Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam, 15 May, 2022 Wakati dunia  ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya Familia Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA)kinawakumbusha watanzania kutathimini hali ya maendeleo ya familia, na kuwahimiza wazazi na walezi kutoa huduma muhimu za matunzo na kuzuia vitendo vya ukatili kwa watoto ambavyo vimekithiri hapa nchini.
Kama kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inavyosema: Dumisha amani na upendo kwa familia imara, jitokeze kuhesabiwa TAMWA tunawakumbusha wanafamilia kuepuka migogoro inayopelekea kusambaratika na kuacha watoto wakikosa huduma muhimu ikiwamo upendo wa wazazi au walezi.  
“Hivi karibuni kumeripotiwa matukio kadhaa ya ukatili wa watoto ikiwemo vipigo, mauaji, udhalilishaji wa kingono na hata watoto waliojiingiza katika vitendo vya uhalifu maarufu kama Panya Road, ambayo yanaonyesha wazi kuwa ipo hitilafu kubwa iliyoikumba taasisi ya familia Dr. Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji-TAMWA
 Kadhalika  kauli mbiu hii ya kitaifa ya Siku ya Kimataifa ya Familia inazikumbusha familia umuhimu wa kushiriki sensa ya watu na makazi itakayofanyika Agosti 23, mwaka huu, zoezi ambalo litaiwezesha serikali kubaini takwimu sahihi za watu na kaya ili kupanga mipango ya maendeleo kuanzia ngazi ya familia. 
‘Sensa ni zoezi muhimu la kitaifa kwani ni ukweli usiopingika kuwa maslahi ya watoto na sapoti ya familia kama taasisi vinakamilishwa kwa kubainishwa kwa takwimu sahihi za watu, mipango ya kifedha, na rasilimali nyingine zinazomilikiwa na familia, baada ya zoezi hili TAMWA tunaiomba serikali kutengeza Sera ya familia iyakayoainisha wajibu, maslahi ya kiuchumi na mipango kwa familia kama taasisi Dr. Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji- TAMWA
Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloangalia maslahi ya watoto (UNICEF) zinaonyesha kuwa asilimia 60 ya ukatili wa watoto unafanyika majumbani na asilimia 40 unafanyika mashuleni, hivyo kuna umuhimu wa watanzania wote kuthamini na kuimarisha taasisi ya familia kwa upendo na amani.
Pia kwa mujibu wa taarifa za makosa ya ukatili wa jinsia na unyanyasaji zilizotolewa na Jeshi la Polisi katika kipindi cha Januari hadi Disemba mwaka 2021 zinaonyesha mikoa ya kipolisi iliyoongoza kwa ukatili dhidi ya watoto ni Arusha 808, Tanga 691, Shinyanga 505, Mwanza 500 na Ilala 489.  
Kadhalika makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ya matukio ni ya ubakaji 5,899, kumpa mimba mwanafunzi 1677, ulawiti 1,114, kumzorotesha mwanafunzi masomo 790 na shambulio 350. 
Familia ni chanzo cha rasilimali watu, na ndio maana Baraza kuu la Umoja wa Mataifa mnamo mwaka 1993 lilitoa tamko namba 47/237 na  kuitangaza Mei 15 kuwa siku maalumu ya kutathimi hali ya familia, upatikanaji wa huduma muhimu na maendeleo yao.  
TAMWA tunaendelea kusisitiza watanzania, kuthamini ngazi ya familia, kama eneo la kwanza la kuonyesha upendo, kuanzisha maendeleo na kurithisha vizazi vyetu elimu, mali na hekima. 
Ngazi ya familia ndiko kunakoanzia maendeleo, afya na kunakojenga taswira ya tabia ya mtu mmoja mmoja, familia ni muhimu, Dr Rose Reuben. 
Mkurugenzi Mtendaji 
Rose Reuben
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Dar es Salaam, Juni 16, 2023. Watanzania leo wanaungana na dunia nzima kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, maadhimisho ya siku hii  yalianza mwaka 1991 baada ya kuteuliwa na Umoja wa Afrika katika kuenzi michango ya watoto walioshiriki maandamano Mjini Soweto, Afrika Kusini mwaka 1976 pamoja na kujengea jamii uelewa juu ya umuhimu wa elimu bora kwa watoto.

Kauli mbiu ya maadhimisho haya  kitaifa kwa mwaka huu ni “Zingatia Usalama wa Mtoto katika Ulimwengu wa Kidijitali” kauli mbiu hiyo inasisitiza kuwalinda watoto na kuwaongoza kwenye matumizi ya kidijitali ikiwemo simu za mkononi, kompyuta na runinga kwa kuwa vikitumika vibaya vinaweza sababisha  ukatili wa mitandaoni kwa watoto.

Siku ya Mtoto wa Afrika hutumika kuwakumbusha watoto wetu hatua ya kijasiri waliyoichukua wenzao huko Afrika Kusini katika kulinda haki zao. Watoto wanakumbushwa kwamba wanaweza kuleta mabadiliko hata wakiwa wadogo.

 Kwa hivyo, Siku Ya Mtoto wa Afrika inaadhimishwa kwa maslahi mapana ya watoto wa Afrika na inapaswa sisi watu wazima kujitolea kwa hali na mali katika nafasi zetu ili kushughulikia changamoto nyingi zinazokabili watoto katika bara zima na hasa hapa nyumbani Tanzania.

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) katika kuadhimisha siku hii, tunatoa rai kwa jamii kuweza kuongeza ulinzi kwa watoto kwa kuwakinga na vitendo vya ukatili  dhidi yao ikiwemo ukatili wa mitandaoni, mimba za utotoni, ndoa za utotoni, ulawiti, ubakaji, ukeketaji, unyanyapaa na ajira za watoto.

TAMWA kupitia tamko hili ambalo ni sehemu ya maadhimisho, kinamtaka kila mtu kwenye jamii kuwa chachu ya kutengeneza mazingira rafiki kwa watoto kuweza kutoa taarifa  endapo ataona viashiria vya ukatili vinavyofanywa na  mtu yoyote katika mazingira atakayo kuwepo mtoto ikiwemo ya mitandaoni.

Licha ya kuwepo kwa msukumo wa  mabadiliko ya teknolojia yanayopelekea watoto kuhamasika kutumia simu za mkononi, compyuta na runinga katika kupata taarifa, ni jukumu la kila mtu kuwafundisha watoto matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii, pamoja na kuwepo kwa mazingira stahiki ili kuwalinda na ukatili ikiwemo udhalilishaji wa kimtandao,.

Katika mkataba wa haki za mtoto duniani uliopitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa miaka 30 iliyopita umeonesha dhahiri unayosimamia zaidi  nguzo kuu nne ambazo ni haki ya kutobaguliwa, kuhakikisha mahitaji yake yanatimizwa, haki ya kuishi na kuendelezwa na haki ya kusikilizwa hivyo hatuna budi kuhakikisha tunatekeleza hilo.

Katika hali isiyo ya kawaida, nyumbani, shuleni, barabarani pamoja na nyumba za ibada zimekuwa ni sehemu zinazoripotiwa kwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto huku wanaokabidhiwa jukumu la kumlinda mtoto wakiwa ndio watuhumiwa wa matukio hayo wakiwemo  wazazi, walimu, walezi, ndugu pamoja na majirani.

Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Mambo ya Ndani nchini Tanzania kutoka Julai 2022 hadi Mei 2023, jumla ya mashauri 14,184 ya matukio ya Ukatili wa kijinsia kwa Watoto yalitolewa taarifa katika Vituo vya Polisi ikilinganishwa na matukio 12,642 yaliyotokea Mwaka 2021/22.

Aidha, Katika Hotuba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima alisema “kuanzia Januari 2022 hadi Machi 2023 jumla ya matukio ya Ukatili 15,901 yaliripotiwa Polisi. Kati ya matukio hayo Kesi 671 ndiyo zilifikishwa Mahakamani ambapo 368 zilizotolewa hukumu na kesi 303 zinaendelea”.

Aidha pengine kwa kuongezeka kwa matukio haya inadhihirisha  kuwa kuna muamko  kwenye jamii  katika kuripoti  masuala ya ukatili kwa watoto au pengine ni ongezeko la ukatili limezidi na si kwakuwa kuna mwamko wa jamii katika kuripoti matukio hayo.

 TAMWA tunatoa wito kwa jamii kuendelea kufichua vitendo hivyo katika vyombo vya usalama ili kutokomeza matukio hayo  dhidi ya watoto kwani mtoto wa mwenzio ni wako.

“Kutokomeza ukatili dhidi ya watoto ni jukumu la kila mtu na tusiruhusu mtoto wa kike kupoteza fursa ya elimu na kufurahia utoto wake kwa kumlazimisha kuingia katika ndoa akiwa na umri mdogo pia ni ukiukwaji wa haki za binadamu, hivyo tunaihimiza Serikali kufanyia marekebisho sheria zote zinazokandamiza ustawi wa watoto ikiwemo sheria ya ndoa ya mwaka 1971”.Dkt Rose Reuben

“Ndoa za utotoni ni suala la afya pamoja na ukiukwaji wa haki za binadamu, kwani wasichana walioolewa kwa umri mdogo wana uwezekano mkubwa wa kuathiriwa  na fistula na vifo vya kina mama” Dkt Rose

Licha ya juhudi za Tanzania kukomesha ukatili dhidi ya  watoto, uelewa kuhusu kinga na mikakati kwa ujumla hautoshi. Ukatili dhidi ya watoto umefichua athari kubwa katika vipengele vya msingi vya afya ya kihisia, kitabia, na kimwili pamoja na maendeleo ya kijamii katika maisha yote na hasa katika mazingira ya elimu ambapo ujuzi wa mtoto unakuzwa.

TAMWA tunatoa wito kwa serikali yetu sikivu, jamii ya watanzania na wadau wote kushirikiana katika kushughulikia matukio ya vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ambayo yanaendelea kushamiri kwa kasi kubwa hapa nchini na duniani kote kama tunavyoshuhudia kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.

Katika kumlinda mtoto wa afrika TAMWA tunaomba ushirikiano wa wadau wote wakiwemo wazazi, walezi, wanasheria, serikali kwa ujumla, wadau wa maendeleo kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha ulinzi na usalama wa watoto wetu ni wa uhakika na endelevu.

 “TAMWA tunampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri mwenye dhamana, ambao  wanaonesha wazi kuwa wanasimamia vyema haki za  watoto, tumewaona na kuwasikia wakipinga ukatili kwa watoto hatuna budi kusimama nao katika hili “ Dkt Rose Reuben

TAMWA katika kuadhimisha siku hii tunaendelea kufanya kampeni za kuelimisha na kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto kupitia vyombo vya habari na mitandao yetu ya kijamii. (Istagram @tamwa, Twitter @tamwa, pamoja na Facebook @tamwa Tanzania.

Kwa mawasiliano zaidi;

Tanzania Media Women Association (TAMWA)

P.O.BOX 8981, Dar es Salaam

Website: https://www.tamwa.org/

Find us @Facebook, twitter, instagram

Mobile: +255 22 2772681

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Oktoba 11, 2022. Watanzania leo wanaungana na dunia nzima kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Kike. Siku hii inaadhimishwa  ifikapo Oktoba 11 kila mwaka kama wakati wa kukumbushana kuhusu nafasi ya mtoto wa kike katika nyanja mbalimbali, za kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutamaduni.
 
 Hivyo basi kwa kuzingatia umuhimu wa siku hii, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) tunaikumbusha jamii, wadau na serikali kuwa bado matukio ya ukatili wa kijinsia kwa watoto wa kike yanaendelea kushika kasi nchini.
 
Kadhalika, kwa kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu isemayo: Muda Wetu ni sasa, haki zetu, Mustakabali Wetu”. TAMWA na WFT tunalenga kuikumbusha jamii kuendelea kuibua na kuchukua hatua dhidi ya vitendo hivi vya ukatili wa kijinsia, hasa rushwa ya ngono, ubakaji, ulawiti, vipigo na ndoa za mapema kwa watoto wa kike. 
 
TAMWA na WFT tumebaini kuwa licha ya  vyombo vya dola kuchukua hatua na kupinga vikali vitendo hivyo dhidi ya watoto wa kike lakini bado matukio ya rushwa ya ngono, ubakaji, ulawiti, mimba za mapema na udhalilishaji yanazidi kushamiri huku watuhumiwa wengi wakiwamo wazazi, walezi, walimu pamoja na watu wao wa karibu ambao ndio wamepewa jukumu la kulinda watoto hao.
 
Imeshuhudiwa kuwepo kwa matukio kadhaa ya ukatili wa kijinsia kwa  watoto  wa kike katika kipindi cha  Julai hadi  Septemba mwaka huu  jambo ambalo linatupa wasiwasi kuwa huenda elimu ya kulinda haki za mtoto wa kike bado haijawafikia wengi.
 
Baadhi ya matukio hayo ni pamoja na lile la mwanafunzi wa darasa la saba, Shule ya msingi Shahende, Geita, Helena Mashaka (13) anayedaiwa kuchomwa  moto mikononi na mama yake hali iliyosababisha kushindwa kufanya mitihani yake ya darasa la saba. 
 
Kadhalika, mtoto Farida Makuya (16)  anadaiwa kuuwawa usiku wa Jumanne, Oktoba 4, 2022 nyumbani kwao Mtumba jijini Dodoma na watu wasiojulikana. 
 
Wakati huo huo, Padri wa Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kuwabaka na kuwalawiti watoto zaidi ya 10 wa mafundisho ya kipaimara na kisha kuwapa fedha kiasi cha kati ya Sh 3,000 hadi 5, 000. 
 
Tukio jingine ni la mwanafunzi wa darasa la sita, (12), wa Shule ya Msingi Mbagala Kuu, Dar es Salaam,  anadaiwa kubakwa na Mwalimu wake, ambapo  Mwalimu huyo amekuwa akimpatia binti huyo ufunguo wa makazi yake binafsi ili endapo akimuhitaji aweze kufika kwake kwa urahisi.
 
Hata hivyo, tunaipongeza serikali kupitia vyombo vya sheria kwa kutumia muda mfupi kusimamia na kutoa hukumu dhidi ya mwalimu wa shule ya msingi ya Global, Dar es Salaam, aliyehukumiwa kifungo cha maisha kwa kubaka na kulawiti mwanafunzi wa miaka minane. 
 
Utafiti uliofanywa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Watoto (UNICEF) umebaini kuwa wasichana milioni 120, duniani wamewahi kulazimishwa kufanya ngono bila ridhaa yao.
 
Pamoja na ukatili huo kwa watoto wa kike, WFT na TAMWA  bado wanasisitiza jamii kuepuka rushwa ya ngono hasa kwa watoto wa kike. 
 
Mwaka 2020, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ilichapisha ripoti ya utafiti na kuibua kuwepo kwa rushwa ya ngono katika Vyuo Vikuu viwili vya umma nchini, ambavyo ni Chuo kikuu cha Dar Es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM)
 
Kadhalika, mwaka 2021, TAMWA kwa kushirikiana na (WFT) ilitekeleza mradi wa kuangazia rushwa ya ngono kwa wanahabari. TAMWA ilifanya utafiti na kubaini wanahabari wanakabiliwa kwa kiasi kikubwa na rushwa ya ngono na ukatili mwingine ndani ya vyombo vyao vya habari. 
 
TAMWA tumebaini kuwa wasichana wanahabari vyuoni  hukumbana na vitendo vya rushwa ya ngono na kusababisha wengi kuikimbia taaluma  hiyo wakihofia vitendo vya rushwa ya ngono ambayo hukumbana navyo kuanzia wakiwa vyuoni Mkurugenzi wa TAMWA, Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA na WFT bado tunaendelea kuipongeza TAKUKURU kwa kufanya mabadiliko ya kifungu cha 25 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya Mwaka 2007.  Hii ni dhamira chanya kwa serikali katika kushughulikia uovu huu katika nchi yetu. Kwa njia hii, inabakia kuwa sheria ya msingi katika kujenga msingi wa maadili ya taifa katika ngazi na taasisi zote. 
 
“Hata hivyo katika kifungu kidogo cha 2,cha sheria hii,  tumeona kuwa uchambuzi wa sheria unachanganya  neno ukahaba na ngono: Pale ambapo kuna makubaliano ya pande zote, ya kubadilishana ngono kwa ajili ya huduma, au pesa, (katika kesi hii hakuna unyang'anyi wa mamlaka). Hivyo tunaomba kuondolewa kwa kifungu kinacholeta utata kati ya rushwa ya ngono na ukahaba Rose Marandu, Mkurugenzi Mtendaji, WFT
 
Hivyo basi tunapoadhimisha siku hii ya mtoto wa kike, tunatamani dunia itambue thamani yao katika maendeleo, afya yao, elimu yao, uchumi wao na ushiriki wao katika siasa, jamii ikiutambua mchango wao, itasimamia katika ulinzi wao na hivyo kupunguza matukio haya ya rushwa ya ngono. 
Tunaomba serikali kupitia Takukuru, kuendelea kujikita katika mapambano haya wakishirikiana na wadau, ili jamii iwe na taarifa za kutosha kuhusu usalama wa watoto wa kike Rose Marandu,WFT
Hatutaacha, hatutanyamaza, hadi uwepo usalama wa watoto wa kike Tanzania!
 
 
Dkt. Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji
Chama Cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA)
 
 
Rose  Marandu
Mkurugenzi Mtendaji
Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT)
Mwisho

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
June 10th, 2022, Dar es Salaam. The Tanzania Media Womens Association (TAMWA) calls on the Tanzanian government to continue to use the negotiation, and reconciliation process and to follow the procedures for the transfer of land and national resources.
 
The request comes after reports from June 8, 9 and today 10, 2022, showing pastoralists of the Loliondo Maasai tribe and army forces protesting the implementation of the border marking of 1500 square kilometers of their villages for natural resource conservation trending in social media. 
 
We understand and agree with the Prime Minister Kassimu Majaliwa that the loss of peace in any area is causing inconvenience to women, the elderly and children and therefore calls on the government to return to the negotiating table to end the Loliondo conservation crisis with the Maasai community.
 
TAMWA have witnessed many conflicts being resolved through dialogue and reconciliation in this country so we believe that even this conflict can also be resolved without resorting to force or inciting violence that is smearing the nation with human rights abuses.
 
Dr Rose Reuben,
 
 
Executive Director
 
TAMWA

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active
  • Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Mkoa, Bi.AgnessMgaya
  • Mwenyekiti wa Chama cha Waandishiwa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Bi Joyce Shebe
  • Mkurugenziwa Chama wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA, Dr. Rose Reuben.
  • Wanachama wa TAMWA, wakiwamo pia na baadhi ya waanzilishi.
  • Wahariri kutoka Vyombo mbalimbali vya Habari
  • Viongozi wa Asasi za Habari Tanzania,
  • Wanasayansi na watafiti
  • Wadau wa masuala ya jinsia na Afya
  • Waandishiwa Habari,
  • Wageniwaalikwa,
  • Mabibi na Mabwana

 

Nawasilimu kwa Jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania!

Awali ya yote, napenda kutumiafursa hii kumshukuru mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutukutanisha katika mkutano huu muhimu wa uzinduzi wa utafiti wa haki ya afya ya uzazi kwa wanawake wa mijini na vijijini kupitia vyombo vya habari.

Aidha, nami nichukue nafasi hii kuwapa pole kwa kuondokewa na mmoja wa waanzilishi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Bi. Leyla Sheikh mwezi uliopita “Bwana alitoa Bwana ametwaa, jina lake lihimidiweAmen”

Ni furaha yangu kuungana nanyi katika warsha hii ambayo nimeambiwa ni mwendelezo wa kutekeleza mradi wenu wa Uchechemuzi wa Masuala ya Haki ya Afya ya Uzazi kwa wanawake wa mijini na vijijini kupitia Vyombo vya Habari uliofadhiliwa na Wakfu wa wahisani wa Wellspring.

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Nimeambiwa kuwa, baadhi yenu mmekuwa hapa kwa siku mbili zilizopita mkijifunza na kujadili mchango wa vyombo vya Habari kwa namna ambavyo vyombo hivyo vinaweza kuongeza uelewa wa Haki za Afya ya Uzazi. Niwapongeze sana TAMWA kwa hatua hii ambayo moja kwa moja inalenga ustawi wa jamii yetu kwani uelewa unajengwa kwa taarifa sahihi na waandishi wa Habari mnaweza kufikia watu wengi kwa wakati mmoja.

Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana

Nchi yetu imesaini mikataba mbali mbali ya Kimataifa na Kikanda ambayo ina lengo la kuboresha afya ya uzazi, mama na mtoto. Lengo namba 3 la Maendeleo Endelevu (SDG 3), kipengele cha 7 linazungumzia upatikanaji wa huduma za afya uzazi kwa wote, ikiwemo uzazi wa mpango, kupata habari zinazohusiana na afya ya uzazi na kuweka afya ya uzazi katika mipango ya Serikali, ifikapo mwaka 2030.Aidha, Kifungu namba 14 (g) cha Itifaki ya Maputo (Maputo Protocol) kinazungumzia haki za afya ya uzazi kwa wasichana na wanawake.

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Ikumbukwe kuwa, nchi yetu inatekeleza mikataba hiyo ya kimataifa kwa kuingiza masuala ya afya ya uzazi mama na mtoto katika mipango yake yote kuanzia Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2024/2025), Mpango Mkakati wa Tano wa Sekta ya Afya (2021/2022 – 2024/2025). Mipango hii yote inatekelezwa na Wizara kupitia Mpango mmoja wa Taifa wa afya ya Uzazi, Mama, Mtoto na Lishe (One Plan III). Pamoja na mpango huu kuna Mpango Maalum wa uwekezaji katika afya ya Uzazi kwa Vijana na Kupambabana na Unyanyasaji wa Kijinsia na Unyayasaji dhidi ya Watoto (National Accelerated Action And Investment Agenda For Adolescent Health And Wellbeing - NAIA-AHW) 2021/22 – 2024/25).

Hivyo, sote tunashuhudia kwa namna ambavyo nchi yetu inatilia maanani afya ya Uzazi, mama na Mtoto kupitia miongozo hiyo. Sambamba na hayo, Wizara inafanya jitihada kubwa kuhakikisha kuwa tunatekeleza haki za Afya ya Uzazi katika shughuli zetu za kila siku na tunafanya kazi na wadau mbalimbali wakiwamo mashirika yasiyo ya kiserikali na ndiyo maana nami nimekuja hapa kuungana nanyi kwani tunaelewa kuwa afya ya uzazi sio tu kuwa ni huduma bali pia ni haki ya msingi katika ustawi wa jamii.

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Wizara imeendelea huhakikisha kuwa haki za afya ya uzazi zinapatikana nchini kote ikiwemo kununua na kusambaza bidhaa za uzazi wa mpango.  Mathalani, katika kipindi cha Julai 2022 hadi Machi 2023 Serikali ilinunua na kusambaza vidonge vya uzazi wa mpango 2,538,247 sawa na asilimia 89 ya lengo, sindano za uzazi wa mpango aina ya Depo-provera dozi2,564,691 sawa na asilimia 94 ya lengo na vipandikizi 552,494 sawa na asilimia 81 ya lengo. Aidha, Serikali imeendelea kuwapelekea wananchi huduma hizi kwa kufanya huduma za mkoba (outreach services) ambapo asilimia 18 ya wateja wa njia za uzazi wa mpango walipata huduma kupitia njia hii katika kipindi nilichokitaja. Kuongezeka kwa matumizi ya njia za kisasa za uzazi kunadhihirishwa na takwimu za mwaka 2021/2022 (DHS / MIS) ambapo matumizi hayo yameongezeka kutoka asilima 32 (TDHS 2015/16) hadi 38(DHS/MIS 2022/23).

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Pamoja na kutoa huduma za uzazi wa Mpango, Wizara imeendelea kuandaa miongozo, kanuni, sera na sheria mbalimbali zinazowezesha utoaji wa haki za afya ya uzazi kwa wanawake na vijana nchini. Vilevile, huduma za matibabu kwa wanawake ambao wamepata changamoto za kuharibikiwa na mimba au baada ya mimba kutoka (cPAC: comprehensive postabortion care) zinapatikana kuanzia ngazi ya chini ya utoaji wa huduma za afya yaani zahanati na pia mafunzo kwa watoa huduma pamoja na vifaa vinatolewa kwa ajili ya huduma hii.

Jitihada hizi za Serikali katika afya ya uzazi kwa vijana zinaonesha mafanikio kwani Takwimu za mwaka 2021/2022 (DHS/MIS 2021/22) zinaonesha kuwa kiwango cha mimba za utotoni kimeshuka kidogo kutoka asilimia 27 ya mwaka 2015/16 hadi asilimia 22. Ni mategemeo yangu kuwa kwa jitihada za Serikali pamoja na wadau kama TAMWA kiwango hiki kitashuka zaidi.

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Pamoja na mafanikio tunayoyapata katika Sekta ya Afya, ikiwemo katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto bado tuna changamoto ya upungufu wa wataalamu wa kutosha katika kutoa elimu kwa vijana wa uelimishaji rika, muda wa watoa huduma kuwa mdogo na wataalamu kuwa na muda finyu wa kutekeleza majukumu yao kutokana na kukabiliwa na majukumu mengine na uhitaji wa wale wanaowahudumia. Na ili kupambana na hili, Wizara ina mpango wa kurudisha kada ya watumishi wa afya katika ngazi ya Jamii (Community Health Workers) kuanzia mwaka huu wa fedha. Hii itasaidia kuwafikia wananchi walio wengi zaidi kuliko kuwasubiri waje vituoni.

Mtakubaliana na mimi kuwa, ili kuboresha huduma za afya ya uzazi, tunahitaji kupata taarifa sahihi na njia salama, zenye ufanisi, nafuu na zinazokubalika katika upangaji waujauzito kwa kuchagua hivyo basi ni lazima Wananchi wapewe taarifa sahihi ili waweze kujikinga na mimba zisizotarajiwa na magonjwa ya zinaa.

 

Ndugu wana warsha, mabibi na mabwana

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania -TAMWA kimefanya Utafiti unaoonyesha jinsi vyombo vya habari vinavyoandika habari kuhusu wanawake na wasichana wa vijijini na mijini katika haki za afya ya uzazi nchini Tanzania.Utafiti huo ulifanyika kwa kukusanya, kuchambua, na kutoa taarifa za kina zinazotolewa katikavyombo vya habari.

Utafiti huo ulikuwa na madhumuni ya kurutubisha nakuwezesha ustadi wa watendaji wa vyombo vya habari katika kukuza matokeo ya haki za afya ya uzazi na jinsia hapa nchini. Pamoja na hayo,utafiti huo ulilenga kutoa takwimu za msingi zinazohitajika kwa mradi wenye mada isemayo: "Uchechemuzi kupitia vyombo vya habari Vijijini na Mijini kwa Wanawake na Wasichana katika Haki za Afya ya Uzazi wa Kijinsia”nchini Tanzania.

Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana

Katika utafiti huu, tumeambiwa kuwa taarifa kutoka kwa wanawake na wasichana zilikusanywa, kuchambuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya mahojiano na wanahabari, wahariri, watafiti  wa vyombo vya habari vya mkoa wa Dar es Salaam na walibaini yafuatayo:

  • Miongoni mwa vyombo 20 vilivyotumika katika utafiti huu, ilibainika kuwa, nusu hutoa zaidi habari za kisiasa, kijamii na uchumi lakini masuala ya Afya ya Uzazi hayapewi kipa umbele.
  • Wanahabari 125 walithibitisha ukosefu wa maarifa juu ya masuala ya Haki za Afya ya Uzazi (Sexual and Reproductive Health Rights - SRHR)ikiwa ni pamoja na upungufu wa maarifa husika ya kuripoti au kushughulikiamaudhui yanayoleta utata katika utafutaji wa data kutoka kwa watafiti.
  • vyombo vya habari 17 (85%) vinashughulikia programu za Afya ya Uzaziza ndani zinazojumuisha masuala ya Usafi wa Hedhi au UWAKI, nahivyo hawana nafasi au programu maalum za masuala ya afya ya Uzazi isipokuwa kama kuna ufadhili ambao haudumu kwa muda mrefu. Pia, ilielezwa kuwa, ni vyombo 3 (15%) tu vya habari vyenye  programu maalum za Afya ya Uzazi zinazozalishwa na vyombo vya habari maalum vya masuala hayo.
  • Kutokuwepo kwa mitandao maalumu ya wanahabari wa Afya ya Uzazi nchini hususan upande wa Bara ikilinganishwa na masuala mengine ya kijamii, kisiasa au kibiashara kunapunguza ukuzaji wa ajenda hiyo kwa jamii.
  • Uelewa mdogo miongoni mwa wanawake na wasichana wa mijini na vijijini ikiwa ni pamoja na nafasi ndogo ya kutafuta huduma za Afya ya Uzazi.
  • Afya ya Uzazi imebinafsishwa na inahusishwa na kanuni na miiko ya mila na tamaduni, hivyo ni vigumu kupata vyanzo vya habari na kuna utayari mdogo wawatu kujadili jambo hilo kupitia vyombo vya habari.
  • Ushiriki duni kutoka kwa watafiti na taasisi za kitaaluma katika utoaji wa taarifa na takwimu kuhusuHaki za Afya ya Uzazi kwa vyombo vya habari, kwa sababu tu watafitina wasomi wanapendelea jarida, vitabu na mijadala ya kitaaluma.
  • Sera za vyombo vya habari, hazitoi kipaumbele masuala ya Haki za Afya ya Uzazi, kwa sababu hazichangii mapato.
  • Kadhalika utafiti huo ulibaini kuwa, wanahabari wengi hawajapata mafunzo ya Haki za Afya ya Uzazi, ambapo asilimia 76 ya wanahabari waliohojiwa, walisema kuwa, hawajapata mafunzo hayo, na asilimia 22 tu ndiyo waliopata mafunzo.
  • Watafiti 7 waliohojiwa walibaini kuwa kuna haja ya uchechemuzi wa masuala ya Haki ya Afya ya Uzazi na kushauri kuwa, kuna haja ya kuwajengea uwezo wanahabari ili waweze kuripoti masuala ya afya ya uzazi
  • Kwa ujumla afya ya uzazi imekuwa ikitangazwa na kueleweka kama huduma na sio haki kwa wananchi wetu kwani matokeo yanaonyesha kuna uchapishwaji mdogo wa maudhui ya Haki za Afya ya Uzazi.  Pia, hakuna uchapishwaji wa habari za kina za utendaji, kampeni za kiafya, na za uchunguzi kuhusu Haki za Afya ya Uzazi.

 

 

 

Ndugu wanawarsha, mabibi na mabwana

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ina nia ya kuboresha huduma za afya ya uzazi na kuwalinda wasichana, wanawake na watoto kutokana na unyanyasaji wa kijinsia na unyanyasaji dhidi ya watoto. Vilevile, kuimarisha afya na kuepusha magonjwa yanayosababishwa na ngono, ikiwemo VVU, pamoja na mimba za utotoni. Jitihada hizi zitafanikiwa sana endapo wanahabari watapata taarifa sahihi na za kutosha na za kina kuhusu masuala ya Afya ya Uzazi na kuyafikisha kwa wanachi kwa usahihi wake.

Mwisho,

Kabla sijamaliza hotuba yangu, nitumie fursa hii kwa mara nyingine kuwashukuru Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA) kwa utafiti mzuri ambao umeleta matokeo yatakayosaidia Serikali katika kuboresha utoaji wa huduma za afya hapa nchini ikiwemo huduma za afya ya uzazi mama na mtoto.  Wizara inathamini, mchango wa wanahabari kama injini ya kuwafikia wadau na jamii nzima katika kutoa elimu kuhusu umuhimu wa haki za afya ya uzazi. Vilevile, nawashukuru wadau wa sekta ya afya wanaoshirikiana na Serikali katika kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma za afya hapa nchini.

Baada ya kusema haya machache, naushukuru sana uongozi wa TAMWA kwa kunialika katika Warsha ya Uzinduzi wa Utafiti wa Haki ya Afya ya Uzazi kwa Wanawake wa Mijini na Vijijini kupitia vyombo vya Habari

 

 

Ahsanteni sana kwa kunisikiliza

Search