Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Mheshimiwa Mgeni Rasmi Mkuu wa Mkoa Wa Mjini Magharibi,
Waheshimiwa Maaskofu, Masheikh, Wachungaji na viongozi mbalimbali wa dini.
Waheshimiwa viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa, viongozi mwa serikali, wakuu wa vyombo vya usalama na taasisi mbali mbali.
 
Itifaki imezingatiwa!
 
Tunaanza kwa salamu maalum isemayo:
 
Dini mbalimbali, Amani na Upendo, Amani na upendo, Dini mbalimbali.
 
Awali ya yote tuchukue nafasi hii kumshukuru mwenyezi Mungu aliye mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema hata kuifikia siku hii ya leo tukiwa wazima na kukutana kwa pamoja viongozi wa dini na viongozi wa vyama vya siasa kwa ajili ya Warsha hii muhimu kwetu sisi na Taifa letu pendwa la Tanzania. 
Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Kamati za Amani tunachukua nafasi hii kwa upekee kuwashukuru wenzetu wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kuona umuhimu wa viongozi wa dini katika kutoa mchango wetu kwa viongozi wa vyama vya siasa na jamii hususan juu ya nafasi ya mwanamke tunapoelekea katika uchaguzi mkuu Oktoba, 2020.
 
Ndugu mgeni Rasmi, lengo la Warsha hii pamoja na kuielimisha jamii juu ya umuhimu wa kufanya uchaguzi wa haki, kuheshimiana, amani na utulivu lakini pia ni kuona ni kwa namna gani jamii inapaswa kuzingatia umuhimu wa kuchagua viongozi  wenye sifa, ikiwamo kuzingatia nafasi ya mwanamke. 
 
Ndugu mgeni Rasmi na wana warsha, ni ukweli ulio wazi kuwa wanawake wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali hasa katika uwakilishi wa nafasi za uongozi kutokana na mfumo wa dume uliojengeka miongoni mwa jamii. Hatusemi wapewe tu uongozi kwa sababu ni wanawake bali kwa uwezo walio na ufanisi walionao. 
Wengi tunashuhudia sehemu kubwa ya jamii inamwangalia mwanamke kwa dhana tofauti na wakati mwingine kumtolea hukumu na kuonekana kama kiumbe kisichoweza kuleta maendeleo katika jamii yake. Jambo lililo kinyume hata na mafundisho yetu katika vitabu vyetu vitakatifu. 
Kwa mfano, maandiko ya Biblia yanashuhudia kwamba katika historia ya ukombozi kutoka Agano la Kale, hadi Agano Jipya tunaiona nafasi ya mwanamke jinsi alivyoshiriki katika utume na kukamilisha historia ya ukombozi wa mwanadamu kama tunavyoweza kuona  mifano mbalimbali ya wanawake jasiri na wenye uthubutu kama vile; Debora, Ester, Mariamu Magdalene na wenzake. Pia Qur’an tukufu nayo inasisitiza.
Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012, takwimu zinaonyesha wanawake ni zaidi ya asilimia 51. Hata hivyo, ni asilimia 30 tu ya wanawake wanaoshiriki katika uongozi kwenye vyama vya siasa, Serikali, Bunge, Mahakama na katika nafasi nyingine za uongozi katika jamii.
Sote tunafahamu Tanzania imeridhia Mikataba na Matamko mbalimbali ya Kimataifa yanayotoa haki kwa kila mtu kushiriki katika utawala wa nchi, haki za kisiasa na kiraia na mingine inayotoa miongozo ya ushiriki sawa wa kijinsia. Hii ni pamoja na Tamko la Kimataifa kuhusu Haki za Binadamu (UDHR: 1948), Mkataba wa Kimataifa wa kutokomeza aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake (CEDAW: 1979, Ibara namba 7: a,b na c).
Mapendekezo ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC 1325(2000) Mpango Kazi wa Beijing (1995), Malengo ya Millenia ya Maendeleo (Lengo la 13), pamoja  na Mkataba wa Afrika kuhusu haki za Binadamu ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Ziada wa Maputo.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) pamoja na mapendekezo ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (2014/15)pamoja na Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia (URT: 2000) zimebainisha haki za wanawake kushiriki katika nafasi mbalimbali za uongozi. 
Hata hivyo, pamoja na dhamira ya Serikali ya kufikia usawa wa kijinsia katika uongozi yaani 50 kwa 50, hali halisi inaonyesha bado wanawake wako nyuma katika nafasi za uongozi. 
Mkuu wa kitengo cha Wanawake katika Umoja wa Mataifa, Phumzile Mlambo-Ncguka, aliwahi kusema “Usawa baina ya wanawake na wanume ni ndoto ambayo bado inakwepwa” 
Ni katika mazingira hayo sisi Viongozi wa Dini na Viongozi wa Kamati ya Amani tupo mstari wa mbele katika kuhamasisha jamii  kuona umuhimu wa kutekeleza kwa vitendo juu ya nafasi ya uongozi kwa mwanamke.
Zipo sababu nyingi zenye kumkwamisha mwanamke katika nafasi ya uongozi na moja kati ya vikwazo vya mwanamke kupata uongozi ni mfumo dume ndani ya vyama vya siasa. 
Imebainika kwamba, vyama vingi vya siasa vinawatumia wanawake katika shughuli za uhamasishaji katika kuongeza idadi ya wanachama na kueneza sera za chama ikiwemo wakati wa kampeni katika kuwavuta wapiga kura lakini kwa asilimia kubwa haimuoni mwanamke kama ni mdau kwa ajili ya nafasi ya uongozi na kushika nafasi ya nguvu ya kimaamuzi.  
Vikwazo hivi  ni pamoja na nguvu ndogo ya mwanamke kiuchumi, rushwa, lugha dhalilishi, mila potofu, na wakati mwingine hii imesababisha baadhi ya wanawake  washindwe kujiamini katika kukabiliana na vitendo mbalimbali vya ukatili wa kijinsia.
Hata hivyo pamoja na changamoto hizo sote tumekuwa tukishuhudia namna ambavyo wanawake kadhaa ambao walipata fursa ya kuongoza waliweza kuongoza kwa ustadi na weledi mkubwa wakati mwingine kuliko hata wanaume. 
Miongoni mwao ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Hassan Suluhu, Spika wa zamani wa Bunge, Mama Anna Makinda, Aliyekuwa Naibu Spika, Dk. Tulia Akson na mawaziri, wakuu wa Mikoa na Wilaya na wengine wengi pasipo kumsahau mama yetu Asha-Rose Migiro ambaye aliipeperusha Bendera ya Taifa letu katika anga za kimataifa akiwa kama Naibu wa katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na ambaye kwa sasa pia ameteuliwa kama Balozi wa Tanzania chini Uingereza, nafasi ambayo anaisimamia kwa uweledi mkubwa.
Haya yote na mengine mengi yanadhihirisha wanawake ni watu wenye nguvu na uwezo katika uongozi hivyo wapewe nafasi kwa kuwachagua kwa ajili ya maendeleo ya Taifa hili, tukiamini wazi wataendeleza  vita ya rushwa, ufisadi, dawa za kulevya na mengine mengi kwa ustawi wa Taifa letu ikiwamo kusimamia haki za wanyonge.
 
Sisi Kamati ya Amani na Viongozi wa Dini tunaendelea  kusisitiza umuhimu wa nafasi ya mwanamke katika uongozi juu ya nafasi mbalimbali kwani wanawake wana mchango mkubwa katika kuinua uchumi kama tunavyofahamu mchango wa wanawake katika ukuaji wa uchumi kwa nchi yetu na kwa Afrika kwa ujumla. 
Kamati ya Amani tunaamini wanawake wakichaguliwa katika nafasi za uongozi watakuwa na fursa ya kutunga sera na kushiriki katika vyombo vya maamuzi, hivyo basi ni wazi maendeleo na mapinduzi makubwa ya kiuchumi katika Taifa letu pendwa la Tanzania yatatokea.
 Ikumbukwe kwamba wanawake ni zaidi ya nusu ya idadi ya watu duniani hivyo ili kuutokomeza umasikini ni lazima wanawake wapewe nafasi na kushirikishwa kikamilifu katika uongozi. Biblia inasema “Wanawake watangazao habari ni jeshi kubwa” (Zaburi 68:11b) hivyo ni wazi wanayo nguvu ya kufanikisha hili.  
Lakini pia upo msemo uliozoeleka kwa wengi kwamba “kila palipo na maendeleo ya mwanaume nyuma yake yupo mwanamke” hivyo mwanamke aliyezoeleka kuwa nyuma na bado akamuwezesha mwingine kutimiza wajibu wake, ni wazi pindi akipewa nafasi ataitekeleza vizuri zaidi. 
Sasa wakati umefika mwanamke achaguliwe na kuwekwa mbele, kwani tunaamini atafanya mambo mengi na kwa ufanisi zaidi. 
Ukweli huu unathibitishwa na maandiko Matakatifu kama tunavyoweza kusoma, Mithali 14:1 “ Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake ; bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe” Biblia inamtazama mwanamke kama ni mjenzi kuanzia ngazi ya familia. Na bila shaka sote tutakubali Taifa imara ni zao la familia zilizo imara. Quran Tukufu nayo inasema “Mwanamke ni madrasa” yaani ni chuo cha kuelimisha jamii.
Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon amewahi kusema kwamba “kote duniani ubaguzi dhidi ya wanawake bado umeenea, ingawa ni dhahiri kuwa usawa kwa wanawake ni maendeleo kwa wote” 
Hii ni sawa na kusema kwamba nchi zenye usawa zaidi wa kijinsia zina maendeleo zaidi kiuchumi, na kampuni zenye wanawake zaidi kwenye bodi zao zinatengeneza faida zaidi. 
Mikataba ya amani inayowashirikisha wanawake hufanikiwa zaidi; Mabunge yenye wanawake zaidi humulika masuala mengi zaidi, ikiwamo masuala ya afya, elimu pamoja na kupinga ubaguzi na kuwasaidia watoto.
Na hata waziri wa Mambo ya Nje wa zamani wa Marekani Bi Hillary Clinton, amewahi kusema kwamba wanawake wanaposhinda, ulimwengu unashinda na hivyo ajenda mpya ya maendeleo ni lazima iwe jumuishi. 
“Ni lazima tuhakikishe kuwa wanawake popote pale wana haki ya kupata ajira, kumiliki na kurithi mali, waweze kuwa utambulisho rasmi na halali, usawa katika elimu, wawe na washiriki kama wadau katika ujenzi wa amani, kutokomeza ukatili wa kijinsia, na pia ndoa za utotoni” 
Katika hili sisi Kamati ya Amani na Viongozi wa Dini tunachukua nafasi hii kuwahimiza wanawake wenyewe kwanza kuwa mstari wa mbele katika nafasi mbalimbali za uongozi. Kwa mfano, Mheshimiwa George H. Mkuchika (Mb) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, ambaye alikuwa mgeni rasmi wa Maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilayani Newala hivi karibuni, aliwaasa wanawake nchini akisema:  “Wanawake wasitegemee nafasi za upendeleo walizotengewa na Serikali na badala yake wachukue fomu na kuingia katika kinyang’anyiro na wanaume kugombea”
Ndugu Mgeni Rasmi kupitia wasilisho hili tumeweza kuona sura ya umaskini ni ile ya mwanamke, idadi kubwa ya wajinga wa kutokujua kusoma na kuandika duniani ni wanawake na wasichana. Mwanamke mmoja kati ya watatu kwenye nchi maskini au tajiri duniani atakumbwa na ukatili wa vipigo au kingono katika maisha yake. 
Mamilioni ya wanawake na watoto wanauzwa utumwani. Lakini matatizo yote haya yana majibu! Majibu ni kuwawezesha wanawake, na majibu yako mikononi mwetu sote kwa kuwapa nafasi katika ngazi mbalimbali za uongozi.
Kama tulivyoweza kuona mila na utamaduni, umasikini, mfumo duni, lugha dhalilishi, kutokujiamini, mifumo na itikadi ndani ya vyama vya siasa, uelewa mdogo, kutokujengewa uwezo, na kutokupewa msaada wa kutosha haya na mengine mengi yamekuwa vikwazo kwenye jamii yetu kuhakikisha kwamba wanawake wanajihusisha kwenye ngazi za maamuzi na kushika nafasi mbalimbali za uongozi. 
Hivyo basi, sisi kama Viongozi wa Dini tunaona kwamba kuna umuhimu mkubwa kuwa Wanawake ni wadau muhimu katika shughuli zote za kisiasa na maendeleo ya jamii. Idadi yao kama wapiga kura, wanachama wa vyama vya siasa, na kama wazalishaji wanaoendeleza kizazi, ni kubwa na haiwezi kupuuzwa. Kwa kuzingatia hayo, sisi Viongozi wa Dini tunatarajia na kutegemea kwamba tutumie nafasi zetu ili kuleta;
i. Kuhamasisha amani kwenye ushirikishwaji wa wanawake na katika suala zima la uchaguzi.
ii. Kuhamasisha wanawake wengi kushiriki kwenye ngazi mbalimbali za uongozi.
iii. Kuzuia migogoro isiyo ya lazima kwenye ushirikishwaji wa wanawake kwenye ngazi mbalimbali za uongozi.
iv. Kuhamasisha jamii kubadili mtazamo kuhusu wanawake kugombea nafasi mbalimbali za uongozi na kuwachagua.
Mwisho tunapohitimisha ushauri wetu sisi Viongozi wa Dini na Viongozi wa Kamati za Amani ni kuona vyama vya Siasa na Watanzania wote kwa ujumla tunahitaji kuchagua viongozi walio bora wakiwamo wanawake kwa ajili ya maslahi mapana ya Taifa letu kwa vizazi vya sasa na vitakavyokuja. 
Katika kufanikisha hayo tunasihi ushirikiano kutoka vyama vyote vya siasa kuendelea kutanguliza uzalendo wa nchi yetu kwanza na maslahi mapana ya Taifa letu hili pendwa. 
Sote kwa pamoja tukemee na kuwaelimisha wafuasi wetu kuondokana na vitendo vyote vyenye kuashiria uvunjaji wa Amani. Ugomvi, matusi, kejeli hayo yote sio utamaduni wetu. Tuendeleze utamaduni wa kuhojiana kwa hoja!
 Katika sura 16 Aya ya 125 (Surat Nahil) Qur’an Tukufu inasema “Ita katika njia ya mola wako kwa hekima na mawaidha mazuri na jadiliana nao kwa namna iliyo nzuri zaidi” 
Hivyo tunasisitiza tena na kuvisihi vyama vyote vya siasa, kwamba viwahimize Watanzania wote kwa pamoja pasipo kujali itikadi zetu, dini zetu, makabila, rangi zetu n.k bali kutanguliza mbele Uzalendo wa nchi yetu! Kwani lazima tufahamu Tanzania yetu inathamani zaidi kuliko tofauti zetu.
Tunatoa rai kwa kila mdau wa uchaguzi ikiwemo Tume ya Uchaguzi, vyama vyote vya siasa na wanachama wao, vyombo ya ulinzi na usalama hasa Jeshi la Polisi na Taasisi nyingine zote zinazohusika kuona zinaendesha shughuli zao kwa amani, upendo, kweli na haki kwa mujibu wa Sheria, kanuni na taratibu tulizo jiwekea ili kuona kuwa tunakuwa na uchaguzi wa amani na utulivu wenye kudumisha umoja na mshikamano wa Taifa letu pendwa la Tanzania. 
Tunaendelea kusihi katika mambo yote yatakayotendeka ni muhimu  maslahi ya Taifa yatangulizwe kwanza bila kujali maslahi ya mtu binafsi au ya makundi yetu madogo yaliyo mazao ya itikadi, falsafa au imani zetu. 
 
Katika wakati wote Sisi Viongozi wa Dini tutaendelea kudumu katika Sala na Dua ili Mungu atuvushe salama na tukiwa wamoja wenye amani na upendo.  
 
“Dini mbalimbali, Amani  na Upendo, Amani na upendo, Dini mbalimbali” !.
 
HAKI YA MWANAMKE KATIKA UONGOZI NA USHIRIKISHWAJI
 
 
NAFASI YA MWANAMKE KUELEKEA UCHAGUZI MKUU WA 2020 KATIKA MUSTAKABALI WA HAKI, HESHIMA NA UTULIVU KATIKA KUCHAGUA VIONGOZI BORA 16/09/2020.
HAKI YA MWANAMKE KATIKA UONGOZI NA USHIRIKISHWAJI.
Haki ya mwanamke katika uongozi na ushirikishwaji, kipengele chenye mzozo na rai tofauti. Ama haki za mwanamke katika ushirikiswaji, ni jambo lililo wazi  katika umuhimu na kubadilika kwake katika uislam, bali hata linavodhihiri kwa uwazi kabisa katika maisha ya mwanadam ambapo wanawake anachukua nafasi yake kama mshirika mkubwa wa wanaume katika ujenzi wa familia, jamii na taifa. 
Mwenyezi mwungu mtukufu anatuwekea wazi katika qur’ani juu ya ushirikishwaji katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali pale aliposema katika suratil tawbah 9;71 kuwa;
Tafsiri yake;
Na waumini wanaume na waumini wanawake wap kwa wao ni wasimamizi huamrisha mema na hukataza maovu na husimamisha swala na hutoa zaka na humtii mwenyezi mungu na mtume wake. Hao mwenyezi mungu atawarehemu.  Hakika mwenyezi mungu ni mtukufu mwenye hekima.
Yaani waumini wanaume na waumini wanawake wao kwa wao wanapendana na kusaidiana (kushirikiana) kwa mujibu wa imani wanaamrisha yanayoamrishwa na dini yao, na wanakatazwa wanayokatazwa. Wanasimamisha swala kwa nytajati zake na wanatoa zake kuwapa wanaostahiki kwa wakati wake. Wanatii anayowaamrisha mwenyezi mungu ntume wake na wanayaepuka  anayokataza mwenyezi mungu na mtume wake. Na hao ndio watakaokuwa chini ya rehema ya mwenyezi mungu kwa kuwa mwenyezimungu ni muweza wa  kuwalinda kwa rehema na mwenye hekima katika upaji.
 
Ni dhahiri kuwa pamoja na kuwepo aya nyingine zinazoonyesha kuwepo haki za mwanamke wa kiislamu katika ushirikiswaji, ayah ii inaliweka wazi hilo pale (SW)  anapoliweka wazi fungamano la mwanamke na mwanamme katika kuyaendea mambo ya msingi yanayohusiana na lengo la kuumbwa kwao ikiwa katika ayah ii basi ushiriki wake katika mambo mengine akiwa mwenza  wa mwanamme uko wazi kiimani na kiakili.
Kuna rai tofauti juu ya haki ya mwanamke katika uongozi  wa jumla na utawala, kuna makundi mawili yenye hoja za msingi katika  hiki kundi  linaloondoa ustahiki wa wanawake katika uongozi na utawala (uongozi mkuu), na kundi linaloona  kuwa mwanamke ana haki ya uongozi wa jumla ukiondoa utawala (ukhalifa).
Msingi wa tofauti ni namna walivyoifahamu aya ya 34 ya suratin nisaa 4;34 pale mwenyezi mungu aliposema;
Tafsiri;
Wanaume ni msimamizi wa mwanamke, kwa kufadhilishwa na mwenyezi mungu baadhi yao juu ya baadhi na kwa mali yao wanayotoa.
Kundi la kwanza  linaona kuwa usimamizi na uongozi wa jumla ni kwa wanaume tu, kutokana na ubora wa mazingatio, rain a ziada ya nguvu za kinafsi na kutabia walizonazon, na wanawake ni dhaifu katika hayo na wanatawaliwa mbele ya wanaume wala hawashirikiswi katika uongozi.
Kundi hili linadai pia kuwa hata kama aya huu itahusishwa na mambo ya familia, hoja itabaki palepale kuwa kama mwanamke mwenye kushindwa kiongoza familia yake moja basi ni dhahiri kuwa atashindwa pia kuyaongoza na kuyasimamia mambo ya watu (jamii ) na kutatua matatizo yao.
 
Hata hivyo kundi la pili linaona kuwa mahusiano baina wanaume na wanawake katika mambo ya jumla ni mahusiano ya kiutawala na kuwa daraja na usimamizi wa wanaume uliotajwa ndani ya qur’aan 4;34 haukulenga isipokuwa katika  maisha ya ndoa ambayo yanalazimisha katika kuendesha kwake kuwepo kidato cha mwisho katika ngazi ya uwajibikaji na utoaji maamuzi  yao ni wanaume . na kuondolewa wanawake katika maswala ya uendeshaji wa familia hakumaanishi  kutoweza  kwake, bali ni mgawanyo wa majukumu kwa Yule anayestahiki zaidi (aliye bora zaidi katika utekelezaji) kwamfano wakati jukumu la usimamizi wa jumla nkupewa wanaume, jukumu la kuchukua ujauzito na malezi ya motto limewekwa kwa mwanamke kimaumbile kwa kuwa yeye ndiye mtekelezaji bora wa jukumu hilo.
Kundi hili linajenga hoja kwa kuitumia surati tawbah 9;71 ambayo tumeitaja mwanzoni katika suala suala la usimamizi wa jumla ni suala la kushirikiana baina ya wanaume na wanawake.
Kama vile wamehilatilafiana makundi ayo mawili  katika kuielewa aya ya 34 ha suratin Nissa, wamehitilafiana  pia katika kuielewa hadithi ilipomfikia mtume  S.A.W) habari kuwa watu wa ajemi wamemtawalisha binti wa mfalme wao mtume (S.A.W) ALISEMA ‘hawatafaulu watu waliolitawalisha jambo lao kwa wanawake’.
Katika kuielewa khadithi hii kundi la kwanza linaiona kuwa linawakusanya wanawake wote wa aina zote za uongozi, katika kundi la pili  linaiona kuwa  khadithi hii inahusiana zaidi na utawala wa kiajemi  kama dua mbaya kwao. Lipo kundi jengine lililoiona khadithi hii kuwa inalenga uongozi  mkuu (ukhalifa) na si uongozi katika Nyanja nyengine.
HITIMISHO LA MADA YA UONGOZI NA USHIRIKISWAJI
Pamoja kuwepo kwa makundi mawili katika swala la haki ya mwanake wa kiislamu katika kuongoza na kwamba kundi moja  linaongelea kuwa mwanamke wa kiislamu hana haki ya kuongoza  katika ngazi yoyote ile, na kundi la pili  linaona kuwa mwanamke anahaki ya kuongoza katika nafasi za chini, na kwamba hana haki ya kuongoza katika ngazi ya juu ambayo ni ya mwisho katika uongozi.
 
Mtazamo wtu tunaona kuwa tifauti hiyo inakuwa na maana katika jamii ambayo ni ya kiislamu na inaongozwa kwa msingi ya kiislam. Ama katika jamii  amabyo ni ya kislamu amabyo mfumo wa maisha , utawala na uongozi si wa kiislamu mtazamo wetu  utakuwa tofauti na mitazamo  miwili hiyo, na mfano wa hilo ni jamii yetu ya watanzania ambayo makundi ya imani na itikadi tofauti jambo ambalo imepelekea utaratibu wa maisha hata muundo wa utawala  kutokwenda kwa mtazamo wa dini kwani katiba ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania inasema tunanukuu ‘ bila liathiri sheria zinazohusika na jamuhuri ya muungano kazi ya kutangaza dini  kufanya ibada na kueneza dini itakuwa huru na jambo la hiari  ya mtu binafsi  na shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi.
Msimamo wa nchi na utaratibu wake  unaonekana kuwa uwazi katika kifungu hicho cha katiba kwahoyo swala la uongozi kwa mwanamke wa kislamu katika jamii kama hii linakuwa ni dharura.
Tumeona hapo nyuma kwamba uongozi kwa mwanamke wa kiislamu katika jamii kama hii utakuwa ni jambo la dharura na uislamu katika mafunzo yake unaitambua swala la dharura . amesem mwenyezi mungu mtukufu katika surat al baqara (2/173) ‘atakaye lazimika hali ya kuwa si mwenye kufanya uovu na si mwenye kuvuka mipaka  hapana madhambi juu yake kwa hakika mwenyezi mungu ni msamehevu sana mingi wa rehema’ ayah ii katika sehemu yake ya mwanzo ilikuwa inazungumzia kuhusu kuharamishwa kwa jina lisilokuwa la mwenyezi mungu sasa Yule ambaye hapatakuwa mbele yake zaidi ya vitu hivyo na akawa anapoteza maisha ya nafsi yake huyo anaruhusiwa kuvitumia hivyo kwa kiasi cha dharura yake.
Na mwenyezi mungu mtukufu katika kuonyesha wepesi wa dini hii, amesema katika surati Al-Hajj aya ya 78 na hakufanya mwenyezi mungu juu yenu  katika dini ugumu wowote ; kutokana na wepesi wa dini, na kutokana na dharura hiyo mwanamke muisilamu katika nchi kama hii atachukua nafasi yake katika uongozi ili kwenda sambamba na utaratibu wan chi hii, na ndiyo maana hata watu wa somo la usuul fiqhi wamesema katika kanuni hii (dharura huhalalisha yaliyozuiwa) (ugumu huleta wepesi) (madhara huondolewa).
 
Amesema sayyed qutubi katika tafsiri yake iitwayo fiidhwilla AL-Quaran juzuu ya pili uk 157 ‘ pamoja na hayo uislamu unafanya hesabu ya mambo ya dharura na kwa hiyo unayaruhusu yale yaliyozuiliwa na inahalaliswa yaliyogharamishwa, isipokuwa msingi uwo kwasababu ya kuwa umeachiwa, unao uwezo wa kuyachukua yaliyoharamishwa mengine katika mawanja yote’.
 Kwa msingi huo mwanamke wakislamu anayo haki ya kushiriki katika uongozi kwa mtazamo huu.
Ushirikiswaji wa wanawake
Ulipokuwa uisilamu ulipoutambua utu wa mwanamke na kumpa haki zake zote ambazo anastahiki na ambazo zimewekwa wazi huko nyuma kupitia aya na hadithi mbalimbali za mtume mohammad (S.A.W) mwanamke si nusu ya jamii tu, bali ni mama wa jamii, kwani kuporomoka kwa wanawake  ni lazima kutasababisha kuporomoka kwa umma wote, kwani hapana mwanamme yoyote isipokua ni motto wa mwanamke nay eye ndie aliyemtunza na kumlea katika hatua ya kwanza, na kwa kiasi cha shakhasia yake na ubora wake na elimu yake na kuzingatiwa kwake inajengeka hali ya utu wake na nafasi yake katika maisha.
Historia ya uislamu imetuifadhi namna nyingi za kushirikishwa kwa mwanamke katika mambo mbalimbali ya maendeleo, wakwanza kumwamini mtume  ( SAW) wakati alipopatwa na fazaa kwa kujiwa na malaika jibrili kwa mara ya kwanza, na pia  aliweza kuitumia mali yake katika maendeleo ya dawa ya kiislamu, alisema mtume katika kuthibitisha hilo  ‘aliniamini bi khadija wakati waliponikanusha watu wengine na alinisaidia kwa mali yake wakati waliponinyima watu wengine.
 
Na mwanamke ndiye aliyemfanya omar bin AL-khattab, aingie katika uislamu, naye ni dada yake wakati alipomkuta anasoma Qur’aan, na mwanamke ndiye wa kwanza kuoendekeza kwa mtume (SAW) atengenezewe mimbari msikituni kwani pamepokewa kutoka na jabir kwamba mtume (SAW) atengenezewe mimbari msikitini kwani pamepokewa kutoka na jabir kwamba  mtume  (SAW) alikuwa akitoa hotuba zake akiwa amesimama katika kigogo cha mtende, akaambiwa na mwanamke ‘ewe mjumbe wa mwenyezi mungu hivi sikutengenezei  kitu ambacho ukalia kwani mimi ninamtoto ambaye ni seremala’ akasema mtume (SAW) iwapo tutapenda akatengeneza Yule mwanamke mimbari . imethibitishwa na abou Dawoud na tirmidhy na annasai.
Mwanamke pia alishirikishwa katika uwanja wa vita, na kufanya yale ambayo anayaweza.
Imepokea kutoka kwa jaafar bin Muhammad kwa baba yake kwamba najdah alimwandikia ibni abbasi kuhusu mbmbo matano; ibnu Abbas akasema ‘lau si kwamba nitakuwa nimeficha elimu nisingekuandika’ Najdah akasema ‘ama baada ya hayo nataka unieleze je  alikuwa mjumbe wa mwenyezi mungu (SAW) alipigana vita akiwa pamoja na wanawake?  Na je alikuwa anawapangia fungu katika ngawira? Ibn Abbas akajibu ; kwa hakika alikuwa akipigana vita hali ya kuwa yupo pamoja na wanawake hali ya kuwa wanawatibu majeruhi ma wanapewa ngawira’.
Tunajifunza kutokana na maswali najdah akimuuliza ibn Abbas na majibu yake kwamba uislamu ulimshirikisha mwanamke katika mambo mengi ya jamii isitoshe kuwa mtume (SAW) alimshirikisha mwanamke katika mazingira ya hatari sana  mazingira ya vita, mahali ambapo kwa mtazamo wa kawaida pengine ingeonekana kuwa mazingira hayo hayaendi sambamba na hali ya mwanamke, isipokuwa kwa mtazamo wa uislamu, kupitia utekelezaji wa mtume alikusudia  kuonyesha kwa matendo namna ambayo mwanamke anayo haki ya kushirikishwa katika mambo yote.
 
                                                    SHK.ALHADM.SALUM
                    SHK WA MKOA D’SALAAM/M/KITI KAMATI YA AMANI.

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
WAJIBIKA KULINDA UTU WA MWANAMKE UPATE KURA YAKE
01/09/2020
Wanamtandao wa Katiba, Uchaguzi na Uongozi ambao ni watetezi wa haki za wanawake na wasichana, yakiwemo masuala ya kukuza ushiriki wao katika uongozi wa kisiasa,    na pia tukiwa ni  wadau wakuu wa uchaguzi kama wapiga kura na wagombea katika nafasi mbalimbali za uchaguzi. Tumekuwa  tukifuatilia  kwa ukaribu mkubwa sana mchakato mzima wa uchaguzi tangu ulipoanza na matukio mbalimbali ambayo tayari yameshajitokeza ikiwemo utumiaji wa lugha za matusi na kauli mbaya za udhalilishaji dhidi ya wanawake wanaogombea na wafuasi wa vyama kwa ujumla. Kwa mfano, kumekuwepo na lugha za kutukana Wanawake wagombea wakiitwa “Malaya”, n.k 
 
Ni vema tutambue kwamba kasumba hii mbali na kwamba ni kinyume na haki za binadamu na ni kosa kisheria, inarudisha nyuma jitihada za serikali katika kufikia usawa wa kijinsia na kurudisha nyuma ari ya wanawake wengi kugombea nafasi za uongozi kwa sababu ya kuogopa kudhalilishwa. Halikadhalika,  inanyamazisha sauti za wanawake ambao ni zaidi ya nusu ya watanzania wote ambao ni wapiga kura wakuu na ambao wanahaki ya ushirki salama katika masuala ya kisiasa, suala ambalo halina tija kwa taifa letu. Kutokana na hali hii, tunaona umuhimu wa vyombo na mamlaka zinavyohusika kuwawajibisha kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Maadili ya Uchaguzi kwa wote wanaotumia matusi na lugha za kudhalilisha wanawake.
 
 Sisi, Wanamtandao watetezi wa haki za wanawake nchini, tunachukulia matukio haya kama kuvunjwa kwa Ibara ya 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977), inayokataza ubaguzi wa aina yoyote, na  tunaikumbusha jamii  kwamba Kanuni ya Makosa ya Adhabu, Sura ya 16, kifungu cha 89 kinataja kutumia lugha chafu dhidi ya mtu mwingine kuwa ni kosa la jinai. 
 
Tunaomba Umma wa Watanzania na Vyombo mbalimbali vinavyosimamia uchaguzi wa taifa hili utambua kwamba, ushiriki wa wanawake katika michakato ya uchaguzi ni haki yao ya kikatiba, na zimebainishwa katika sheria mbalimbali za nchi. 
 
Tume ya Taifa ya Uchaguzi huweka  wazi Kanuni mbalimbali za uchaguzi na Maadili ya vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi kwa  lengo la kuweka mazingira wezeshi kwa Watanzania wote, wakike na wakiume, kushiriki katika mchakato huu wa uchaguzi na kutoa mchango wao, kwa uhuru, uwazi na amani. Vile vile, Sheria ya Vyama vya Siasa, iliyorekebishwa mwaka 2018, katika kifungu chake cha 9, inakataza viongozi na wanachama wake kutamka au kutumia lugha za matusi, maneno ya kudhalilisha, uchochezi, au alama ambazo zinaweza kusababisha au kuhatarisha amani na ukosefu wa umoja wa kitaifa.
 
 Vilevile  Kanuni za  maadili ya Uchaguzi zilizotolewa katika Gazeti la Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania la tarehe 5/06/2020 zimebainisha mambo yaliyokatazwa kufanywa na vyama vya siasa kifungu ca 2.2 (b)  kinakataza kutumia lugha ya matusi, kashfa, kejeli, udhalilishaji na vitisho au lugha inayochochea uvunjfu wa amani au kuashiria ubaguzi wa jinsia, ulemavu, rangi au maumbile kwenye mikutano na kwenye shughuli zote za kampeni.
 
Kwa kuzingatia hili katazo, na kwa kuzingatia haki zetu za kikatiba na sheria za nchi, Sisi kama watetezi wa  haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa nchini, tunataka yafuatayo yazingatiwe ili kutokomeza udhalilishaji wa wanawake hasa kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi mkuu: 
Tunazitaka mamlaka zinazohusika (Tume ya Uchaguzi, Msajili wa Vyama Vya Siasa, na Taasisi nyingine husika kuwachukulia hatua kali kwa wagombea, pamoja na wapambe wao, wanaotoa lugha za kudhallisha na kutukana wanawake kwenye kampeni au mahali popote wakati huu wa uchaguzi m
Tunawataka viongozi wa taasisi mbalimbali zikiwemo za dini, na hasa vyama vya siasa, Asasi za Kiaraia, na Jamii yote kwa ujumla ya Tanzania kukemea vikali tabia hizi za kudhalilisha wanawake hasa kipindi hiki cha uchaguzi.
 
Vyama vya Siasa vitambue kwamba vina wajibu wa kulinda, kutetea na kudumisha haki na usawa wa Wanawake ndani ya vyama vyao na katika jamii kwa ujumla, kwa kuwa Wanawake ndiyo kundi kubwa la wapiga kura Tanzania. Kwahiyo lazima viheshimu UTU wa mwanamke  na kutoa fursa na kuweka mazingira yaliyo ya wazi na wezeshi ili wanawake wengi washiriki kikamilifu katika kutimiza haki yao ya kikatiba kama wagombea  na wapiga kura.
 
Mwisho na siyo kwa daraja, sisi wanawake wote kwa ujumla wetu, bila kujali Imani za kiitikadi, tukemee, tukatae na kuwajibisha wale wote wenye kutudhalilisha kwa njia yoyote ile, ikiwa ni pamoja na kututukana  
 
Tunawataka wanahabari na vyombo vya Habari kutumia taaluma yao vizuri kutetea UTU, HAKI ya mwanamke na hususani kipindi hiki cha uchaguzi. Vyombo vya Habari visishiriki katika kusambaza taarifa zenye lugha za matusi na udahlili zilizodhamiria katika kumdalilisha mwanamke wa Taifa hili.
 
 
Tamko hili la kukemea lugha za matusi dhidi ya wanawake ni mwendelezo wa matamko ambayo Wanamtandao tumeshayatoa tangu uchaguzi huu uanze. TUNALAANI NA KUKEMEA KWA NGUVU ZOTE MATUMIZI YA LUGHA ZA MATUSI, LUGHA ZA KEJELI, UDHALILISHAJI,  KATIKA KIPINDI CHOTE CHA UCHAGUZI
 
 
Imetolewa leo Septemba 1, 2020
Mtandao wa Wanawake Katiba Uchaguzi na Uongozi.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinaungana na Watanzania wote kuomboleza kifo cha Mwanadiplomasia Mkongwe, mwanahabri mahiri na Rais wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa.

TAMWA inakumbuka mchango wa Rais Mstaafu Hayati BWM katika kuijenga nchi hii kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni lakini hasa inaukumbuka mchango wake katika kujenga na kuhimiza usawa jinsia, kisheria, kisera na katika ngazi za maamuzi.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Zanzibar, Septemba 16th, 2020. Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi.
Waheshimiwa viongozi wa dini, wakiwamo maaskofu, masheikh, wachungaji.
Waheshimiwa viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa serikali, wakuu wa vyombo vya usalama na wanahabari. 
Itifaki imezingatiwa!
“Dini mbalimbali, Amani na Upendo, Amani na upendo, Dini mbalimbali!
Kwanza napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mungu kwa kutukutanisha katika kusanyiko hili na kutupa afya njema. 
 Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinayo furaha kubwa na kinatoa shukrani za dhati kwa viongozi wa dini mbalimbali, viongozi wa serikali, wanahabari, vyombo vya usalama na taasisi nyingine zisizo za kiserikali kwa kukubali kujumuika nasi katika warsha hii muhimu. 
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
Bila shaka wengi wetu tunafahamu fika kuwa Tanzania inatarajia kufanya uchaguzi mkuu ifikapo Oktoba 28 mwaka huu. 
Kutokana na tukio hilo kubwa la kihistoria, TAMWA imeona ni vyema kuhimiza na kukumbusha suala la nafasi ya mwanamke katika uchaguzi na kuishirikisha kamati ya Amani ya Viongozi wa dini nchini ambayo inaundwa na viongozi wa dini mbalimbali. 
Uwepo wako mahali hapa, ndugu mgeni rasmi, viongozi hawa wa dini na wadau wengine wa masuala ya Amani, umeonyesha dhahiri kuwa jambo hili ni zito na linaonyesha  mmeipa uzito ajenda hii na mnathamini nafasi ya mwanamke katika uchaguzi mkuu ujao.  
 
Ndugu mgeni Rasmi,
Ushiriki wa Wanawake katika siasa na katika ngazi za maamuzi, ni eneo lililo na changamoto lukuki na hivyo linahitaji kuhimizwa na viongozi wa ngazi za juu, asasi za kiraia, wanawake wenyewe na viongozi wa dini. 
Makundi niliyoyataja hapo juu yakitimiza wajibu wake katika kuhimiza na kuelimisha juu ya umuhimu wa wanawake katika uongozi, basi ni dhahiri kuwa, tutafikia ule usawa wa 50 kwa 50 ambao tumekuwa tukiupigia kelele kwa muda mrefu. 
Kwa sasa takwimu zinaonyesha kuwa bado ni asilimi 37 tu ya wanawake ndio walioko katika ngazi za maamuzi bungeni, hata hivyo bado tunaona kuna mapengo katika ushiriki wao ambayo hayana budi kuzibwa.
 
 Ndugu mgeni rasmi,
 Mapengo hayo ni pamoja na lugha dhalilishi wakati wa uchaguzi zinazowakatisha tamaa wanawake kuwania nafasi za uongozi, uteuzi usiozingatia jinsia ndani ya vyama vya siasa, hofu na kutojiamini kwa baadhi ya wanawake wenye nia ya kugombea na ilani za vyama zisizozingatia jinsia. 
Mapengo mengine yaliyobainika ni pamoja na rushwa ya ngono inayotajwa kutumika wakati wa uchaguzi, rushwa ya kifedha, uchumi duni kwa wanawake wanaotaka kugombea na hivyo kupelekea kushindwa kufanya kampeni. 
Mapengo mengine ni mila na desturi kandamizi, zinazowazuia kabisa wanawake wasishiriki katika siasa.
 
Ndugu mgeni rasmi,
Ipo pia mitazamo hasi katika jamii kuwa mwanamke anapoingia katika siasa basi amejishushia heshima na hadhi yake kwani hakuumbwa kuwa kiongozi, hayo yote yanachangia kupunguza idadi ya wanawake viongozi. 
Mapengo mengine ni chama kuwa na mapendekezo na utaratibu binafsi kwa kumthamini mwanaume zaidi hususan katika majimbo ambayo chama kina matarajio makubwa ya ushindi.
 
Ndugu mgeni rasmi na viongozi wa dini, 
TAMWA inawasihi kuendelea kuhimiza umuhimu wa wanawake kushiriki siasa na katika ngazi za maamuzi kwani nyinyi mnaaminika katika jamii kutokana na wajibu wenu mkuu. 
Viongozi wa dini, mna nafasi kubwa katika kuhimiza jamii, kuondoa mila na mitazamo potofu inayochochea ushiriki duni wa wanawake katika siasa na katika ngazi za maamuzi. 
 
 Ndugu mgeni rasmi,
Viongozi wa dini wanategemewa kuhubiri Amani na mshikamano katika kipindi cha uchaguzi na amani hiyo itapatikana iwapo makundi yote maalum wakiwamo watu wenye ulemavu na wanawake, watashiriki kikamilifu katika uchaguzi. 
Ndugu mgeni rasmi.
 Kwa kuwa Tanzania imesaini mikataba mbalimbali inayolenga kuongeza ushiriki wa wanawake katika siasa na mikataba mbalimbali ya amani,  hivyo basi, tunaomba yafuatayo yazingatiwe ili kuondoa vikwazo vyote vinazouia ushiriki wa wanawake katika siasa. 
 
1. Taasisi za dini kutoa elimu kuhusu ushiriki wa wanawake katika siasa na kuondoa mitazamo yote potofu inayokwamisha ushiriki wao  na kutoa mafundisho katika Quran na Biblia yanayomuonyesha mwanamke kama shupavu na mleta mabadiliko ili kuwajengea wanawake kujiamini. 
 
2. Serikali  na viongozi wa dini kukemea na kuwachukulia hatua  wanaotoa lugha dhalilishi  kwa wagombea wanawake wakati wa uchaguzi.
 
3. Vyama vya Siasa vitambue kwamba vina wajibu wa kulinda, kutetea na kudumisha haki na usawa wa Wanawake ndani ya vyama vyao na katika jamii kwa ujumla, kwa kuwa Wanawake ndiyo kundi kubwa la wapiga kura Tanzania. 
 
4. Vyama vya siasa vizingatie mchakato wa uteuzi wa wagombea kwa kuzingatia mrengo wa jinsia, kama Sheria Mpya ya Uchaguzi inavyoainisha.
 
5. Tunawaomba wanahabari kutumia kalamu zao kimaadili kwa kuepuka kuchochea lugha dhalilishi na kuidunisha taswira ya mwanamke katika jamii. 
 
6. Vyombo vya vya habari na wanahabari wanapaswa kupaza sauti zao kuhimiza ushiriki wa wanawake katika siasa na kulinda utu wake ili kuleta Amani na ushiriki kamilifu katika uchaguzi.
 
7. Wanawake waondoe dhana chonganishi zinazoenezwa kuwa hawapendani na hawawezi bali waendelee kusimama imara na kujitokeza kwa wingi katika chaguzi zijazo.
 
TAMWA tunaliombea Taifa likatawaliwe na upendo, Amani na mshikamano katika uchaguzi mkuu ujao Oktoba 28.
 Mungu ibariki Tanzania!
 
Rose Reuben.
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam Agost 12, 2020. Wakati macho na masikio ya Watanzania yakiisubiri kwa hamu Oktoba 28 ambayo ni siku ya uchaguzi mkuu nchini, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF) pamoja na Global Peace Foundation (GPF) tunaoa mapendekezo kwa  vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi, kuondoa changamoto zote zinazochagiza ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
Uchaguzi Mkuu unafanyika wakati ambapo kati ya wagombea 16 waliochukua fomu kugombea urais, wapo wanawake wawili mpaka sasa ambao ni Queen Cathbert Sendinga wa Chama cha ADC, na Cecilia Augustino wa Demokrasia Makini walioteuliwa na vyama vyao kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi huo. Kadhalika, wapo wanawake watano wanaowania umakamu wa Rais, katika mchakato huu wa uchaguzi. 
Lakini TAMWA, WiLDAF  na GPF  taasisi ambazo malengo yake ni kuwepo kwa jamii yenye amani, inayoheshimu haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia, na amani zimeona ni vyema kuikumbusha jamii, wadau wa masuala ya siasa na ya jinsia  kuzifanyia kazi changamoto zinazochangia ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
 TAMWA WiLDAF  na GPF  chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake Afrika, (AWDF) kupitia mradi wa ‘Wanawake Sasa’ imeendesha midahalo mbalimbali ya wanawake kutoka  vyama vya siasa ,wakiwamo wanawake wanasiasa, viongozi wa dini na kubaini kuwa bado kuna changamoto  zinazopelekea ushiriki mdogo wa wanawake katika siasa.
Midahalo tuliyofanya  katika  kanda za Dodoma, Arusha, Zanzibar na Dar es Salaam, iliibua changamoto zinazowakabili wanawake katika siasa ikiwamo lugha dhalilishi  zinazowavunja moyo wanawake  wanaogombea au walio katika nafasi za uongozi pamoja na familia zao kuwania nafasi mbali mbali za uongozi.
Wanawake wanaogombea nafasi za uongozi, hukutana na changamoto  ya lugha dhalilishi wakati wa kampeni, na hata wakati wa utendaji wao wa kazi ili tu kuwakatisha tamaa na kuwarudisha nyuma. Kama tunataka uchaguzi wa haki na wa kidemokrasia, ni muhimu kwa tume ya uchaguzi na vyombo vya usalama kupiga marufuku na kutoa adhabu kali kwa wanasiasa watakaotoa lugha hizi dhidi ya wanawake, Rose Reuben, Mkurugenzi TAMWA.
Katika midahalo hiyo, TAMWA , WiLDAF  na GPF  tumebaini kuwepo kwa rushwa ya kifedha katika shughuli za kawaida za siasa na hasa wakati wa chaguzi mbali mbali za ndani ya vyama, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu. Hii ni pamoja na tabia za wajumbe wanaotegemewa kupiga kura kuwa na hulka ya kudai au kujenga mazingira ya kupewa kitu kidogo ili waweze kutoa ushirikiano kwa mgombea. Hii inaathiri  wanawake ambao wengi wao hawana kipato cha kutosha hasa wanawake vijana. 
 
Pia tumebaini uwepo wa vitendo vya kuomba au kutengeneza mazingira ya rushwa ya ngono kwa baadhi ya wanaume wenye dhamana za kusimamia michakato ya chaguzi au mamlaka ndani ya vyama vya siasa.Changamoto hiyo husababisha wanawake kudhalilishwa na kuharibiwa ndoto zao za kisiasa na wakati mwingine familia au wenzi wao kuwazuia kushiriki katika siasa. 
Hayo na mengine mengi, yanachangia wanawake, kuvunjika moyo na hivyo kutoshiriki shughuli za siasa au kukosa nafasi za uongozi pale wanapokuwa na msimamo wa kutotoa rushwa.
Katika hili tunapenda kutoa rai kwa wanawake wenzetu kukataa kabisa kudhalilishwa na kutojihusisha na vitendo vya rushwa ya fedha au ngono na pia tunashauri jumuiya za wanawake ndani ya vyama vya sisasa kuvunja ukimya na kuhakikisha hoja za rushwa katika siasa inazungumzwa katika kila vikao vya jumuiya na vikao vingine muhimu. 
Pia tunaviomba vyama vya siasa viweke utaratibu madhubuti na wa siri wa kutoa taarifa za vitendo hivi na kuwe na kamati huru ndani ya vyama zisizofungamana na yeyote zitakazoratibu upokeaji, ufuatiliaji na utoaji adhabu kwa wale ambao bado wanaendekeza vitendo hivi vya kuwadhalilisha wanawake.   
Changamoto nyingine zilizoibuliwa katika midahalo hiyo,  ni Ilani za vyama vya siasa ambazo hazitoi nafasi kwa wanawake kuwa viongozi na kupata nafasi ya kugombea katika majimbo. Tumebaini wanawake wengi wanashindwa kushiriki uchaguzi kwa kutopata baraka hii kuanzia ndani ya vyama.
Wakati huo huo tunavitaka, vyama hivyo viwachague wanawake wenye uwezo wa kisiasa na wa uongozi.
Tunapenda kuvipongeza vyama vya siasa ambavyo vimetoa nafasi za wanawake kugombea nafasi za udiwani na ubunge na hata urais katika kura za maoni. 
“Mwaka huu wanawake wengi wamejitokeza. Tungependa kuviomba vyama vya siasa kuhakikisha kuwa wale wanawake wenye uwezo wasimamishwe kugombea nafasi hizo na tunawaomba wananchi wote kuwachagua wanawake waliosimamishwa kugombea nafasi za ubunge na udiwani, na wengine wapewe nafasi za teuzi mbalimbali Mkurugenzi wa GPF , Martha Nghambi. 
Tunavikumbusha vyama kuendelea kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake ambao hawakupata nafasi mwaka huu ili waweze kusimama na kugombea chaguzi zijazo ndani ya vyama vyao, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
Kadhalika tunapenda kuwaasa wanawake kuepuka kugawanywa na zile kauli kuwa, hawapendani badala yake waendelee kushirikiana na kupeana fursa mbalimbali za kisiasa, kiuchumi na masuala ya kijamii.
Kauli hizi za kuwa wanawake hatupendani si za kweli bali zimekuwa zikitumika katika jamii kuwagawa wanawake kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, Reuben 
Tunatarajia kuwa serikali, wadau wa siasa, vyombo vya usalama vitazingatia kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DK John   Pombe Magufuli ya kuwepo kwa mazingira wezeshi kwa wanawake katika uchaguzi mkuu na katika nafasi za uongozi na maamuzi. Pia tunampongeza kwa kuendelea kumchagua Mama Samia Suluhu kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao. 
 
Tungependa kumalizia kwa kusisitiza kauli zilizotolewa na Rais, viongozi wa vyama mbali mbali na tume ya taifa ya uchaguzi kuwa uchaguzi wa mwaka huu utakuwa ni  huru, haki na wa amani. 
Tunawakumbusha wagombea wote kuhakikisha kuwa hawatoi kauli zozote za uvunjifu wa Amani, kuchochea vurugu, kuwagawa watu kwa dini au makabila yao au matusi na udhalilishaji wa kijinsia kwa wagombea wengine. 
Wakati huo, TAMWA, WiLDAF na GPF  inaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuendelea kuhimiza uchaguzi huru, wa haki na usawa na kutengenezwa kwa mazingira sawa ya ushindani kwa wagombea wote.
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ubariki Uchaguzi Mkuu wa Octoba 2020. 
 
Rose Reuben Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
Anna Kulaya Mkurugenzi - WILDAF
Martha Nghambi Mkurugenzi - GPF

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Ndugu Wanahabari,

Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kunijalia uzima, afya njema na kuniwezesha kukutana nanyi ili niweze kuongea na watoto, wazazi/walezi na jamii kupitia kwenu wanahabari kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kwa mwaka 2020.

Ndugu Wanahabari,

Tarehe 16 Juni, ya kila mwaka, Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika ikiwemo Tanzania huadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika. Chimbuko la maadhimisho haya ni mauaji ya watoto takribani 2,000 yaliyofanywa na Utawala wa Makaburu katika Kitongoji cha Soweto, nchini Afrika Kusini tarehe 16 Juni, 1976. Mauaji hayo yalitokea wakati wa maandamano ya wanafunzi waliokuwa wakipinga mfumo wa elimu ya kibaguzi nchini humo. Mwaka 1991 viongozi wa Umoja wa Nchi za Afrika walifanya uamuzi wa kuienzi siku hiyo ikiwa ni kumbukumbu ya mauaji ya watoto hao. Maadhimisho haya yanatumiwa na wadau wote katika nchi za Afrika kutathmini ya hali ya upatikanaji wa haki na ulinzi kwa watoto kwa lengo la kuboresha ustawi na Maendeleo ya watoto.

Search