Press Release

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Zanzibar, Septemba 16th, 2020. Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi.
Waheshimiwa viongozi wa dini, wakiwamo maaskofu, masheikh, wachungaji.
Waheshimiwa viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa serikali, wakuu wa vyombo vya usalama na wanahabari. 
Itifaki imezingatiwa!
“Dini mbalimbali, Amani na Upendo, Amani na upendo, Dini mbalimbali!
Kwanza napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mungu kwa kutukutanisha katika kusanyiko hili na kutupa afya njema. 
 Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinayo furaha kubwa na kinatoa shukrani za dhati kwa viongozi wa dini mbalimbali, viongozi wa serikali, wanahabari, vyombo vya usalama na taasisi nyingine zisizo za kiserikali kwa kukubali kujumuika nasi katika warsha hii muhimu. 
 
Ndugu Mgeni Rasmi,
Bila shaka wengi wetu tunafahamu fika kuwa Tanzania inatarajia kufanya uchaguzi mkuu ifikapo Oktoba 28 mwaka huu. 
Kutokana na tukio hilo kubwa la kihistoria, TAMWA imeona ni vyema kuhimiza na kukumbusha suala la nafasi ya mwanamke katika uchaguzi na kuishirikisha kamati ya Amani ya Viongozi wa dini nchini ambayo inaundwa na viongozi wa dini mbalimbali. 
Uwepo wako mahali hapa, ndugu mgeni rasmi, viongozi hawa wa dini na wadau wengine wa masuala ya Amani, umeonyesha dhahiri kuwa jambo hili ni zito na linaonyesha  mmeipa uzito ajenda hii na mnathamini nafasi ya mwanamke katika uchaguzi mkuu ujao.  
 
Ndugu mgeni Rasmi,
Ushiriki wa Wanawake katika siasa na katika ngazi za maamuzi, ni eneo lililo na changamoto lukuki na hivyo linahitaji kuhimizwa na viongozi wa ngazi za juu, asasi za kiraia, wanawake wenyewe na viongozi wa dini. 
Makundi niliyoyataja hapo juu yakitimiza wajibu wake katika kuhimiza na kuelimisha juu ya umuhimu wa wanawake katika uongozi, basi ni dhahiri kuwa, tutafikia ule usawa wa 50 kwa 50 ambao tumekuwa tukiupigia kelele kwa muda mrefu. 
Kwa sasa takwimu zinaonyesha kuwa bado ni asilimi 37 tu ya wanawake ndio walioko katika ngazi za maamuzi bungeni, hata hivyo bado tunaona kuna mapengo katika ushiriki wao ambayo hayana budi kuzibwa.
 
 Ndugu mgeni rasmi,
 Mapengo hayo ni pamoja na lugha dhalilishi wakati wa uchaguzi zinazowakatisha tamaa wanawake kuwania nafasi za uongozi, uteuzi usiozingatia jinsia ndani ya vyama vya siasa, hofu na kutojiamini kwa baadhi ya wanawake wenye nia ya kugombea na ilani za vyama zisizozingatia jinsia. 
Mapengo mengine yaliyobainika ni pamoja na rushwa ya ngono inayotajwa kutumika wakati wa uchaguzi, rushwa ya kifedha, uchumi duni kwa wanawake wanaotaka kugombea na hivyo kupelekea kushindwa kufanya kampeni. 
Mapengo mengine ni mila na desturi kandamizi, zinazowazuia kabisa wanawake wasishiriki katika siasa.
 
Ndugu mgeni rasmi,
Ipo pia mitazamo hasi katika jamii kuwa mwanamke anapoingia katika siasa basi amejishushia heshima na hadhi yake kwani hakuumbwa kuwa kiongozi, hayo yote yanachangia kupunguza idadi ya wanawake viongozi. 
Mapengo mengine ni chama kuwa na mapendekezo na utaratibu binafsi kwa kumthamini mwanaume zaidi hususan katika majimbo ambayo chama kina matarajio makubwa ya ushindi.
 
Ndugu mgeni rasmi na viongozi wa dini, 
TAMWA inawasihi kuendelea kuhimiza umuhimu wa wanawake kushiriki siasa na katika ngazi za maamuzi kwani nyinyi mnaaminika katika jamii kutokana na wajibu wenu mkuu. 
Viongozi wa dini, mna nafasi kubwa katika kuhimiza jamii, kuondoa mila na mitazamo potofu inayochochea ushiriki duni wa wanawake katika siasa na katika ngazi za maamuzi. 
 
 Ndugu mgeni rasmi,
Viongozi wa dini wanategemewa kuhubiri Amani na mshikamano katika kipindi cha uchaguzi na amani hiyo itapatikana iwapo makundi yote maalum wakiwamo watu wenye ulemavu na wanawake, watashiriki kikamilifu katika uchaguzi. 
Ndugu mgeni rasmi.
 Kwa kuwa Tanzania imesaini mikataba mbalimbali inayolenga kuongeza ushiriki wa wanawake katika siasa na mikataba mbalimbali ya amani,  hivyo basi, tunaomba yafuatayo yazingatiwe ili kuondoa vikwazo vyote vinazouia ushiriki wa wanawake katika siasa. 
 
1. Taasisi za dini kutoa elimu kuhusu ushiriki wa wanawake katika siasa na kuondoa mitazamo yote potofu inayokwamisha ushiriki wao  na kutoa mafundisho katika Quran na Biblia yanayomuonyesha mwanamke kama shupavu na mleta mabadiliko ili kuwajengea wanawake kujiamini. 
 
2. Serikali  na viongozi wa dini kukemea na kuwachukulia hatua  wanaotoa lugha dhalilishi  kwa wagombea wanawake wakati wa uchaguzi.
 
3. Vyama vya Siasa vitambue kwamba vina wajibu wa kulinda, kutetea na kudumisha haki na usawa wa Wanawake ndani ya vyama vyao na katika jamii kwa ujumla, kwa kuwa Wanawake ndiyo kundi kubwa la wapiga kura Tanzania. 
 
4. Vyama vya siasa vizingatie mchakato wa uteuzi wa wagombea kwa kuzingatia mrengo wa jinsia, kama Sheria Mpya ya Uchaguzi inavyoainisha.
 
5. Tunawaomba wanahabari kutumia kalamu zao kimaadili kwa kuepuka kuchochea lugha dhalilishi na kuidunisha taswira ya mwanamke katika jamii. 
 
6. Vyombo vya vya habari na wanahabari wanapaswa kupaza sauti zao kuhimiza ushiriki wa wanawake katika siasa na kulinda utu wake ili kuleta Amani na ushiriki kamilifu katika uchaguzi.
 
7. Wanawake waondoe dhana chonganishi zinazoenezwa kuwa hawapendani na hawawezi bali waendelee kusimama imara na kujitokeza kwa wingi katika chaguzi zijazo.
 
TAMWA tunaliombea Taifa likatawaliwe na upendo, Amani na mshikamano katika uchaguzi mkuu ujao Oktoba 28.
 Mungu ibariki Tanzania!
 
Rose Reuben.
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Chama cha wanahabari wanawake Tanzania TAMWA, kinaungana na watanzania wote , wakiwemo watoto wa tanzania, kuadhimisha siku ya mtoto wa Afrika. Hii ni siku muhimu sana kwa sababu wadau, jamii na nchi kwa ujumla wake, tunapaswa kutafakari masuala mbalimbali yanayohusu watoto kupitia siku hii.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Dar es Salaam, Mei, 20. 2022.  Imekuwa ni ada sasa kwa duru zetu za habari kutawaliwa na  matukio ya ubakaji hasa kwa watoto.

Katika kipindi cha Januari hadi Mei mwaka huu, matukio makubwa yaliyotikisa vyombo vya habari ni pamoja na lile la mkoani Katavi, ambapo mwalimu wa Mafundisho ya dini ya Kikristo Joseph John, kukamatwa kwa kulawiti watoto wanne.

Tukio jingine ni lile la mkazi wa Iringa, kudaiwa kumlawiti mtoto wake  wa kambo na shemeji yake. Kadhalika, liliripotiwa tukio lililobeba vichwa vingi vya habari la mtoto wa miaka 14 mkazi wa Iringa, kuwalawiti watoto wenzake 14 wote wa kiume.

Kadhalika hili la juzi, Mei 18 ambapo mwalimu wa Madrasa Jumanne Ikungi, mkazi wa Arusha kwa tuhuma za kuwalawiti wanafunzi takribani 22 wa shule ya msingi Mkonoo, jijini Arusha. Mkuu wa wilaya ya Arusha, Said Mtanda alithibitisha  baada ya kufika katika shule hiyo na kuzungumza na wazazi, walimu na wanafunzi ikiwa ni baada ya kukamilisha alichokiita uchunguzi wake juu ya mwalimu huyo wa madrasa.

 Kwa matukio hayo yaliyoripotiwa kati ya Januari na Mei, inatosha kusema kuwa watoto wetu hawapo salama na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) tunalazimika kusema, ‘watoto hawa hawana pa kukimbilia’.

“Mwenendo huu wa matukio ya ubakaji na ulawiti wa watoto tena na walimu, viongozi wa dini na wazazi au walezi, unadhihirisha kuwa tatizo hili bado ni kubwa nchini na linahitaji maamuzi magumu kutoka kwa watunga sera wetu,” Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben.

TAMWA pamoja na wadau wengine wa masuala ya jinsia, tumekuwa tukiimba wa kuitaka jamii kuzuia ukatili kwa miaka zaidi ya 30 sasa tukililia mabadiliko ya sera, sheria na hata kutoa elimu kwa jamii. Lakini bado tatizo hili linaendelea, tena sasa likitekelezwa na viongozi waliotegemewa kuwalinda watoto wetu, tuliodhani kuwa ni walimu wa kukuza maadili mema kwa watoto.

“Tunahitaji zaidi ya sheria kukomesha ukatili huu, tunahitaji maamuzi magumu kutoka ngazi zote kuanzia familia, wanajamii, viongozi wa dini zote na serikali kwa ujumla wake kwa sababu watoto walio taifa la kesho, wanaharibiwa kimwili na kisaikolojia” Dk Rose Reuben.

Wakati huo huo, taarifa za makosa ya ukatili wa jinsia na unyanyasaji zilizotolewa na Jeshi la Polisi katika kipindi cha Januari hadi Disemba 2021 zinaonyesha mikoa ya kipolisi iliyoongoza kwa ukatili dhidi ya watoto ni Arusha 808, Tanga 691, Shinyanga 505, Mwanza 500 na Ilala 489. 

Kadhalika makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ya matukio ni ya ubakaji 5,899, kumpa mimba mwanafunzi 1677, ulawiti 1,114, kumzorotesha mwanafunzi masomo 790 na shambulio 350.

Wakati tukiendelea kutafuta suluhisho la janga hili, TAMWA inaendelea kutoa elimu katika shule za sekondari na msingi, kuhusu mada za ukatili wa kijinsia, lakini bado hakuna mitaala shuleni inayogusa masuala ya afya ya uzazi moja kwa moja.

“Utafiti uliotolewa hivi karibuni na Taasisi ya Haki Elimu, unaonyesha kuwa watoto wengi hawafundishwi elimu ya afya ya uzazi, lakini  zaidi hasa walimu nao wanaogopa kufundisha wanafunzi mada hizo, hapa ndipo mzizi wa tatizo ulipo,”

“Ni dhahiri kuwa mambo yanayouhusu afya ya uzazi na ukatili wa kingono hayazungumzwi ndani ya familia wala shuleni tena wengine wanaona ni mambo ya aibu yasiyostahili kujadiliwa, hivyo yanabaki kuwa masuala ya wadau na serikali ambao nao husuluhisha tatizo na sio mzizi wa tatizo,” Dk Rose Reuben.

Wakati tukijiandaa na zoezi la Sensa ya Watu na Makazi, ifikapo Agosti 23,  ni wakati muhimu kwa  viongozi, wazazi, walezi, wasimamizi wa sheria, wadau wa masuala ya jinsia na watoto kujitathmini wapi penye mapengo, ili tuzibe ombwe hili la ubakaji wa watoto.

TAMWA imesikitishwa na ubakaji huu wa watoto unaoendelea hapa nchini na tunamuomba Rais Samia Suluhu Hassan, kutamka kuwa hili ni janga na kutoa maamuzi magumu kunusuru watoto wetu.

 Dk Rose Reuben

Mkurugenzi Mtendaji

TAMWA

User Rating: 3 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar InactiveStar Inactive

Dar Es Salaam , Oktoba 2, 2020.

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) tunachukua fursa hii, kuutambulisha kwenu mradi wa “Rushwa ya ngono miongoni wanahabari wanawake katika vyombo vya habari” unaofadhiliwa na Mfuko wa Wanawake Tanzania - Women Fund Tanzania (WFT).

TAMWA ilianzishwa 1987, na wanahabari wanawake, kwa lengo la utetezi wa ustawi wa haki za wanawake na watoto kupitia taaluma yao na vyombo vya habari.

“Kwa kuwa TAMWA kiini chake ni wanahabari,  hivyo basi jukumu la utekelezaji wa mradi huu, unaowalenga wanahabari litakwenda kutekelezwa kwa kiasi kikubwa kwa kushirikiana na nyinyi wanahabari na vyombo vya habari,” Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA.

TAMWA tunakwenda kuutekeleza mradi huu tukifahamu kabisa kuwa zipo tafiti mbalimbali zinazoonyesha kuwa bado kuna rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari.

“Wakati huo huo, wanahabari wameonekana kuwa kimya kuhusu matukio hayo, aidha kwa kuogopa kupoteza ajira zao au pengine wakichelea kuaibika zaidi pindi watakapoweka wazi masahibu yao,” Reuben

Kimsingi, rushwa ya ngono haikubaliki na ni tabia isiyopendeza inayoshusha utu na kuwafanya waathirika kudhalilika, kupata msongo wa mawazo na kukosa kujiamini mahala pa kazi, lakini baya zaidi ni kuwa matukio mengi hayaripotiwi.

Baadhi ya watafiti, kama Barton A na Storm, (2014) walibaini kuwa asilimia 48 ya wanahabari wanawake waliohojiwa walikiri kuwa wamewahi kukumbana na  rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari kwa namna moja au nyingine na asilimia 83 kati ya hao, walisema hawakuripoti matukio hayo.

“Ombwe hili ni kubwa na huenda likawaathiri hata wanahabari wachanga walio vyuoni, ambao huenda wakakataa tamaa ya kuingia katika tasnia hii na hivyo kuizorotesha tasnia lakini baya zaidi, kukosa wanahabari wanawake katika nafasi za juu za uongozi na wenye mafanikio katika tasnia hiyo,”Reuben

Kadhalika, imebainika kuwa vyombo vyingi vya habari nchini havina sera madhubuti zilizowekwa kuwaongoza wanahabari katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinapowakumba ikiwamo masuala ya rushwa ya ngono katika mazingira ya kazi   na  hivyo kuchangia kuongezeka kwa visa vya rushwa ya ngono.

“Hivyo basi, kukiwa na ombwe kama hilo, TAMWA katika utekelezaji wa mradi huu, itafanya tathmini kwa kupitia maswali, ili kujua yanayowasibu wanahabari” Reuben

Kadhalika, TAMWA itawajengea uwezo wanahabari, wakiwamo wahariri na wanawake wanahabari walio katika vyombo vya habari.

Kisha, TAMWA itashirikiana na vyombo vya habari kufanya uchechemuzi, kufanya mazungumzo  na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuwashirikisha matokeo ya tathmini na kuelimisha jamii kuhusu rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya Habari na kwa kutumia mitandao ya kijamii.

Katika mradi huo TAMWA itashirikisha wadau mbalimbali  wa habari wakiwamo, MISA, TEF, MCT, TCRA na OSHA.

Mradi huo utatekelezwa jijini Dar es salaam ambapo ni kitovu cha vyombo vyingi vya habari nchini zikiwamo Redio, Runinga, magazeti na mitandao ya kijamii.

TAMWA inaamini kuwa kwa kufanya tathimini ya rushwa ya ngono katika vyombo vya habari na kuwajengea kuwajengea uwezo wanahabari, itawawezesha pia kufichua na kuandika vyema habari zinazohusu rushwa hii ambayo kwa mujibu wa mila na desturi za watanzania walio wengi imekuwa ikizungumzwa kwa kwa kificho au kutokuzungumzwa kabisa.

TAMWA inatambua kuwa uwepowa Sheria ya Rushwa ya ngono ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU)

Lakini zaidi hasa, tunataka wanahabari wapaze sauti zao, tuvunje ukimya, wayazungumze yanayowasibu, na kuondoa kabisa ukatili wa kijinsia wa aina hii ambao unachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya tasnia ya habari ikiwa ni pamoja na kuua vipaji.

Pasipo kuvunja ukimya uliotanda dhidi ya suala la rushwa ya ngono, waathirika kujengewa uwezo wa kukusanya vidhibiti visivyokuwa na mashaka yoyote taasisi yenye mamlaka ya kushughulikia makosa haya haziwezi kufanya kazi yake kwa ufasaha na kuleta mabadiliko katika jamii yetu.

Kadhalika serikali, taasisi za habari na za jinsia, zinatakiwa kushirikiana kumaliza tatizo hili ambalo halijazungumzwa kwa kina ili tuvunje ukimya huu.

Mkurugenzi Mtendaji

Rose Reuben

TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Novemba 29, 2022, Dar es Salaam. Miaka minne iliyopita, Chama cha  Wanahabari Tanzania(TAMWA) ilitekeleza mradi wake wa kuchapisha habari za uchunguzi juu ya unyanyasaji wa kingono mahala pa kazi na vyuo vikuu.
 
Mwaka mmoja uliopita, TAMWA ilitekeleza mradi mwingine uliofanana na huu, kwa kufanya utafiti kuangalia hali halisi ya rushwa ya ngono katika vyumba vya habari. 
Yote haya, yaliiwezesha TAMWA kubaini kuwa kuna tatizo  kubwa la rushwa ya ngono na unyanyasaji wa kingono mahala pa kazi na katika elimu ya vyuo vikuu. Matokeo ya tafiti na uchapishaji wa habari kuhusu rushwa ya ngono, yalichagiza wadau na waathirika kuweka wazi hali halisi ya rushwa ya ngono na unyanyasaji wa kingono katika mazingira ya kazi na elimu.  
 
Hivyo basi, leo wakati dunia inafanya maadhimisho ya Siku 16 kupinga ukatili wa jinsia,  yanayokwenda na kauli mbiu isemayo: Kila uhai una thamani, tokomeza mauaji na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto.
 
TAMWA  kwa kushirikiana na wanamtandao wa kupinga ukatili wa jinsia hapa nchini pamoja na  wadau wetu wa maendeleo  kwanza tunajisikia fahari kuibua mengi kuhusu athari ya rushwa ya ngono na unyanyasaji wa kingono mahala pa kazi na katika taasisi za elimu na kwa kuendeleza mjadala huu katika jamii kupitia vyombo vya habari.
 
TAMWA kupitia miradi yake inayohimiza kuzuia ukatili katika jamii, tumeweza kufanya yafuatayo;
Kwanza, kuvunja ukimya uliotawala miongoni mwa wanahabari katika kusema kinagaubaga au kundika kuhusu madhila wanayopitia wanapodhalilishwa kingono.
 
TAMWA imebaini asilimia 48 tu ya wanahabari ndio wanaoweza kusema wazi kuhusu madhila ya rushwa ya ngono wanayopitia katika vyumba vya habari. Asilimia 52 inayobaki, hawawezi kusema wazi kuhusu changamoto hiyo.
Kadhalika TAMWA kwa kushirikiana na wadau wakiwamo Internews na WFT na Tasisi ya kuzuia Rushwa (TAKUKURU)wamebaini kuwa rushwa ya ngono katika vyuo vikuu ni janga kubwa linalochagiza kushuka kwa kiwango cha taaluma, kuzalisha wahitimu wasio na sifa na kuharibu talanta kwa wale wanaokataa rushwa hiyo. 
 
Tumebaini kuwa wanahabari wengi wanawake wameacha kazi kwa kuhofia udhalilishaji wa kijinsia katika tasnia hiyo, wapo wanafunzi waliohama vyuo na kuacha shule kwa kuombwa rushwa ya ngono.  
Kadhalika, imebainika kuwa wapo viongozi katika maeneo ya kazi, wanaotoa kazi kwa upendeleo kwa kuomba rushwa ya ngono badala ya kuangalia uwezo na vipaji. 
Juzi akifungua kongamano la wadau wa rushwa ya ngono kwa wanafunzi na wakufunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, jijini Dodoma, Naibu Waziri Utumishi, Deogratius Ndejembi, amesema rushwa ya ngono inasababisha kuzalishwa wasomi wasio na tija na kuwanyima haki wanafunzi.  
Kauli ya Ndejembi inachochea mjadala unaoonyesha  zaidi ukubwa wa tatizo hili na kutukumbusha watanzania  kuchukua hatua za ziada  kupambana na rushwa ya ngono mashuleni, vyuoni na katika sekta ya ajira na utumishi wa umma, tatizo ambalo linatishia kuharibu vipaji. 
“Hivyo basi, huu ni wakati kwa wadau wanaopinga ukatili wa  jinsia, watetezi wa haki za binadamu, wahanga wa ukatili na serikali   kukumbushana kuwa rushwa hii inavunja haki za binadamu, ni kosa la jinai kisheria, inaharibu utu, na inaua vipaji hapa nchini amesema Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA na WFT Tunaiomba serikali kama ambavyo tayari imeshaanza kulichukulia kwa uzito suala hili, iendelee kuwawajibisha wale wanaomba rushwa ya ngono kwa wanafunzi na kwa wafanyakazi.Kadhalika, , tunaomba wanafamilia, wanawake  na wanaume, vijana wa kike na wakiume na jamii kwa ujumla,  wadau wa kuzuia ukatili wa jinsia, wahanga wa rushwa ya ngono na unyanyasaji wa kingono kushiriki katika mijadala inayoweza kuleta suluhisho la janga hili tupinge ukatili wa kijinsia na kuhamasisha uwazi zaidi. 
 
“Sote tunaweza kuwa watetezi na sauti zetu kwa pamoja zinaweza kuleta  mabadiliko tunayotafutaDr Rose Reuben.
 
Tunapoadhimisha Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, TAMWA tunatamani  kuwa asiwepo yeyote, popote pale, atakayefanyiwa  ukatili wa kijinsia hapa nchini. Lakini zaidi hasa tunasema; Rushwa ya ngono mahala pa kazi, vyuoni na mashuleni ni janga na inarudisha nyuma maendeleo ya jamii yetu.
Dr Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA.

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active

Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimewataka wazazi, walezi, jamii hasa wanahabari kuchukua hatua na kulinda haki za wahanga wa ukatili wa jinsia na usalama wao katika mitandao ya jamii ili kuepusha udhalilishaji zaidi unaoweza kujitokeza.


TAMWA inachukua hatua hii baada ya kuendelea kusambaa kwa video fupi na maudhui, ya binti wa kidato cha tano wa shule ya Panda Hill mkoani Mbeya, aliyetoroka shule na kisha kudaiwa kukimbilia kwa mwanaume aitwaye Baba Jose.


Baada ya kusambaa kwa maudhui hayo, kumeendelea kusambaa video fupi na taarifa mbalimbali zikimuonyesha binti huyo akijieleza na kwenda mbali zaidi kuwa alifanyiwa ukatili wa kijinsia yaani kubakwa na mwalimu wake wa nidhamu, jambo lililovuta maoni mengi dhalili.


Hofu ya TAMWA inajikita zaidi katika utu, usalama, na hatma ya baadaye ya binti huyu ambaye mahojiano yake yanaendelea kusambaa huku wasambazaji na waandaji wa maudhui hayo wakiacha sura yake ionekane wazi wazi, jambo ambalo linavuta hisia na maneno dhalili yanayoweza kuweka usalama wake na afya yake ya akili hatarini.


TAMWA tunaamini kuwa binti huyu bado anayo nafasi ya kujenga hatma yake, hata kuendelea na masomo na baade kuwa mwanajamii mwenye mchango mkubwa kwa taifa.
Pia vyombo vya dola vilivyochukua maelezo yake ya awali vinauwezo wa kuhakikisha haki yake inapatikana vizuri zaidi kuliko mijadala inayozuka baada ya mahojiano yake na waandishi wasiofuata maadili na kusambaza mitandaoni.
Binti huyu bado ana haki ya kulindwa na wazazi, walezi, jamii, serikali na waandishi wa habari na ndio maana TAMWA tunapata wasiwasi anavyoendelea kuhojiwa na kusambazwa mitandaoni ambako kunazua hisia na mijadala dhalili, kutukanwa na kutuhumiwa.


Lakini pia, mpaka sasa inatushangaza kwani hatujaona wazazi au walezi wake wakisimama moja kwa moja kuzungumzia suala hilo na badala yake binti huyo ameachwa kujieleza peke yake kwa wanahabari ambao nao wameshindwa kulinda utu wa muathirika kwa mujibu wa maadili ya uandishi. Maadili ya uanahabari yanasisitiza kuficha sura ya waathrika wa ukatili hata ikiwezekana wazazi wa mtu/mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji, ili kumlinda na kulinda utu wake na kumpunguzia maumivu ya ukatili aliopitia na katika hili binti huyu anastahili kulindwa.

Kwa mujibu wa kanuni zilizotengenezwa Baraza la Habari Tanzania (MCT,2020) ni kinyume cha maadili kuwabainisha watoto walionyanyaswa, kutumika vibaya au walioshtakiwa na kupatikana na hatia ya jinai. Kanuni hizo zinawataka waandishi wa habari kuchukua tahadhari katika kutumia picha na majina na waepuke kuchapisha taarifa kunapokuwa na uwezekano wa kuwaathiri wahusika.


Inaelezwa kuwa baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kutoa amri ya kutafutwa kwa binti huyo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera naye alitoa amri ya kusakwa. Alipopatikana taarifa zinaeleza kuwa, mwanamke aliyejitambulisha kama mama Abdul, ambaye naye alisema, binti huyo alipelekwa kwake na mwanaume mmoja aitwaye baba Jose, ambaye naye alisema: “Ni mke wake ...” Na baada ya hapo vyombo vya dola vilikusanya maelezo.

Katika hali hiyo TAMWA, kama wadau wa habari na watetezi haki za wanawake, wasichana na watoto, tunawataka wazazi, walezi , jamii na wanahabari kuwajibika na kulinda haki za wanawake na watoto, waliopitia ukatili wa kijinsia, ili kuepusha madhara ya kudumu na makubwa zaidi, ya kimwili na kisaikolojia kwa muathirika.


Imetolewa na


Dkt Rose Reuben

Mkurugenzi Mtendaji.

Search