Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinaungana na Watanzania wote kuomboleza kifo cha Mwanadiplomasia Mkongwe, mwanahabri mahiri na Rais wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa.

TAMWA inakumbuka mchango wa Rais Mstaafu Hayati BWM katika kuijenga nchi hii kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni lakini hasa inaukumbuka mchango wake katika kujenga na kuhimiza usawa jinsia, kisheria, kisera na katika ngazi za maamuzi.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam, Machi 29, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mwanahabari wa IPP Media, Blandina Sembu.
 
Taarifa ya Jeshi la Polisi inasema kuwa, mwili wa Sembu, aliyekuwa mtangazaji wa kipindi cha Wanawake, kinachorushwa na ITV, uliokotwa katika maeneo ya Bamaga usiku wa kuamkia Machi 28, hali ambayo inaonyesha utata wa mazingira ya kifo chake. 
 
TAMWA kimesikitishwa na tukio hilo lililompoteza mwanaharakati wa masuala ya wanawake, masuala ya watu wenye ulemavu na mwanahabari aliyeipenda kazi yake. 
 
"TAMWA ikiwa ni mdau mkuu wa wanahabari wanawake nchini , kimeguswa na tukio hilo na tunaziomba mamlaka husika kuchukua hatua za uchunguzi ili kujua undani wa kifo cha Sembu ikiwa kimesababishwa na watu basi hatua kali zichukuliwe kwa watekelezaji wa tukio hilo" Rose Reuben, Mkurugenzi wa TAMWA
 
TAMWA  itamkumbuka Sembu kwa mchango wake mkubwa katika masuala ya Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi kwani alikuwa ni mjumbe wa kamati ya  Muungano wa Ushiriki Tanzania iliyoangazia Ushiriki wa watu wenye ulemavu, wanawake na vijana katika siasa na uongozi. 
 
 Kuondoka kwa Sembu ni pengo kubwa kwa tasnia ya habari, jumuiya za watu wenye ulemavu na pia katika jumuiya zinazotetea haki za wanawake nchini kwani alijitoa kwa dhati na alihakikisha anasemea haki za makundi hayo, pale inapobidi.
 
TAMWA inatoa salamu za pole kwa wanafamilia wote wa Blandina Sembu, Watendaji na Wanahabari wa IPP Media, wanaharakati wa masuala ya jinsia, watu wenye ulemavu na wanahabari  wote  nchini.
 
Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji- TAMWA.

User Rating: 3 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Julai 20, 2021.
Leo Julai 20, gazeti la Jamhuri, linalotolewa kila wiki, katika ukurasa wake wa kwanza na kuendelea ukurasa wa tatu limeandika habari yenye kichwa  kinachosema: Mambo ya Nje haijamchukulia hatua Balozi".
Katika habari hiyo, inayomtuhumu Balozi wa Libya nchini Tanzania, Bwana Kamal Ramadan Krista kuhusika katika usafirishaji haramu wa wasichana na unyanyasaji wa kingono, Mkurugenzi wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Dk Rose Reuben amenukuliwa akisema kuwa: Sina maoni yoyote kwa sababu habari hii haikufanyiwa uchunguzi wa kutosha
Taarifa hiyo ikaeleza zaidi kuwa Dk Rose“Alipoelezwa kuwa suala hilo ni la kukiukwa kwa haki za watoto wa kike na kusafirishwa nje ya nchi kinyume na sheria huku TAMWA ikijipambanua kuwa watetezi wa haki za wanawake, alishauri watafutwe Polisi wa Kimataifa(Interpol) na Idara ya Uhamiaji. 
Aya ya mwisho ya habari hiyo imesema: Mkurugenzi huyo ameonyesha kutofurahishwa na gazeti la Jamhuri kuandika tuhuma dhidi ya mwanadiplomasia huyo.
Mkurugenzi wa TAMWA anakiri kupigiwa simu na kutembelewa na mwandishi wa Habari wa gazeti hilo Bwana Alex Kizenga tarehe 16 Julai mwaka huu majira ya mchana ambako alihitaji maoni dhidi ya Habari iliyochapishwa katika gazeti hilo wiki tatu nyuma iliyomtuhumu Balozi Krista kusafirisha wasichana wa kitanzania kwenda kufanya biashara ya ngono nchini mwake.   
Mbali na kukataa kutoa maoni kuhusu Habari hiyo kwa msimamo kuwa haikuwa na taarifa kutoka vyanzo vya msingi ama vilelezo. Mkurugenzi wa TAMWA hakukubali kutoa maoni wala kuzungumza maneno kama ilivyonukuliwa na gazeti hilo na  badala yake mhariri na mwandishi  wa Jamhuri Media ambao walidhamiria kumuandika katika taarifa hiyo wamemlisha maneno Mkurugenzi wa TAMWA Dk Rose Reuben.
Ifahamike kuwa chama hiki ni cha kihabari na hivyo kinafahamu misingi yote ya taaluma ya habari na mawasiliano na hivyo tunasikitishwa na mmonyonyoko huu wa maadili uliofanywa  na gazeti la Jamhuri.
Kwa unyenyekevu tunawataka waombe radhi katika gazeti hilo. 
Kadhalika, TAMWA inafanya kazi na wanahabari kila siku na imekuwa ikiruhusu mahojiano na Mkurugenzi Dk Rose Reuben bila kuweka vikwazo, lakini endapo chama hakijatoa ruhusa ya kunukuliwa, basi maombi hayo yaheshimiwe kama maadili ya kihabari yanavyofundisha. 
Kwa kuwa TAMWA ni sehemu ya wanahabari, tunapenda kutoa wito kwa wanahabari wote kufuata misingi na maadili ya habari pindi wanapotimiza majukumu yao. 
Dkt. Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji ~ TAMWA.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 13, 2021. Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kuteua wanawake wawili katika Baraza la Mawaziri.
 
Uteuzi huo umefanyika jana ambapo Dkt Ashatu Kijaji ameteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na  Teknolojia ya Habari, wakati Dkt Stergomena Tax ameteuliwa kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
Uteuzi huu unafanya idadi ya mawaziri wanawake kufikia saba, kutoka watano walioteuliwa awali. 
 
TAMWA tunampongeza Rais Samia pia kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kumteua mwanamke kushika wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
"Uteuzi alioufanya Rais, wa kuongeza mawaziri wawili katika baraza unaonyesha dhahiri kuwa wanawake wanaaminika na wana uwezo wa kuleta mabadiliko katika Nyanja zote, kisiasa, kiuchumi na kijamii" Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA tunaamini kuwa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi ndiyo nguzo muhimu ya kuleta usawa na ndicho chanzo cha kuleta mabadiliko chanya katika jamii ambayo yataletwa katika usawa, haki na uwajibikaji. 
 
"Rais Samia, ameweza kuonyesha lile ambalo lilidhaniwa haliwezekani kwa kuwaweka mawaziri wanawake katika wizara nyeti  kama ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa, pia kwa kuendelea kuteua mawaziri wanawake, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala" amesema Dkt Reuben
 
Kadhalika tunampongeza Rais kwa ile kauli yake wakati akiwaapisha mawaziri hao aliposema: Nimeamua kuvunja taboo (mwiko), iliyoaminika kwamba wizara ya ulinzi lazima akae mwanaume mwenye misuli yake, kazi ya wizara ile si kupiga mizinga au kushika bunduki,  nimevunja taboo(mwiko) hiyo na kumteua dada yetu Tax kutokana na upeo wake mkubwa alioupata akiwa Jumuiya ya Nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara
 
“Hakika Rais amevunja dhana ya kuwa wanaume pekee ndiyo wenye uwezo wa kushika wizara hii, na kwa hili tunategemea Dkt Tax hatatuangusha, bali atasimamia vyema nafasi hiyo na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika masuala ya ulinzi na usalama,kwa kuwa ana uwezo na upeo" Dk Reuben 
Kadhalika TAMWA tunampongeza Rais Samia kwa kusikiliza kilio cha wanahabari na kuunganisha Wizara ya Habari, Mawasiliano na ile ya Teknolojia ya Mawasiliano, kuwa moja. 
Hatua hiyo itawafanya wadau wa habari kufanya kazi kwa ufanisi na wepesi zaidi kuliko hapo awali. 
TAMWA tunaamini kuwa Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi na katika ngazi za maamuzi ndicho chanzo cha haki, usawa na uwajibikaji na maendeleo  ya nchi. 
Wanawake Wanaweza! Kazi Iendelee!
Dkt Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

User Rating: 4 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Inactive
Dar es Salaam, Oktoba 1, 2020. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kina furaha kubwa kuutambulisha umma wa Watanzania, kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa ‘Wanawake Wanaweza’, unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Wanawake (UN-Women).
Hii ni fursa adhimu kwa TAMWA ambayo baadhi ya malengo yake makuu ni utetezi wa haki za wanawake na watoto, kuongeza ushiriki wa wanawake katika uongozi, kuondoa mifumo kandamizi inayochochoea ukatili kwa makundi hayo maalum, kwa kutumia vyombo vya habari. 
Hivyo basi jukumu  la TAMWA  katika mradi huu ni kuongeza uelewa kwa umma kuhusu umuhimu wa ushiriki wa Wanawake katika siasa na katika uongozi na madhara ya magonjwa ya mlipuko kama Covid-19 kwa wanawake na wasichana.
“Katika kufanikisha lengo kuu la mradi huu, TAMWA itawajengea uwezo wanahabari  katika kuripoti habari za jinsia na ufuatiliaji wa ushiriki wa wanawake katika uongozi na siasa,Rose  Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA. 
Kadhalika ili kufanikisha hayo, TAMWA itaendesha midahalo ya kihabari kwa ajili ya kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu umuhimu wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi. 
Mikoa 16 ambayo ni Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga, Mwanza, Mara, Mbeya, Ruvuma, Lindi na Mtwara, Wilaya 112 za mikoa hiyo na kata 458, ndiyo maeneo  yatakayotumika kama sampuli ya utekelezaji wa malengo ya mradi huu.
Kama ilivyoelezwa hapo juu, kuwa malengo ya mradi huu yatatimizwa kwa kutumia vyombo vya habari, hivyo basi TAMWA itashirikiana na wadau wake wakuu ambao ni vyombo vya habari, zikiwamo runinga 10, redio za kijamii 50, radio za masafa marefu 10 , magazeti 20 na mitandao ya kijamii, ili kuifikia jamii. 
TAMWA inatambua kuwa ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi (hasa ya kisiasa) bado ni mdogo, hali ambayo inakinzana na azma ya kujenga jamii isiyokuwa na ubaguzi kama ilivyobainishwa kwenye dira ya Taifa 2025, Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania 1977, pamoja na sheria mbalimbali za nchi. 
Kwa mfano, ripoti ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, (NEC: 2016) inaonyesha kuwa, asilimia 17 ya mawaziri ni wanawake, makatibu wakuu wanawake ni asilimia 11, wakuu wa mikoa ni asilimia 23, wakuu wa wilaya ni asilimia 28 na hii inaonyesha kuwa bado nafasi ya mwanamke katika ngazi za uongozi ni mdogo. 
“Hata hivyo, bado tunaupongeza  uongozi wa awamu ya tano, kwa mara ya kwanza alichaguliwa Makamu wa Rais mwanamke nchini, Mama Samia  Suluhu Hassan Reuben
Hivyo basi katika kipindi cha mwaka mmoja wa utekelezaji wa mradi huu, TAMWA, inatarajia kutumia nyenzo zake muhimu kuongeza uelewa kwa jamii na kuhakikisha wanawake wanaonekana kuwa viongozi halali na madhubuti katika jamii yetu Reuben 
Kama tulivyoainisha awali, kuwa wadau ni muhimu katika utekelezaji wa mradi huu, hivyo wadau wengine tutakaowashirikisha ni Chuo Kikuu cha Dar es Salam, kitivo cha Sayansi ya Jamii, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Shirika la  Wanasheria Wanawake na Maendeleo Afrika, (WILDAF), Viongozi wa dini na Mtandao wa radio za kijamii nchini (TADIO), Wizara ya Habari na Wizara ya Afya.
Wengine ni Mtandao wa Wanawake Viongozi Afrika (AWLN) na machampioni wa GEWE, Viongozi wa kimila, Kituo cha Demokrasia nchini(TCD).
 Hawa wote ni wadau ambao TAMWA itafanya nao kazi wakati wa utekelezaji wa mradi huu, na kwa nafasi yao watakuwa na mengi ya kuishirikisha TAMWA na umoja huu ndicho chanzo cha mafanikio ya utekelezaji wa mradi huu, Rose Reuben
TAMWA ambayo kiini chake ni wanahabari, inatarajia kushirikiana na vyombo vya habari ili kufikisha hii ajenda ya ushiriki wa wanawake katika siasa na katika uongozi kwa jamii, tukiamini kwamba, wanawake ni nguzo muhimu katika maendeleo ya jamii. 
Viongozi wa dini, taasisi za habari, taasisi za jinsia, ambazo TAMWA inakwenda kushirikiana nazo, ni nguzo muhimu katika kufanikisha adhma kuu ya mradi huu,Reuben.
Bila kuwasahau viongozi wa kimila na viongozi wa mikoa, wilaya na kata mbalimbali ambazo tutazifikia, TAMWA inatarajia ushirikiano mkubwa kutoka kwao. 
Mkurugenzi Mtendaji 
Rose Reuben
TAMWA.
 

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Machi 8th 2022, Dar es Salaam. Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, kinalazimika kutupia jicho lake kwenye usalama wa wanahabari wanawake katika vyumba vya habari nchini Tanzania.
 
Ulazima huu umekuja baada ya kuwepo kwa mwendelezo wa matukio, ushahidi, na ripoti za kitafiti zinazoonyesha kuwa wanahabari wanawake siyo tu Tanzania bado wanapitia unyanyasaji wa kingono katika vyumba vya habari. 
 
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kwa mwaka huu, yamebebwa na Kauli mbiu isemayo; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu. Kauli hii inatupeleka zaidi kutaka kuweka usawa katika vyumba vya habari baada ya kubaini kuna mdudu anayetafuna tasnia ya habari kimya kimya. 
 
 Utafiti uliofanywa na Asasi ya Wanawake katika Habari Africa (WIN) mwaka 2022 ulibaini kuwa, asilimia 41 ya wanawake wanahabari waliwahi kufanyiwa unyanyasaji wa kingono wakiwa katika maeneo ya kazi. 
 
Hivyo basi wakati tukiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, TAMWA inahimiza Wamiliki wa vyombo vya habari, watunga sera, serikali na wanahabari wote kwa ujumla kutupia jicho unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa ndani ya vyumba vya habari.
 
Unyanyasaji wa kingono kwa wanahabari iwe ndani au nje ya vyumba vya habari, una madhara makubwa katika chombo cha habari, taaluma ya habari, aina ya habari zitakazoandikwa na hata katika maendeleo ya nchi yenyewe. Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk  Rose Reuben.
 
Udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari wanawake, unachagiza wanahabari wengi wa kike kuikimbia tasnia  na hilo limesababisha kupoteza vipaji lukuki ambavyo vingekuzwa iwapo kusingekuwa na bughudha hiyo.
 
 
Kadhalika udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari unashusha hadhi ya chombo cha habari, kwani pindi mwanahabari anapotoa shutuma kuwa mhariri au kiongozi wa chombo cha habari kamdhalilisha kingono, basi ni dhahiri chombo hicho hutazamwa vibaya. Kadhalika vivyo hivyo anapotoa taarifa kuwa amedhalilishwa na chanzo cha habari.
 
Kaika utafiti uliofanywa na TAMWA kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) mwaka 2021, kuhusu hali ya rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari, ilibainika kuwa wanahabari wanawake wamewahi kukutana na udhalilishaji huu, kimwili, kimaneno na hata baadhi walifukuzwa kazi. 
 
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyoiona TAMWA katika tafiti hizo ni ukimya. Wanahabari wengi wanawake hawataki kusema pindi wanapodhalilishwa, hivyo wanaishi katika msongo, maumivu, fedheha na wengine kuacha kabisa tasnia, kwa sababu ya udhalilishaji wa aina hii.  Dk Rose Reuben.
 
Utafiti wa TAMWA ulibaini kuwa wanafunzi wengi wa tasnia ya habari wa vyuo vikuu wanaokwenda kujifunza kwa vitendo  katika vyumba vya habari wamekutana na udhalilishaji huo na kujikuta wakiikimbia tasnia hiyo mara tu wanapomaliza masomo yao. 
 
Hata utafiti wa WIN uliofanyika Afrika nzima kuangalia ukubwa  wa tatizo hilo, ulibaini kuwa ni asilimia 4 tu ya wanahabari wanawake wanaopaza sauti zao pindi wanapofanyiwa ukatili huu.
 
Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, kwanza tunawaasa wanahabari kupaza sauti zao na kueleza bayana madhila wanayopitia katika kazi zao ikiwamo udhalilishaji wa kingono.
 
Imetosha sasa wanahabari kuwa kipaza sauti cha kusemea matatizo ya wengine  katika jamii, ilhali tatizo lao wamelinyamazia kimya, Dk Rose Reuben.
 
Kadhalika tunaviomba vyombo vya habari kuhakikisha vinaweka na ketekeleza sera ya jinsia ndani ya vyumba vya habari, na sera ya kupinga unyanyasaji na rushwa ya ngono na sera hizi zijulikane na wote ndani ya vyumba vya habari. 
 
Katika utafiti wa TAMWA tulibaini kuwa vyumba vingi vya habari havina sera ya jinsia wala sera za kupinga rushwa na unyanyasaji wa kingono, na vile vyenye sera hizi hazitumiki au hazijulikani na wanahabari/ wafanyakazi wengine, Dk Rose Reuben.
 
Lakini zaidi tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu sheria ya mwaka 2017 inayoangalia rushwa ya ngono mahala pa kazi. Hii itasaidia wanawake na wasichana kuifahamu  kujua kuwa uwepo wa sheria hii na namna ya kukusanya ushahidi wa madhila hayo. 
 
Lakini wakati huo huo serikali ione umuhimu wa kupeleka ajenda ya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu na hata mashuleni, ili kuwajengea uelewa watoto wa Tanzania uelewa na athari ya rushwa hii. 
 
Kwa mfano, hivi karibuni yamekuwapo matukio kadhaa ya wahadhiri kwa vyuo vikuu kuwadhalilisha kingono wanafunzi na huku video zao za utupu zikivuja. Haya na mengine mengi yapo pia katika vyombo vya habari na mahala pa kazi ikiwamo serikalini. 
 
Kwetu sisi TAMWA hili ni janga na ni muuaji wa kimya kimya wa utu wa wanawake,  endapo lisipochukuliwa hatua basi mabinti zetu vyuoni na wanataaluma katika uandishi watapoteza mwelekeo na hivyo tutapoteza vipaji na nguvu kazi, Dk Rose Reuben.
 
 
Kama kauli mbiu ya mwaka huu isemavyo, Haki Sawa kwa maendeleo Endelevu ndivyo tunavyotaka wanahabari wanawake waheshimiwe na wathaminiwe, watimize wajibu wao bila kulazimishwa au kurubuniwa kutoa rushwa ya ngono. 
 
Tunachoweza kusema TAMWA ni; Mwanahabari mwanamke anaweza kuripoti habari za uchunguzi kama mwanaume, anaweza kuripoti michezo kama mwanaume, anaweza kuripoti katika vita kama ilivyo kwa wanaume. Uanamke wake, hauondoi ujasiri, utimamu na umakini katika taaluma  yake. 
 
Kadhalika, Mwanahabari mwanamke hapimwi kwa sura wala sauti yake, bali ujuzi na kipaji katika taaluma yake ya uanahabari. 
 
TAMWA tunasisitiza kuwa hiki ni; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu kama kauli mbiu  ya mwaka huu isemavyo. 
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
 
Dk Rose Reuben
TAMWA
 

Search