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania la tarehe 5/06/2020 zimebainisha mambo yaliyokatazwa kufanywa na vyama vya siasa kifungu ca 2.2 (b)  kinakataza kutumia lugha ya matusi, kashfa, kejeli, udhalilishaji na vitisho au lugha inayochochea uvunjfu wa amani au kuashiria ubaguzi wa jinsia, ulemavu, rangi au maumbile kwenye mikutano na kwenye shughuli zote za kampeni.
 
Kwa kuzingatia hili katazo, na kwa kuzingatia haki zetu za kikatiba na sheria za nchi, Sisi kama watetezi wa  haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa nchini, tunataka yafuatayo yazingatiwe ili kutokomeza udhalilishaji wa wanawake hasa kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi mkuu: 
Tunazitaka mamlaka zinazohusika (Tume ya Uchaguzi, Msajili wa Vyama Vya Siasa, na Taasisi nyingine husika kuwachukulia hatua kali kwa wagombea, pamoja na wapambe wao, wanaotoa lugha za kudhallisha na kutukana wanawake kwenye kampeni au mahali popote wakati huu wa uchaguzi m
Tunawataka viongozi wa taasisi mbalimbali zikiwemo za dini, na hasa vyama vya siasa, Asasi za Kiaraia, na Jamii yote kwa ujumla ya Tanzania kukemea vikali tabia hizi za kudhalilisha wanawake hasa kipindi hiki cha uchaguzi.
 
Vyama vya Siasa vitambue kwamba vina wajibu wa kulinda, kutetea na kudumisha haki na usawa wa Wanawake ndani ya vyama vyao na katika jamii kwa ujumla, kwa kuwa Wanawake ndiyo kundi kubwa la wapiga kura Tanzania. Kwahiyo lazima viheshimu UTU wa mwanamke  na kutoa fursa na kuweka mazingira yaliyo ya wazi na wezeshi ili wanawake wengi washiriki kikamilifu katika kutimiza haki yao ya kikatiba kama wagombea  na wapiga kura.
 
Mwisho na siyo kwa daraja, sisi wanawake wote kwa ujumla wetu, bila kujali Imani za kiitikadi, tukemee, tukatae na kuwajibisha wale wote wenye kutudhalilisha kwa njia yoyote ile, ikiwa ni pamoja na kututukana  
 
Tunawataka wanahabari na vyombo vya Habari kutumia taaluma yao vizuri kutetea UTU, HAKI ya mwanamke na hususani kipindi hiki cha uchaguzi. Vyombo vya Habari visishiriki katika kusambaza taarifa zenye lugha za matusi na udahlili zilizodhamiria katika kumdalilisha mwanamke wa Taifa hili.
 
 
Tamko hili la kukemea lugha za matusi dhidi ya wanawake ni mwendelezo wa matamko ambayo Wanamtandao tumeshayatoa tangu uchaguzi huu uanze. TUNALAANI NA KUKEMEA KWA NGUVU ZOTE MATUMIZI YA LUGHA ZA MATUSI, LUGHA ZA KEJELI, UDHALILISHAJI,  KATIKA KIPINDI CHOTE CHA UCHAGUZI
 
 
Imetolewa leo Septemba 1, 2020
Mtandao wa Wanawake Katiba Uchaguzi na Uongozi.

Search