Press Release

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
June 10th, 2022, Dar es Salaam. The Tanzania Media Womens Association (TAMWA) calls on the Tanzanian government to continue to use the negotiation, and reconciliation process and to follow the procedures for the transfer of land and national resources.
 
The request comes after reports from June 8, 9 and today 10, 2022, showing pastoralists of the Loliondo Maasai tribe and army forces protesting the implementation of the border marking of 1500 square kilometers of their villages for natural resource conservation trending in social media. 
 
We understand and agree with the Prime Minister Kassimu Majaliwa that the loss of peace in any area is causing inconvenience to women, the elderly and children and therefore calls on the government to return to the negotiating table to end the Loliondo conservation crisis with the Maasai community.
 
TAMWA have witnessed many conflicts being resolved through dialogue and reconciliation in this country so we believe that even this conflict can also be resolved without resorting to force or inciting violence that is smearing the nation with human rights abuses.
 
Dr Rose Reuben,
 
 
Executive Director
 
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam, 15 May, 2022 Wakati dunia  ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya Familia Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA)kinawakumbusha watanzania kutathimini hali ya maendeleo ya familia, na kuwahimiza wazazi na walezi kutoa huduma muhimu za matunzo na kuzuia vitendo vya ukatili kwa watoto ambavyo vimekithiri hapa nchini.
Kama kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inavyosema: Dumisha amani na upendo kwa familia imara, jitokeze kuhesabiwa TAMWA tunawakumbusha wanafamilia kuepuka migogoro inayopelekea kusambaratika na kuacha watoto wakikosa huduma muhimu ikiwamo upendo wa wazazi au walezi.  
“Hivi karibuni kumeripotiwa matukio kadhaa ya ukatili wa watoto ikiwemo vipigo, mauaji, udhalilishaji wa kingono na hata watoto waliojiingiza katika vitendo vya uhalifu maarufu kama Panya Road, ambayo yanaonyesha wazi kuwa ipo hitilafu kubwa iliyoikumba taasisi ya familia Dr. Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji-TAMWA
 Kadhalika  kauli mbiu hii ya kitaifa ya Siku ya Kimataifa ya Familia inazikumbusha familia umuhimu wa kushiriki sensa ya watu na makazi itakayofanyika Agosti 23, mwaka huu, zoezi ambalo litaiwezesha serikali kubaini takwimu sahihi za watu na kaya ili kupanga mipango ya maendeleo kuanzia ngazi ya familia. 
‘Sensa ni zoezi muhimu la kitaifa kwani ni ukweli usiopingika kuwa maslahi ya watoto na sapoti ya familia kama taasisi vinakamilishwa kwa kubainishwa kwa takwimu sahihi za watu, mipango ya kifedha, na rasilimali nyingine zinazomilikiwa na familia, baada ya zoezi hili TAMWA tunaiomba serikali kutengeza Sera ya familia iyakayoainisha wajibu, maslahi ya kiuchumi na mipango kwa familia kama taasisi Dr. Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji- TAMWA
Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloangalia maslahi ya watoto (UNICEF) zinaonyesha kuwa asilimia 60 ya ukatili wa watoto unafanyika majumbani na asilimia 40 unafanyika mashuleni, hivyo kuna umuhimu wa watanzania wote kuthamini na kuimarisha taasisi ya familia kwa upendo na amani.
Pia kwa mujibu wa taarifa za makosa ya ukatili wa jinsia na unyanyasaji zilizotolewa na Jeshi la Polisi katika kipindi cha Januari hadi Disemba mwaka 2021 zinaonyesha mikoa ya kipolisi iliyoongoza kwa ukatili dhidi ya watoto ni Arusha 808, Tanga 691, Shinyanga 505, Mwanza 500 na Ilala 489.  
Kadhalika makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ya matukio ni ya ubakaji 5,899, kumpa mimba mwanafunzi 1677, ulawiti 1,114, kumzorotesha mwanafunzi masomo 790 na shambulio 350. 
Familia ni chanzo cha rasilimali watu, na ndio maana Baraza kuu la Umoja wa Mataifa mnamo mwaka 1993 lilitoa tamko namba 47/237 na  kuitangaza Mei 15 kuwa siku maalumu ya kutathimi hali ya familia, upatikanaji wa huduma muhimu na maendeleo yao.  
TAMWA tunaendelea kusisitiza watanzania, kuthamini ngazi ya familia, kama eneo la kwanza la kuonyesha upendo, kuanzisha maendeleo na kurithisha vizazi vyetu elimu, mali na hekima. 
Ngazi ya familia ndiko kunakoanzia maendeleo, afya na kunakojenga taswira ya tabia ya mtu mmoja mmoja, familia ni muhimu, Dr Rose Reuben. 
Mkurugenzi Mtendaji 
Rose Reuben
TAMWA

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
Ndugu mgeni rasmi,
Wawakilishi wa FES,
Mkuu wa Dawati la Jinsia,
Mwakilishi wa Takukuru,
Wanahabari,
Nawasalimu kwa jina la JMT!
 
Dar Es Salaam, 2nd December, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Friedrich-Ebert-Stiftung (FES) Tanzania, wanaungana na watanzania wote kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.
 
Maadhimisho haya, hufanyika kila ifikapo Novemba 25 hadi Desemba 10 kila mwaka.  Kwa mwaka huu, maadhimisho haya yamepambwa na kauli mbiu isemayo: Pinga ukatili wa kijinsia Sasa 
 
Hata hivyo wakati maadhimisho haya yakiendelea, TAMWA pamoja na FES tumebaini kuwa tatizo la rushwa ya ngono mahala pa kazi linaendelea kushika mizizi katika jamii yetu. 
 
Hilo lilibainika hata wakati TAMWA ilipofanya mradi na Asasi ya Habari ya Internews mnamo mwaka 2019 na kuwashirikisha wanahabari kufanya habari za uchunguzi kuhusu rushwa ya ngono mahala pa kazi.
Makala za wanahabari hao, zilibainisha wazi, rushwa hiyo ipo lakini imegubikwa na ukimya hasa kutoka kwa waathirika. 
Kadhalika, mwaka 2021, TAMWA kwa kushirikiana na Women Fund Tanzania, (WFT) ilitekeleza mradi wa kuangazia rushwa ya ngono kwa wanahabari. TAMWA ilifanya utafiti na kubaini wanahabari wanakabiliwa kwa kiasi kikubwa na rushwa ya ngono na ukatili mwingine ndani ya vyumba vyao vya habari.
Utafiti  uliofanywa na asasi ya EBA nchini Tanzania mwaka 2020 ulibaini kuwa, suala la rushwa ya ngono linafahamika na limetanuka kuanzia katika sekta ya elimu na katika sekta ya ajira. 
 
Tatizo la rushwa ya ngono ni kubwa lakini limegubikwa na ukimya, wahanga wengi hawatoi taarifa wakiogopa kudhalilishwa zaidi, Dr Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA.
 
TAMWA tunasema, rushwa ya ngono vyuoni ndicho chanzo cha kuwa na wanafunzi wasio na tija katika sekta ya ajira, lakini pia ndicho chanzo cha kuzalisha wanaataluma wasio na sifa za kuajiriwa. 
 
Rushwa hii ya ngono mahala pa kazi na vyuoni, ndicho chanzo pia cha maambukizi ya Virusi vya Ukimwi na magonjwa mengine ya zinaa, Dr Rose Reuben. 
Katika tafiti zetu, TAMWA tumegundua kuwa rushwa ya ngono hufanyika sio tu mahala pa kazi, bali wakati mwingine, hata katika kambi za wakimbizi, katika shule za sekondari.
Rushwa ya ngono hurudisha nyuma maendeleo ya mtu mmoja mmoja na nchi kwa sababu matokeo ya ukatili wa aina hii ni kurudisha nyuma ari ya utendaji kazi wa wanafunzi, wafanyakazi au waumini, Dr Rose Reuben
 TAMWA tumeona pia zipo changamoto katika kukabiliana na aina hii ya ukatili, kwanza ni ukimya. Wahanga wengi kushindwa au kuhofia kutoa ushahidi na kuzungumzia suala hili. Lakini pili, ukosefu wa takwimu zitakazowezesha wadau kufanyia kazi aina hii ya ukatili.
Ipo sheria ya makosa ya rushwa, inayogusa rushwa ya ngono, nayo ni sheria namba 11 ya mwaka 2007, kifungu cha 25. Dr Rose Reuben
 
Ukatili kwa njia ya mtandao
Wakati huo huo, tunakemea vikali ukatili kwa njia ya mtandao unaoendelea. Tumeona, tumesikia na wakati mwingine sisi ndiyo tumekuwa waanzilishi wa ukatili huu. Kutumia picha za wanawake vibaya, kutumia lugha dhalili kwa kundi Fulani mitandaoni, kutumia picha za watoto na kuweka maudhui yanayomdhalilisha. Haya ni baadhi tu ya matendo yanayochagiza ukatili wa kijinsia mitandaoni.
 
TAMWA ni wanahabari na wanahabari ni TAMWA, hivyo tunawaomba wadau wetu wa habari, mkatumie kalamu zenu kukemea rushwa ya ngono  ndani ya vyumba vyenu vya habari  na kuvaa joho la kupinga aina zote za ukatili wa kijinsia ikiwamo ule wa kwa  njia ya mtandao. 
 
Kadhalika, tunaipongeza serikali kwa kupitia wadau wake wakiwamo Takukuru, wamefanyia kazi suala la rushwa ya ngono kwa kufanya tafiti kadhaa lakini pia kwa kufanyia kazi makosa ya aina hii. Hongereni! lakini tunatamani  matokeo zaidi, kesi zaidi zipelekwe mahakamani, hukumu itolewe  ili kufanya mahala pa kazi pawe sehemu salama na penye tija. 
Pia tunampongeza  Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kwa kuzindua mwongozo wa madawati ya rushwa ya ngono vyuoni. Tunaomba yakatumike kwa tija. 
Ewe Mwananchi, pinga ukatili wa kijinsia sasa,
 
#KaziIendelee
#ZuiaUkatiliMtandaoni
#ZuiaUkatili
 
Dr Rose Reuben
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Dar es Salaam, Mei, 20. 2022.  Imekuwa ni ada sasa kwa duru zetu za habari kutawaliwa na  matukio ya ubakaji hasa kwa watoto.

Katika kipindi cha Januari hadi Mei mwaka huu, matukio makubwa yaliyotikisa vyombo vya habari ni pamoja na lile la mkoani Katavi, ambapo mwalimu wa Mafundisho ya dini ya Kikristo Joseph John, kukamatwa kwa kulawiti watoto wanne.

Tukio jingine ni lile la mkazi wa Iringa, kudaiwa kumlawiti mtoto wake  wa kambo na shemeji yake. Kadhalika, liliripotiwa tukio lililobeba vichwa vingi vya habari la mtoto wa miaka 14 mkazi wa Iringa, kuwalawiti watoto wenzake 14 wote wa kiume.

Kadhalika hili la juzi, Mei 18 ambapo mwalimu wa Madrasa Jumanne Ikungi, mkazi wa Arusha kwa tuhuma za kuwalawiti wanafunzi takribani 22 wa shule ya msingi Mkonoo, jijini Arusha. Mkuu wa wilaya ya Arusha, Said Mtanda alithibitisha  baada ya kufika katika shule hiyo na kuzungumza na wazazi, walimu na wanafunzi ikiwa ni baada ya kukamilisha alichokiita uchunguzi wake juu ya mwalimu huyo wa madrasa.

 Kwa matukio hayo yaliyoripotiwa kati ya Januari na Mei, inatosha kusema kuwa watoto wetu hawapo salama na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) tunalazimika kusema, ‘watoto hawa hawana pa kukimbilia’.

“Mwenendo huu wa matukio ya ubakaji na ulawiti wa watoto tena na walimu, viongozi wa dini na wazazi au walezi, unadhihirisha kuwa tatizo hili bado ni kubwa nchini na linahitaji maamuzi magumu kutoka kwa watunga sera wetu,” Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben.

TAMWA pamoja na wadau wengine wa masuala ya jinsia, tumekuwa tukiimba wa kuitaka jamii kuzuia ukatili kwa miaka zaidi ya 30 sasa tukililia mabadiliko ya sera, sheria na hata kutoa elimu kwa jamii. Lakini bado tatizo hili linaendelea, tena sasa likitekelezwa na viongozi waliotegemewa kuwalinda watoto wetu, tuliodhani kuwa ni walimu wa kukuza maadili mema kwa watoto.

“Tunahitaji zaidi ya sheria kukomesha ukatili huu, tunahitaji maamuzi magumu kutoka ngazi zote kuanzia familia, wanajamii, viongozi wa dini zote na serikali kwa ujumla wake kwa sababu watoto walio taifa la kesho, wanaharibiwa kimwili na kisaikolojia” Dk Rose Reuben.

Wakati huo huo, taarifa za makosa ya ukatili wa jinsia na unyanyasaji zilizotolewa na Jeshi la Polisi katika kipindi cha Januari hadi Disemba 2021 zinaonyesha mikoa ya kipolisi iliyoongoza kwa ukatili dhidi ya watoto ni Arusha 808, Tanga 691, Shinyanga 505, Mwanza 500 na Ilala 489. 

Kadhalika makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ya matukio ni ya ubakaji 5,899, kumpa mimba mwanafunzi 1677, ulawiti 1,114, kumzorotesha mwanafunzi masomo 790 na shambulio 350.

Wakati tukiendelea kutafuta suluhisho la janga hili, TAMWA inaendelea kutoa elimu katika shule za sekondari na msingi, kuhusu mada za ukatili wa kijinsia, lakini bado hakuna mitaala shuleni inayogusa masuala ya afya ya uzazi moja kwa moja.

“Utafiti uliotolewa hivi karibuni na Taasisi ya Haki Elimu, unaonyesha kuwa watoto wengi hawafundishwi elimu ya afya ya uzazi, lakini  zaidi hasa walimu nao wanaogopa kufundisha wanafunzi mada hizo, hapa ndipo mzizi wa tatizo ulipo,”

“Ni dhahiri kuwa mambo yanayouhusu afya ya uzazi na ukatili wa kingono hayazungumzwi ndani ya familia wala shuleni tena wengine wanaona ni mambo ya aibu yasiyostahili kujadiliwa, hivyo yanabaki kuwa masuala ya wadau na serikali ambao nao husuluhisha tatizo na sio mzizi wa tatizo,” Dk Rose Reuben.

Wakati tukijiandaa na zoezi la Sensa ya Watu na Makazi, ifikapo Agosti 23,  ni wakati muhimu kwa  viongozi, wazazi, walezi, wasimamizi wa sheria, wadau wa masuala ya jinsia na watoto kujitathmini wapi penye mapengo, ili tuzibe ombwe hili la ubakaji wa watoto.

TAMWA imesikitishwa na ubakaji huu wa watoto unaoendelea hapa nchini na tunamuomba Rais Samia Suluhu Hassan, kutamka kuwa hili ni janga na kutoa maamuzi magumu kunusuru watoto wetu.

 Dk Rose Reuben

Mkurugenzi Mtendaji

TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Machi 8th 2022, Dar es Salaam. Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, kinalazimika kutupia jicho lake kwenye usalama wa wanahabari wanawake katika vyumba vya habari nchini Tanzania.
 
Ulazima huu umekuja baada ya kuwepo kwa mwendelezo wa matukio, ushahidi, na ripoti za kitafiti zinazoonyesha kuwa wanahabari wanawake siyo tu Tanzania bado wanapitia unyanyasaji wa kingono katika vyumba vya habari. 
 
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kwa mwaka huu, yamebebwa na Kauli mbiu isemayo; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu. Kauli hii inatupeleka zaidi kutaka kuweka usawa katika vyumba vya habari baada ya kubaini kuna mdudu anayetafuna tasnia ya habari kimya kimya. 
 
 Utafiti uliofanywa na Asasi ya Wanawake katika Habari Africa (WIN) mwaka 2022 ulibaini kuwa, asilimia 41 ya wanawake wanahabari waliwahi kufanyiwa unyanyasaji wa kingono wakiwa katika maeneo ya kazi. 
 
Hivyo basi wakati tukiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, TAMWA inahimiza Wamiliki wa vyombo vya habari, watunga sera, serikali na wanahabari wote kwa ujumla kutupia jicho unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa ndani ya vyumba vya habari.
 
Unyanyasaji wa kingono kwa wanahabari iwe ndani au nje ya vyumba vya habari, una madhara makubwa katika chombo cha habari, taaluma ya habari, aina ya habari zitakazoandikwa na hata katika maendeleo ya nchi yenyewe. Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk  Rose Reuben.
 
Udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari wanawake, unachagiza wanahabari wengi wa kike kuikimbia tasnia  na hilo limesababisha kupoteza vipaji lukuki ambavyo vingekuzwa iwapo kusingekuwa na bughudha hiyo.
 
 
Kadhalika udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari unashusha hadhi ya chombo cha habari, kwani pindi mwanahabari anapotoa shutuma kuwa mhariri au kiongozi wa chombo cha habari kamdhalilisha kingono, basi ni dhahiri chombo hicho hutazamwa vibaya. Kadhalika vivyo hivyo anapotoa taarifa kuwa amedhalilishwa na chanzo cha habari.
 
Kaika utafiti uliofanywa na TAMWA kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) mwaka 2021, kuhusu hali ya rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari, ilibainika kuwa wanahabari wanawake wamewahi kukutana na udhalilishaji huu, kimwili, kimaneno na hata baadhi walifukuzwa kazi. 
 
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyoiona TAMWA katika tafiti hizo ni ukimya. Wanahabari wengi wanawake hawataki kusema pindi wanapodhalilishwa, hivyo wanaishi katika msongo, maumivu, fedheha na wengine kuacha kabisa tasnia, kwa sababu ya udhalilishaji wa aina hii.  Dk Rose Reuben.
 
Utafiti wa TAMWA ulibaini kuwa wanafunzi wengi wa tasnia ya habari wa vyuo vikuu wanaokwenda kujifunza kwa vitendo  katika vyumba vya habari wamekutana na udhalilishaji huo na kujikuta wakiikimbia tasnia hiyo mara tu wanapomaliza masomo yao. 
 
Hata utafiti wa WIN uliofanyika Afrika nzima kuangalia ukubwa  wa tatizo hilo, ulibaini kuwa ni asilimia 4 tu ya wanahabari wanawake wanaopaza sauti zao pindi wanapofanyiwa ukatili huu.
 
Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, kwanza tunawaasa wanahabari kupaza sauti zao na kueleza bayana madhila wanayopitia katika kazi zao ikiwamo udhalilishaji wa kingono.
 
Imetosha sasa wanahabari kuwa kipaza sauti cha kusemea matatizo ya wengine  katika jamii, ilhali tatizo lao wamelinyamazia kimya, Dk Rose Reuben.
 
Kadhalika tunaviomba vyombo vya habari kuhakikisha vinaweka na ketekeleza sera ya jinsia ndani ya vyumba vya habari, na sera ya kupinga unyanyasaji na rushwa ya ngono na sera hizi zijulikane na wote ndani ya vyumba vya habari. 
 
Katika utafiti wa TAMWA tulibaini kuwa vyumba vingi vya habari havina sera ya jinsia wala sera za kupinga rushwa na unyanyasaji wa kingono, na vile vyenye sera hizi hazitumiki au hazijulikani na wanahabari/ wafanyakazi wengine, Dk Rose Reuben.
 
Lakini zaidi tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu sheria ya mwaka 2017 inayoangalia rushwa ya ngono mahala pa kazi. Hii itasaidia wanawake na wasichana kuifahamu  kujua kuwa uwepo wa sheria hii na namna ya kukusanya ushahidi wa madhila hayo. 
 
Lakini wakati huo huo serikali ione umuhimu wa kupeleka ajenda ya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu na hata mashuleni, ili kuwajengea uelewa watoto wa Tanzania uelewa na athari ya rushwa hii. 
 
Kwa mfano, hivi karibuni yamekuwapo matukio kadhaa ya wahadhiri kwa vyuo vikuu kuwadhalilisha kingono wanafunzi na huku video zao za utupu zikivuja. Haya na mengine mengi yapo pia katika vyombo vya habari na mahala pa kazi ikiwamo serikalini. 
 
Kwetu sisi TAMWA hili ni janga na ni muuaji wa kimya kimya wa utu wa wanawake,  endapo lisipochukuliwa hatua basi mabinti zetu vyuoni na wanataaluma katika uandishi watapoteza mwelekeo na hivyo tutapoteza vipaji na nguvu kazi, Dk Rose Reuben.
 
 
Kama kauli mbiu ya mwaka huu isemavyo, Haki Sawa kwa maendeleo Endelevu ndivyo tunavyotaka wanahabari wanawake waheshimiwe na wathaminiwe, watimize wajibu wao bila kulazimishwa au kurubuniwa kutoa rushwa ya ngono. 
 
Tunachoweza kusema TAMWA ni; Mwanahabari mwanamke anaweza kuripoti habari za uchunguzi kama mwanaume, anaweza kuripoti michezo kama mwanaume, anaweza kuripoti katika vita kama ilivyo kwa wanaume. Uanamke wake, hauondoi ujasiri, utimamu na umakini katika taaluma  yake. 
 
Kadhalika, Mwanahabari mwanamke hapimwi kwa sura wala sauti yake, bali ujuzi na kipaji katika taaluma yake ya uanahabari. 
 
TAMWA tunasisitiza kuwa hiki ni; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu kama kauli mbiu  ya mwaka huu isemavyo. 
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
 
Dk Rose Reuben
TAMWA
 

User Rating: 2 / 5

Star ActiveStar ActiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Novemba 25, 2021, Dar es Salaam. Leo Dunia inanza madhimisho ya  Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia. 
 
Maadhimisho haya  yanayobebwa na kauli mbiu isemayo; Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa yanakuja wakati ambapo takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kukithiri kwa matukio ya ukatili wa kijinsia, ikiwamo ubakaji hapa nchini.
 
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinasikitishwa na ongezeko la ukatili huu hasa kwa watoto na wanawake ambao ndio tegemeo katika mustakabali wa kimaendeleo nchini. 
 
Akiwa bungeni, Naibu Waziri wa Afya, Mwanaidi Ali Khamis alinukuliwa akisema, kati ya Januari hadi Septemba mwaka huu, watoto 6168 walifanyiwa ukatili wa kijinsia na kati yao, 3524 walibakwa. Wakati huo Naibu Waziri alisema, wanafunzi 1887 walipata ujauzito katika kipindi hicho hicho. 
 
Takwimu hizi zinaamanisha nini? Zinamaanisha kwamba, iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa basi katika kipindi cha mwaka mmoja, zaidi ya watoto 7000 watakuwa wamebakwa au watoto zaidi ya 12,000 watakuwa wamefanyiwa ukatili.
 
Takwimu hizi mpya zinaogofya na kutufanya TAMWA tuone pengine wadau, ikiwamo serikali, wazazi na walezi, tukubaliane na kutamka kuwa; Ubakaji sasa ni janga.
 
TAMWA tunaona ni wakati sahihi sasa, kwa wadau wa masuala ya ukatili wa kijinsia, kukaa pamoja na kupanga mikakati mipya na madhubuti zaidi ya kumaliza au kupunguza matukio haya kwani sheria na sera nzuri zipo lakini ukatili huo bado unaendelea katika jamii yetu. 
 
Hata hivyo tunaipongeza mahakama kwa kutoa hukumu na kufuatilia kwa ukaribu kesi hizi za ubakaji, kwani ipo mifano ya waliohukumiwa kwa kufanya matukio haya. Tunayapongeza madawati ya jinsia kwa kusimamia upelelezi na kutoa ushauri kuhusu matukio au kesi hizi za ubakaji na ukatili mwingine.  Hata hivyo bado matukio haya yanaendelea kuongezeka kila kukicha. Je tatizo lipo wapi? 
 
Ni muhimu kwa taifa, sasa kuendelea kubuni njia mbadala na mpya za kukabiliana na janga hili. Tunaliita janga kwa sababu, watoto 3524 kubakwa si lelemama, bali ni tatizo kubwa katika jamii yetu ambalo linaharibu kabisa mustakabali wa maisha ya kizazi kijacho.
 
Wakati huo huo, bado kinamama wanaendelea kupokea vipigo, kubakwa, kupewa lugha dhalilishi katika jamii yao hali inayowafanya kuwa kundi linaloomboleza na wakati mwingine kuichukia jinsia yao. 
 
"Ukatili huu, una madhara ya muda mfupi, muda mrefu, kiuchumi, kimwili na kisaikolojia kwa wanawake na wasichana na watoto wote kwa ujumla, kwani inawazuia kushiriki kikamilifu na kwa usawa katika jamii yao," Dk Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA. 
 
"Hakuna namna nyepesi ya kuelezea madhara haya ya ukatili wa kijinsia, tumewahi kuona, pengine tumesikia lakini bado jamii nzima haijajua madhara yake kwa kina labda kwa sababu, matukio haya hayatokei kwa wingi mara moja. Lakini tungewapata waathirika hawa na kuwakusanya pamoja, basi Tanzania ingelia," Dkt Reuben.
 
"Ubakaji huu wa watoto ni janga. Serikali itambue kuwa hili ni janga kwa sababu madhara yake yanaweza yasionekana kwa sasa lakini yataonekana baadaye wakati ambapo kizazi hiki cha sasa kitakapokuwa kimeshika usukani" Dkt Reuben.
 
TAMWA inaamini kuwa taifa salama ni lile linalojenga kizazi salama, ambacho waliopo wanawalinda watoto na kumlinda mwanamke. Hivyo basi, ili kuwa na jamii hiyo hatuna budi kuchagizana kwani; waswahili walisema; Kichango ni kuchagizana Kila mmoja ashiriki kwa namna yake kumaliza ukatili huu.
 
Kidunia hali ni kama hii, takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wanawake(UN-Women)zinaonyesha kuwa ukatili wa wanawake aghalabu hufanywa na mwenza, mume wa zamani au wa sasa. Inaelezwa kuwa wanawake zaidi ya milioni 640 wenye umri wa kuanzia miaka 15 na kuendelea waliwahi kufanyiwa ukatili na wenza.
 
Ukatili huu unatajwa kusababisha msongo wa mawazo, kihoro, mimba zisizotarajiwa, magonjwa ya zinaa ikiwamo UKIMWI na wakati mwingine waathirika kujiua. 
 
Takwimu hizo kadhalika zinaeleza kuwa, zaidi ya wanawake 87,000 duniani waliuawa na nusu yao, (50,000) waliuawa na mwenza au mwanafamilia. Zaidi ya thuluthi, waliuawa kwa makusudi na mwenza/mume wa sasa au wa zamani. 
 
TAMWA imeona zaidi kuwa unyanyasaji huu kwa hapa Tanzania umeendelea kujikita pia katika mashindano ya ulimbwende, vyuo vikuu, vyombo vya habari ikiwemo  mitandaonii pamoja na mahala pa kazi. Haya yote yasipofanyiwa kazi, basi tutakuwa na dunia isiyo salama kwa kundi hili.
 
"Tunampongeza Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ameonyesha wazi kuwa anasimamia vyema haki za wanawake na watoto, tumemuona na kumsikia akipinga lugha dhalilishi kwa wanawake na udunishwaji wa kundi hilo katika nafasi za siasa na uongozi. Kongole Rais wetu,"Dkt Rose Reuben
 
TAMWA hatutaacha kusimamia haki za wanawake, watoto na wanahabari, tutaendelea kupaza sauti hadi tutakapoona amani imetawala tukiendelea kusema "Ewe Mwananchi, Pinga ukatili wa kijinsia Sasa”.
 
Kazi iendelee. 
 
Dk. Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
 

Search