- TAMWA
- Hits: 507
Dar es Salaam, Juni 16, 2023. Watanzania leo wanaungana na dunia nzima kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, maadhimisho ya siku hii yalianza mwaka 1991 baada ya kuteuliwa na Umoja wa Afrika katika kuenzi michango ya watoto walioshiriki maandamano Mjini Soweto, Afrika Kusini mwaka 1976 pamoja na kujengea jamii uelewa juu ya umuhimu wa elimu bora kwa watoto.
Kauli mbiu ya maadhimisho haya kitaifa kwa mwaka huu ni “Zingatia Usalama wa Mtoto katika Ulimwengu wa Kidijitali” kauli mbiu hiyo inasisitiza kuwalinda watoto na kuwaongoza kwenye matumizi ya kidijitali ikiwemo simu za mkononi, kompyuta na runinga kwa kuwa vikitumika vibaya vinaweza sababisha ukatili wa mitandaoni kwa watoto.
Siku ya Mtoto wa Afrika hutumika kuwakumbusha watoto wetu hatua ya kijasiri waliyoichukua wenzao huko Afrika Kusini katika kulinda haki zao. Watoto wanakumbushwa kwamba wanaweza kuleta mabadiliko hata wakiwa wadogo.
Kwa hivyo, Siku Ya Mtoto wa Afrika inaadhimishwa kwa maslahi mapana ya watoto wa Afrika na inapaswa sisi watu wazima kujitolea kwa hali na mali katika nafasi zetu ili kushughulikia changamoto nyingi zinazokabili watoto katika bara zima na hasa hapa nyumbani Tanzania.
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) katika kuadhimisha siku hii, tunatoa rai kwa jamii kuweza kuongeza ulinzi kwa watoto kwa kuwakinga na vitendo vya ukatili dhidi yao ikiwemo ukatili wa mitandaoni, mimba za utotoni, ndoa za utotoni, ulawiti, ubakaji, ukeketaji, unyanyapaa na ajira za watoto.
TAMWA kupitia tamko hili ambalo ni sehemu ya maadhimisho, kinamtaka kila mtu kwenye jamii kuwa chachu ya kutengeneza mazingira rafiki kwa watoto kuweza kutoa taarifa endapo ataona viashiria vya ukatili vinavyofanywa na mtu yoyote katika mazingira atakayo kuwepo mtoto ikiwemo ya mitandaoni.
Licha ya kuwepo kwa msukumo wa mabadiliko ya teknolojia yanayopelekea watoto kuhamasika kutumia simu za mkononi, compyuta na runinga katika kupata taarifa, ni jukumu la kila mtu kuwafundisha watoto matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii, pamoja na kuwepo kwa mazingira stahiki ili kuwalinda na ukatili ikiwemo udhalilishaji wa kimtandao,.
Katika mkataba wa haki za mtoto duniani uliopitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa miaka 30 iliyopita umeonesha dhahiri unayosimamia zaidi nguzo kuu nne ambazo ni haki ya kutobaguliwa, kuhakikisha mahitaji yake yanatimizwa, haki ya kuishi na kuendelezwa na haki ya kusikilizwa hivyo hatuna budi kuhakikisha tunatekeleza hilo.
Katika hali isiyo ya kawaida, nyumbani, shuleni, barabarani pamoja na nyumba za ibada zimekuwa ni sehemu zinazoripotiwa kwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto huku wanaokabidhiwa jukumu la kumlinda mtoto wakiwa ndio watuhumiwa wa matukio hayo wakiwemo wazazi, walimu, walezi, ndugu pamoja na majirani.
Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Mambo ya Ndani nchini Tanzania kutoka Julai 2022 hadi Mei 2023, jumla ya mashauri 14,184 ya matukio ya Ukatili wa kijinsia kwa Watoto yalitolewa taarifa katika Vituo vya Polisi ikilinganishwa na matukio 12,642 yaliyotokea Mwaka 2021/22.
Aidha, Katika Hotuba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima alisema “kuanzia Januari 2022 hadi Machi 2023 jumla ya matukio ya Ukatili 15,901 yaliripotiwa Polisi. Kati ya matukio hayo Kesi 671 ndiyo zilifikishwa Mahakamani ambapo 368 zilizotolewa hukumu na kesi 303 zinaendelea”.
Aidha pengine kwa kuongezeka kwa matukio haya inadhihirisha kuwa kuna muamko kwenye jamii katika kuripoti masuala ya ukatili kwa watoto au pengine ni ongezeko la ukatili limezidi na si kwakuwa kuna mwamko wa jamii katika kuripoti matukio hayo.
TAMWA tunatoa wito kwa jamii kuendelea kufichua vitendo hivyo katika vyombo vya usalama ili kutokomeza matukio hayo dhidi ya watoto kwani mtoto wa mwenzio ni wako.
“Kutokomeza ukatili dhidi ya watoto ni jukumu la kila mtu na tusiruhusu mtoto wa kike kupoteza fursa ya elimu na kufurahia utoto wake kwa kumlazimisha kuingia katika ndoa akiwa na umri mdogo pia ni ukiukwaji wa haki za binadamu, hivyo tunaihimiza Serikali kufanyia marekebisho sheria zote zinazokandamiza ustawi wa watoto ikiwemo sheria ya ndoa ya mwaka 1971”.Dkt Rose Reuben
“Ndoa za utotoni ni suala la afya pamoja na ukiukwaji wa haki za binadamu, kwani wasichana walioolewa kwa umri mdogo wana uwezekano mkubwa wa kuathiriwa na fistula na vifo vya kina mama” Dkt Rose
Licha ya juhudi za Tanzania kukomesha ukatili dhidi ya watoto, uelewa kuhusu kinga na mikakati kwa ujumla hautoshi. Ukatili dhidi ya watoto umefichua athari kubwa katika vipengele vya msingi vya afya ya kihisia, kitabia, na kimwili pamoja na maendeleo ya kijamii katika maisha yote na hasa katika mazingira ya elimu ambapo ujuzi wa mtoto unakuzwa.
TAMWA tunatoa wito kwa serikali yetu sikivu, jamii ya watanzania na wadau wote kushirikiana katika kushughulikia matukio ya vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ambayo yanaendelea kushamiri kwa kasi kubwa hapa nchini na duniani kote kama tunavyoshuhudia kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Katika kumlinda mtoto wa afrika TAMWA tunaomba ushirikiano wa wadau wote wakiwemo wazazi, walezi, wanasheria, serikali kwa ujumla, wadau wa maendeleo kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha ulinzi na usalama wa watoto wetu ni wa uhakika na endelevu.
“TAMWA tunampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri mwenye dhamana, ambao wanaonesha wazi kuwa wanasimamia vyema haki za watoto, tumewaona na kuwasikia wakipinga ukatili kwa watoto hatuna budi kusimama nao katika hili “ Dkt Rose Reuben
TAMWA katika kuadhimisha siku hii tunaendelea kufanya kampeni za kuelimisha na kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto kupitia vyombo vya habari na mitandao yetu ya kijamii. (Istagram @tamwa, Twitter @tamwa, pamoja na Facebook @tamwa Tanzania.
Kwa mawasiliano zaidi;
Tanzania Media Women Association (TAMWA)
P.O.BOX 8981, Dar es Salaam
Website: https://www.tamwa.org/
Find us @Facebook, twitter, instagram
Mobile: +255 22 2772681
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimewataka wazazi, walezi, jamii hasa wanahabari kuchukua hatua na kulinda haki za wahanga wa ukatili wa jinsia na usalama wao katika mitandao ya jamii ili kuepusha udhalilishaji zaidi unaoweza kujitokeza.
TAMWA inachukua hatua hii baada ya kuendelea kusambaa kwa video fupi na maudhui, ya binti wa kidato cha tano wa shule ya Panda Hill mkoani Mbeya, aliyetoroka shule na kisha kudaiwa kukimbilia kwa mwanaume aitwaye Baba Jose.
Baada ya kusambaa kwa maudhui hayo, kumeendelea kusambaa video fupi na taarifa mbalimbali zikimuonyesha binti huyo akijieleza na kwenda mbali zaidi kuwa alifanyiwa ukatili wa kijinsia yaani kubakwa na mwalimu wake wa nidhamu, jambo lililovuta maoni mengi dhalili.
Hofu ya TAMWA inajikita zaidi katika utu, usalama, na hatma ya baadaye ya binti huyu ambaye mahojiano yake yanaendelea kusambaa huku wasambazaji na waandaji wa maudhui hayo wakiacha sura yake ionekane wazi wazi, jambo ambalo linavuta hisia na maneno dhalili yanayoweza kuweka usalama wake na afya yake ya akili hatarini.
TAMWA tunaamini kuwa binti huyu bado anayo nafasi ya kujenga hatma yake, hata kuendelea na masomo na baade kuwa mwanajamii mwenye mchango mkubwa kwa taifa.
Pia vyombo vya dola vilivyochukua maelezo yake ya awali vinauwezo wa kuhakikisha haki yake inapatikana vizuri zaidi kuliko mijadala inayozuka baada ya mahojiano yake na waandishi wasiofuata maadili na kusambaza mitandaoni.
Binti huyu bado ana haki ya kulindwa na wazazi, walezi, jamii, serikali na waandishi wa habari na ndio maana TAMWA tunapata wasiwasi anavyoendelea kuhojiwa na kusambazwa mitandaoni ambako kunazua hisia na mijadala dhalili, kutukanwa na kutuhumiwa.
Lakini pia, mpaka sasa inatushangaza kwani hatujaona wazazi au walezi wake wakisimama moja kwa moja kuzungumzia suala hilo na badala yake binti huyo ameachwa kujieleza peke yake kwa wanahabari ambao nao wameshindwa kulinda utu wa muathirika kwa mujibu wa maadili ya uandishi. Maadili ya uanahabari yanasisitiza kuficha sura ya waathrika wa ukatili hata ikiwezekana wazazi wa mtu/mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji, ili kumlinda na kulinda utu wake na kumpunguzia maumivu ya ukatili aliopitia na katika hili binti huyu anastahili kulindwa.
Kwa mujibu wa kanuni zilizotengenezwa Baraza la Habari Tanzania (MCT,2020) ni kinyume cha maadili kuwabainisha watoto walionyanyaswa, kutumika vibaya au walioshtakiwa na kupatikana na hatia ya jinai. Kanuni hizo zinawataka waandishi wa habari kuchukua tahadhari katika kutumia picha na majina na waepuke kuchapisha taarifa kunapokuwa na uwezekano wa kuwaathiri wahusika.
Inaelezwa kuwa baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kutoa amri ya kutafutwa kwa binti huyo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera naye alitoa amri ya kusakwa. Alipopatikana taarifa zinaeleza kuwa, mwanamke aliyejitambulisha kama mama Abdul, ambaye naye alisema, binti huyo alipelekwa kwake na mwanaume mmoja aitwaye baba Jose, ambaye naye alisema: “Ni mke wake ...” Na baada ya hapo vyombo vya dola vilikusanya maelezo.
Katika hali hiyo TAMWA, kama wadau wa habari na watetezi haki za wanawake, wasichana na watoto, tunawataka wazazi, walezi , jamii na wanahabari kuwajibika na kulinda haki za wanawake na watoto, waliopitia ukatili wa kijinsia, ili kuepusha madhara ya kudumu na makubwa zaidi, ya kimwili na kisaikolojia kwa muathirika.
Imetolewa na
Dkt Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji.
Nawasilimu kwa Jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania!
Awali ya yote, napenda kutumiafursa hii kumshukuru mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutukutanisha katika mkutano huu muhimu wa uzinduzi wa utafiti wa haki ya afya ya uzazi kwa wanawake wa mijini na vijijini kupitia vyombo vya habari.
Aidha, nami nichukue nafasi hii kuwapa pole kwa kuondokewa na mmoja wa waanzilishi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Bi. Leyla Sheikh mwezi uliopita “Bwana alitoa Bwana ametwaa, jina lake lihimidiweAmen”
Ni furaha yangu kuungana nanyi katika warsha hii ambayo nimeambiwa ni mwendelezo wa kutekeleza mradi wenu wa Uchechemuzi wa Masuala ya Haki ya Afya ya Uzazi kwa wanawake wa mijini na vijijini kupitia Vyombo vya Habari uliofadhiliwa na Wakfu wa wahisani wa Wellspring.
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Nimeambiwa kuwa, baadhi yenu mmekuwa hapa kwa siku mbili zilizopita mkijifunza na kujadili mchango wa vyombo vya Habari kwa namna ambavyo vyombo hivyo vinaweza kuongeza uelewa wa Haki za Afya ya Uzazi. Niwapongeze sana TAMWA kwa hatua hii ambayo moja kwa moja inalenga ustawi wa jamii yetu kwani uelewa unajengwa kwa taarifa sahihi na waandishi wa Habari mnaweza kufikia watu wengi kwa wakati mmoja.
Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana
Nchi yetu imesaini mikataba mbali mbali ya Kimataifa na Kikanda ambayo ina lengo la kuboresha afya ya uzazi, mama na mtoto. Lengo namba 3 la Maendeleo Endelevu (SDG 3), kipengele cha 7 linazungumzia upatikanaji wa huduma za afya uzazi kwa wote, ikiwemo uzazi wa mpango, kupata habari zinazohusiana na afya ya uzazi na kuweka afya ya uzazi katika mipango ya Serikali, ifikapo mwaka 2030.Aidha, Kifungu namba 14 (g) cha Itifaki ya Maputo (Maputo Protocol) kinazungumzia haki za afya ya uzazi kwa wasichana na wanawake.
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Ikumbukwe kuwa, nchi yetu inatekeleza mikataba hiyo ya kimataifa kwa kuingiza masuala ya afya ya uzazi mama na mtoto katika mipango yake yote kuanzia Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2024/2025), Mpango Mkakati wa Tano wa Sekta ya Afya (2021/2022 – 2024/2025). Mipango hii yote inatekelezwa na Wizara kupitia Mpango mmoja wa Taifa wa afya ya Uzazi, Mama, Mtoto na Lishe (One Plan III). Pamoja na mpango huu kuna Mpango Maalum wa uwekezaji katika afya ya Uzazi kwa Vijana na Kupambabana na Unyanyasaji wa Kijinsia na Unyayasaji dhidi ya Watoto (National Accelerated Action And Investment Agenda For Adolescent Health And Wellbeing - NAIA-AHW) 2021/22 – 2024/25).
Hivyo, sote tunashuhudia kwa namna ambavyo nchi yetu inatilia maanani afya ya Uzazi, mama na Mtoto kupitia miongozo hiyo. Sambamba na hayo, Wizara inafanya jitihada kubwa kuhakikisha kuwa tunatekeleza haki za Afya ya Uzazi katika shughuli zetu za kila siku na tunafanya kazi na wadau mbalimbali wakiwamo mashirika yasiyo ya kiserikali na ndiyo maana nami nimekuja hapa kuungana nanyi kwani tunaelewa kuwa afya ya uzazi sio tu kuwa ni huduma bali pia ni haki ya msingi katika ustawi wa jamii.
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Wizara imeendelea huhakikisha kuwa haki za afya ya uzazi zinapatikana nchini kote ikiwemo kununua na kusambaza bidhaa za uzazi wa mpango. Mathalani, katika kipindi cha Julai 2022 hadi Machi 2023 Serikali ilinunua na kusambaza vidonge vya uzazi wa mpango 2,538,247 sawa na asilimia 89 ya lengo, sindano za uzazi wa mpango aina ya Depo-provera dozi2,564,691 sawa na asilimia 94 ya lengo na vipandikizi 552,494 sawa na asilimia 81 ya lengo. Aidha, Serikali imeendelea kuwapelekea wananchi huduma hizi kwa kufanya huduma za mkoba (outreach services) ambapo asilimia 18 ya wateja wa njia za uzazi wa mpango walipata huduma kupitia njia hii katika kipindi nilichokitaja. Kuongezeka kwa matumizi ya njia za kisasa za uzazi kunadhihirishwa na takwimu za mwaka 2021/2022 (DHS / MIS) ambapo matumizi hayo yameongezeka kutoka asilima 32 (TDHS 2015/16) hadi 38(DHS/MIS 2022/23).
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Pamoja na kutoa huduma za uzazi wa Mpango, Wizara imeendelea kuandaa miongozo, kanuni, sera na sheria mbalimbali zinazowezesha utoaji wa haki za afya ya uzazi kwa wanawake na vijana nchini. Vilevile, huduma za matibabu kwa wanawake ambao wamepata changamoto za kuharibikiwa na mimba au baada ya mimba kutoka (cPAC: comprehensive postabortion care) zinapatikana kuanzia ngazi ya chini ya utoaji wa huduma za afya yaani zahanati na pia mafunzo kwa watoa huduma pamoja na vifaa vinatolewa kwa ajili ya huduma hii.
Jitihada hizi za Serikali katika afya ya uzazi kwa vijana zinaonesha mafanikio kwani Takwimu za mwaka 2021/2022 (DHS/MIS 2021/22) zinaonesha kuwa kiwango cha mimba za utotoni kimeshuka kidogo kutoka asilimia 27 ya mwaka 2015/16 hadi asilimia 22. Ni mategemeo yangu kuwa kwa jitihada za Serikali pamoja na wadau kama TAMWA kiwango hiki kitashuka zaidi.
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Pamoja na mafanikio tunayoyapata katika Sekta ya Afya, ikiwemo katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto bado tuna changamoto ya upungufu wa wataalamu wa kutosha katika kutoa elimu kwa vijana wa uelimishaji rika, muda wa watoa huduma kuwa mdogo na wataalamu kuwa na muda finyu wa kutekeleza majukumu yao kutokana na kukabiliwa na majukumu mengine na uhitaji wa wale wanaowahudumia. Na ili kupambana na hili, Wizara ina mpango wa kurudisha kada ya watumishi wa afya katika ngazi ya Jamii (Community Health Workers) kuanzia mwaka huu wa fedha. Hii itasaidia kuwafikia wananchi walio wengi zaidi kuliko kuwasubiri waje vituoni.
Mtakubaliana na mimi kuwa, ili kuboresha huduma za afya ya uzazi, tunahitaji kupata taarifa sahihi na njia salama, zenye ufanisi, nafuu na zinazokubalika katika upangaji waujauzito kwa kuchagua hivyo basi ni lazima Wananchi wapewe taarifa sahihi ili waweze kujikinga na mimba zisizotarajiwa na magonjwa ya zinaa.
Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana
Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania -TAMWA kimefanya Utafiti unaoonyesha jinsi vyombo vya habari vinavyoandika habari kuhusu wanawake na wasichana wa vijijini na mijini katika haki za afya ya uzazi nchini Tanzania.Utafiti huo ulifanyika kwa kukusanya, kuchambua, na kutoa taarifa za kina zinazotolewa katikavyombo vya habari.
Utafiti huo ulikuwa na madhumuni ya kurutubisha nakuwezesha ustadi wa watendaji wa vyombo vya habari katika kukuza matokeo ya haki za afya ya uzazi na jinsia hapa nchini. Pamoja na hayo,utafiti huo ulilenga kutoa takwimu za msingi zinazohitajika kwa mradi wenye mada isemayo: "Uchechemuzi kupitia vyombo vya habari Vijijini na Mijini kwa Wanawake na Wasichana katika Haki za Afya ya Uzazi wa Kijinsia”nchini Tanzania.
Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana
Katika utafiti huu, tumeambiwa kuwa taarifa kutoka kwa wanawake na wasichana zilikusanywa, kuchambuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya mahojiano na wanahabari, wahariri, watafiti wa vyombo vya habari vya mkoa wa Dar es Salaam na walibaini yafuatayo:
Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ina nia ya kuboresha huduma za afya ya uzazi na kuwalinda wasichana, wanawake na watoto kutokana na unyanyasaji wa kijinsia na unyanyasaji dhidi ya watoto. Vilevile, kuimarisha afya na kuepusha magonjwa yanayosababishwa na ngono, ikiwemo VVU, pamoja na mimba za utotoni. Jitihada hizi zitafanikiwa sana endapo wanahabari watapata taarifa sahihi na za kutosha na za kina kuhusu masuala ya Afya ya Uzazi na kuyafikisha kwa wanachi kwa usahihi wake.
Mwisho,
Kabla sijamaliza hotuba yangu, nitumie fursa hii kwa mara nyingine kuwashukuru Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA) kwa utafiti mzuri ambao umeleta matokeo yatakayosaidia Serikali katika kuboresha utoaji wa huduma za afya hapa nchini ikiwemo huduma za afya ya uzazi mama na mtoto. Wizara inathamini, mchango wa wanahabari kama injini ya kuwafikia wadau na jamii nzima katika kutoa elimu kuhusu umuhimu wa haki za afya ya uzazi. Vilevile, nawashukuru wadau wa sekta ya afya wanaoshirikiana na Serikali katika kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma za afya hapa nchini.
Baada ya kusema haya machache, naushukuru sana uongozi wa TAMWA kwa kunialika katika Warsha ya Uzinduzi wa Utafiti wa Haki ya Afya ya Uzazi kwa Wanawake wa Mijini na Vijijini kupitia vyombo vya Habari
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza