Press Release

User Rating: 3 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Julai 20, 2021.
Leo Julai 20, gazeti la Jamhuri, linalotolewa kila wiki, katika ukurasa wake wa kwanza na kuendelea ukurasa wa tatu limeandika habari yenye kichwa  kinachosema: Mambo ya Nje haijamchukulia hatua Balozi".
Katika habari hiyo, inayomtuhumu Balozi wa Libya nchini Tanzania, Bwana Kamal Ramadan Krista kuhusika katika usafirishaji haramu wa wasichana na unyanyasaji wa kingono, Mkurugenzi wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Dk Rose Reuben amenukuliwa akisema kuwa: Sina maoni yoyote kwa sababu habari hii haikufanyiwa uchunguzi wa kutosha
Taarifa hiyo ikaeleza zaidi kuwa Dk Rose“Alipoelezwa kuwa suala hilo ni la kukiukwa kwa haki za watoto wa kike na kusafirishwa nje ya nchi kinyume na sheria huku TAMWA ikijipambanua kuwa watetezi wa haki za wanawake, alishauri watafutwe Polisi wa Kimataifa(Interpol) na Idara ya Uhamiaji. 
Aya ya mwisho ya habari hiyo imesema: Mkurugenzi huyo ameonyesha kutofurahishwa na gazeti la Jamhuri kuandika tuhuma dhidi ya mwanadiplomasia huyo.
Mkurugenzi wa TAMWA anakiri kupigiwa simu na kutembelewa na mwandishi wa Habari wa gazeti hilo Bwana Alex Kizenga tarehe 16 Julai mwaka huu majira ya mchana ambako alihitaji maoni dhidi ya Habari iliyochapishwa katika gazeti hilo wiki tatu nyuma iliyomtuhumu Balozi Krista kusafirisha wasichana wa kitanzania kwenda kufanya biashara ya ngono nchini mwake.   
Mbali na kukataa kutoa maoni kuhusu Habari hiyo kwa msimamo kuwa haikuwa na taarifa kutoka vyanzo vya msingi ama vilelezo. Mkurugenzi wa TAMWA hakukubali kutoa maoni wala kuzungumza maneno kama ilivyonukuliwa na gazeti hilo na  badala yake mhariri na mwandishi  wa Jamhuri Media ambao walidhamiria kumuandika katika taarifa hiyo wamemlisha maneno Mkurugenzi wa TAMWA Dk Rose Reuben.
Ifahamike kuwa chama hiki ni cha kihabari na hivyo kinafahamu misingi yote ya taaluma ya habari na mawasiliano na hivyo tunasikitishwa na mmonyonyoko huu wa maadili uliofanywa  na gazeti la Jamhuri.
Kwa unyenyekevu tunawataka waombe radhi katika gazeti hilo. 
Kadhalika, TAMWA inafanya kazi na wanahabari kila siku na imekuwa ikiruhusu mahojiano na Mkurugenzi Dk Rose Reuben bila kuweka vikwazo, lakini endapo chama hakijatoa ruhusa ya kunukuliwa, basi maombi hayo yaheshimiwe kama maadili ya kihabari yanavyofundisha. 
Kwa kuwa TAMWA ni sehemu ya wanahabari, tunapenda kutoa wito kwa wanahabari wote kufuata misingi na maadili ya habari pindi wanapotimiza majukumu yao. 
Dkt. Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji ~ TAMWA.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Mei 3 kila mwaka Duniani kote tunaadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari, Tangu umoja wa mataifa ilipoidhinisha siku hiyo mwaka 1993, Hapa nchini kama wadau na wanahabari tumeendeleza utaratibu huu wa kusherekea maadhimisho haya ambapo kwa mwaka huu  kauli mbiu yake ni “Habari kwa manufaa ya Umma”. 
Lengo la maadhimisho haya ni kukuza uelewa wa umuhimu wa uhuru wa vyombo vya habari na kukumbusha serikali na jamii umuhimu wa kuheshimu na kulinda haki ya uhuru wa Habari kama inavyolindwa katika Ibara ya 19 ya tamko la ulimwengu la haki za binadamu. 
Tunapoelekea  kilele cha maadhimisho haya, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Taasisi zaidi ya 20  za kihabari za kitaifa na kimataifa nchini chini ya Shirika la umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni (UNESCO), Tunaungana na jamii na  ulimwengu  kuadhimisha siku hii adhimu ambayo sherehe za kilele zitafanyika Jijini Arusha siku ya tarehe 3 mwezi wa 5 2021.
TAMWA kwa niaba ya waandaaji wa maadhimisho haya  tunapenda kutoa salamu za pole kwa serikali ya jamuhuli ya muungano wa Tanzania na kwa wananchi wote kwakuondokewa na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano Hayati Dk.John Joseph Pombe Magufuli, Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi Amina.
“Tusimame dakika moja kumuombea Hayati Rais wa awamu ya tano Dk. John Joseph Pombe Magufuli”.
Katika siku hii TAMWA tunawiwa kuikumbusha serikali umuhimu wa kulinda uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari kwa ujumla pia kupongeza serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania MHE. Samia Suluhu Hassan kwakuona umuhimu wa vyombo vya habari kufanya kazi zao kwa  uhuru na kujali uzalendo wa nchi  bila kuvunja sheria.
Rais Samia mapema aliposhika nyazfa ya urais, Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa kuwaapisha makatibu wakuu na naibu makatibu wakuu  alimwagiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuvifungulia vyombo vya habari vilivyofungiwa na kuagiza wahusika kutotumia ubabe kuvidhibiti. 
Pia alishauri Vyombo vya habari visifungiwe kibabe na kuongeza kuwa namnukuu “Watakapofanya makosa adhabu zitolewe kulingana na sheria inavyoelekeza, viacheni vifanye kazi yao isionekane wanazuiwa kuongea,”.
TAMWA kikiwa ni chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania na kufanya shughuli zake nyingi kwa kutumia vyombo vya habari kimefarijika sana kusikia na kuona namna kiongozi wa nchi kulipa uzito suala hili mara tu aliposhika nyazfa hiyo.
Katika Jamii yetu vitendo vya kupokwa kwa uhuru wa habari kwa wanahabari pamoja na Tasnia yote kwa ujumla vimekuwa vikitendwa mara kwa mara na baadhi ya viongozi katika Nyanja mbalimbali za Serikali bila kujali kuwa ni uvunjifu wa haki kwa tasnia ya habari na kwa jamii kwa ujumla.
Ukamataji wa wanahabari kinyume na sheria: Ukamataji wa waandishi wa habari kinyume na sheria mwanzoni mwa mwaka huu tuliona kwa aliyekuwa  Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke Mhe. Lusubilo Mwakabibi, alituhumiwa kuwaweka chini ya ulinzi kwa saa 3 Wanahabari wawili kutokana na kuhudhuria Mkutano wake na Wafanyabiashara wa soko la Mbagala Rangi Tatu pasipo kupewa mwaliko, Wanahabari hao ni Christopher James kutoka ITV & Radio One pamoja na Dickson Billikwija wa Island TV. 
Haki ya Uhuru wa Vyombo vya Habari na wanahabari ni moja ya haki ya msingi ya kiraia ambayo huwapa jamii haki yao ya kupata habari na kusambaza taarifa, haki ya uhuru wa kujieleza pamoja na haki ya uhuru wa maoni ambazo ni haki za msingi katika mataifa yanayojiendesha kwa misingi ya demokrasia.
Uwepo wa sheria kandamizi: Katika hili tumeona sheria kandamizi zimeendelea kuwa kikwazo katika utekelezaji na uhabarishaji na uhuru wa kujieleza nchini Tanzania, kama sheria ya makosa ya kimtandao ya mwaka 2015, Sheria ya upatikanaji wa habari 2016 na kanuni ya maudhui ya kimtandao, Sheria hizi zina vifungu amabvyo havijakidhi viwango vya kimataifa vya uhuru wa kujieleza.
 Ukatili wa kijinsia katika vyombo vya habari: Tafiti ndogo iliyofanywa na Shirika la umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni (UNESCO), tathimini ya muundo na utendaji ndani ya vyombo vya habari dhidi ya uhamasishaji wa usawa wa kijinsia na kupinga udhalilishaji kwa wanahabari wanawake , inaonyesha kuwepo kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika vyumba vya habari. 
Ndugu Wadau wa habari: TAMWA tunasihi wadau wa habari kuungana kwa pamoja kwa lengo la kuwaimarisha wanahabari kwa kuwapa mafunzo, maarifa na kuwajengea uwezo juu ya masuala ya jinsia, ambayo itapelekea kuwezesha wanahabari kujitambua, kujiamini na kusaidia kuwepo kwa usawa wa kijinsia  na kutokomeza ukatili ndani ya vyumba vya habari.
Sera: TAMWA inasihi kuwepo na sera na mfumo rasmi wa kutoa taarifa za masuala ya ukatili wa kijinsia na usalama binafsi ambao hautatoa mwanya wowote wa unyanyasaji wa kingono, na taratibu thabiti za kuripoti unyanyasaji huo.
TAMWA inaomba ushirikiano zaidi kutoka kwa wadau wa habari wakiwemo, Asasi za kiraia,  Wizara ya Habari na Michezo, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee Watoto na Wizara ya sheria na katiba  kwa jamii kwa kuhakikisha uhuru wa habari unaeshimika na kupelekea wanahabari kutoa habari kwakufuata sheria na taratibu na kufikia jamii yote kama kaulimbio yetu inavyo sema “Habari kwa manufaa ya umma” 
Pia kutoa  elimu kwa wanahabari na kwa jamii kuhusiana na ukatili wa kijinsia, Kwani vitendo hivyo ni moja ya sababu ya kupotea kwa uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari katika kutekeleza majukumu yao.
Ndugu Wanahabari na vyombo vya habari: TAMWA tunasihi vyombo vya habari kuwa mastari wa mbale kuahabariasha na kutoa taarifa na kuburudisha kwa kuzingatia maadili yanayoongoza tasnia ya habari pamoja na kufuata sheria za nchi.   
Maadhimisho ya Mwaka 2021 yana mafanikio mengi katika tasnia ya habari, Kufuatia na ongezeko la vyombo vya Habari kulingana na takwimu alizozisema  Hayati Rais wa awamu ya tano Dk.John Joseph Pombe Magufuli, wakati  alivyokuwa Akizindua studio za vyombo vya habari vya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Hayati Rais Magufuli alisema katika kipindi cha miaka mitano serikali yake imeruhusu vyombo vingi zaidi vya habari kuliko wakati mwingine wowote tangu taifa hilo lipate uhuru.
Alisema  mwaka 2015, Tanzania ilikuwa na vituo vya radio 106 na televisheni 25 lakini hadi kufikia mwezi februari 2021 kuna jumla ya vituo vya redio 193, televisheni 46, magazeti 247,televisheni za mtandao 443 na redio za mtandao 23.
 
%%%%%%%%  “Habari kwa manufaa ya umma”  %%%%%%%%%
 
Imetolewa  Mei 27,2021 na:
Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam, Machi 29, 2021. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mwanahabari wa IPP Media, Blandina Sembu.
 
Taarifa ya Jeshi la Polisi inasema kuwa, mwili wa Sembu, aliyekuwa mtangazaji wa kipindi cha Wanawake, kinachorushwa na ITV, uliokotwa katika maeneo ya Bamaga usiku wa kuamkia Machi 28, hali ambayo inaonyesha utata wa mazingira ya kifo chake. 
 
TAMWA kimesikitishwa na tukio hilo lililompoteza mwanaharakati wa masuala ya wanawake, masuala ya watu wenye ulemavu na mwanahabari aliyeipenda kazi yake. 
 
"TAMWA ikiwa ni mdau mkuu wa wanahabari wanawake nchini , kimeguswa na tukio hilo na tunaziomba mamlaka husika kuchukua hatua za uchunguzi ili kujua undani wa kifo cha Sembu ikiwa kimesababishwa na watu basi hatua kali zichukuliwe kwa watekelezaji wa tukio hilo" Rose Reuben, Mkurugenzi wa TAMWA
 
TAMWA  itamkumbuka Sembu kwa mchango wake mkubwa katika masuala ya Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi kwani alikuwa ni mjumbe wa kamati ya  Muungano wa Ushiriki Tanzania iliyoangazia Ushiriki wa watu wenye ulemavu, wanawake na vijana katika siasa na uongozi. 
 
 Kuondoka kwa Sembu ni pengo kubwa kwa tasnia ya habari, jumuiya za watu wenye ulemavu na pia katika jumuiya zinazotetea haki za wanawake nchini kwani alijitoa kwa dhati na alihakikisha anasemea haki za makundi hayo, pale inapobidi.
 
TAMWA inatoa salamu za pole kwa wanafamilia wote wa Blandina Sembu, Watendaji na Wanahabari wa IPP Media, wanaharakati wa masuala ya jinsia, watu wenye ulemavu na wanahabari  wote  nchini.
 
Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji- TAMWA.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Mhe. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Innocent Bashungwa;

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Iddi Hassan Kimata;

Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari; Mhe.Eng. Kundo Andrea Mathew;

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk. Peter Mutuku Mathuki;

Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Anders Sjoberg;

Mwakilishi Mkazi wa Unesco nchini Tanzania, Mhe. Titso Dos Santos;

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Legal Service Facility, Lulu Ng’wanakilala;

Wawakilishi wa Jumuiya ya Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (MOAT);

Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika Tawi la Tanzania (MISA-Tan), Salome Kitomari;

Mwenyekiti wa Mtandao wa Radio za kijamii Tanzania (TADIO) Prosper Kwigize;

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa), Rose Reuben;

Wawakilishi wa Wakfu wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF)

Mwakilishi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT);

Wawakiliishi wa Umoja wa Club za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC)

Mwenyekiti wa Arusha Press Club, Claud Gwandu;

Wahariri na Waandishi wa habari;

Mabibi na Mabwana,

Mheshimiwa mgeni Rasmi, kwanza tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujalia uhai, na ni kwa neema zake kuwa leo tuko hapa kufanya shughuli hii muhimu ya kukumbushana utendaji wa vyombo vyabari nchini na duniani, ambapo hatimaye tutaimarisha ushirikiano kati ya dola, jamii na vyombo vya habari kwa masilahi mapana ya maendeleo ya taifa letu.

Nakushukuru kwa kukubali mwaliko wetu, kwani kwa kufanya hivi Mhe. Waziri unadhihirisha kwa matendo kauli ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati akiwaapisha makatibu wakuu kwamba serikali chini ya uongozi wake itaendelea kuenzi uhuru wa habari.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, April 13, 2021. Wakati kukiwa na mabadiliko ya teknolojia ulimwenguni kote, matukio ya ukatili wa kijinsia nayo yamekuja katika muundo mwingine wa njia ya mitandao ya kijamii.
Kutokana na mabadiliko hayo, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Friedrich Ebert Stiftung (FES), leo kinazindua kampeni maalum ya kupambana na ukatili wa kijinsia unaofanywa kwa njia ya mitandao ZUMICA #ZuiaUkatiliMtandaoni. 
Kampeni hiyo ya  mwezi mmoja, kuanzia mwezi 4 hadi 6 mwaka, 2021 inalenga, kupinga  vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto wa kike mitandaoni.
Ilizoeleka kuwa ukatili wa kijinsia unafanywa katika hali ya kudhuru mwili,  kama vile vipigo, ubakaji/ulawiti, ukeketaji, ndoa za utotoni, mimba za mapema, rushwa ya ngono na matusi, Roes Reuben, Mkurugenzi Mtendaji -TAMWA
Lakini baada ya kukua kwa teknolojia, ukatili huo sasa unafanyika kwa njia ya mtandaoni ambapo wanawake/ wanaume na hata watoto huweza kudhalilishwa kwa namna mbalimbali kwa kutumia mitandao ya internet kama vile facebook, whatsap, instagram, you tube na twitter.
 Wakati huo huo, takwimu za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zinaonyesha kuwa kuna ongezeko kubwa la watumiaji wa intaneti ambapo mpaka mwaka 2017, watumiaji waliongezeka kwa asilimia 16 na kufikia 23 milioni na asilimia 82 kati yao walitumia mitandao hiyo kwa njia ya simu. 
Takwimu za Globalstats  Feb 2020 - Feb 2021, zinaonyesha watanzania wanaotumia mtandao wa Facebook ni  38.81% ukifuatiwa na twitter 20.95% ,Youtube 11.25% na mwisho kabisa Instagram 5.78%.
 
 
“Tumeona  mara kadhaa video za utupu za wanawake, watoto wakike zikisambazwa katika mitandao hiyo. Tumeshuhudia matukio ya video za ngono za wanawake zikisambazwa kwa makusudi kabisa, huu ni udhalilishaji unaofanyika kwa njia ya mtandao, Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji -TAMWA.
Udhalilishaji huu una madhara kisaikolojia na hata kupelekea waathirika kuathirika kisaikolojia, hata kupelekea kujiua au kupoteza mwelekeo katika maisha. 
Nia ya TAMWA na FES ni kuzuia ukatii, kuongeza uelewa kwa jamii kujua madhara ya ukatili huu , lakini hasa wanawake kujua mbinu za kuepuka udhalilishaji wa aina hiyo, Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji -TAMWA.
Tunafahamu kuwa zipo sheria zinazozuia ukatili huu, kwa mfano, Sheria ya Maudhui ya Mitandaoni (Online Content Regulation) inakataza na kutoa adhabu kurusha maudhui ya udhalilishaji ikiwamo picha/video za utupu, lugha za udhalilishaji zinazokwenda kinyume na utamaduni wa Mtanzania.
Hata hivyo, bado udhalilishaji huu unaendelea, pengine ni kwa waathirika kutoifahamu sheria hii, au kuona aibu katika kutafuta haki au hofu ya kudhalilika zaidi pindi kesi itakapopelekwa mahakamani.
TAMWA tunasema, ni vyema kujua kuwa udhalilishaji huu haukubaliki, ni muhimu kutambua kuwa zipo sheria zinazotulinda, na ni muhimu zaidi kujua kuwa wapo wadau wanaoweza kukusaidia kuipata haki yako, Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji-TAMWA.
 
Aidha, kuna adhabu kwa wanaotumia mitandao hii ya kijamii vibaya ikiwamo faini ya Sh 5milioni au kifungo kisichopungua miezi 12 au kwa vyote kwa pamoja. 
Ukatili huu wa mtandaoni umeonekana kuwaathiri zaidi watoto wa kike na wanawake kutokana na namna ya makuzi na desturi za jamii yetu.
Baadhi  ya watekelezaji wa udhalilishaji huu  hutumia mitandao ya kijamii kama fimbo ya kuwachapia wanawake na watoto wa kike pale wanapofanikiwa katika jambo fulani au kupata nyadhifa mbalimbali za uongozi. Wakati mwingine, wanawake na watoto wa kike hudhalilishwa kwa sababu tu, ya wivu wa kimapenzi. 
Kwa mfano unapofika msimu wa uchaguzi ndiyo wakati ambao video au picha  za wagombea wanawake za udhalilisha husambazwa zaidi mitandaoni  kuonyesha kuwa hawafai kupata nafasi  za uongozi wanazowania, Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji-TAMWA.
 
Mifano mingine ni baadhi ya wasanii wa muziki na maigizo nchini hasa wanawake, ambao picha zao kusambaza picha za wanawake za kuwadhalilisha katika mitandao yao ya kijamii. 
Haya matukio yasichukuliwe ya kawaida, yakaonekana kama ada na sehemu ya desturi zetu, tunaiomba serikali iyavalie njuga na kuwapa adhabu kali wanaokutwa na hatia, Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji-TAMWA
TAMWA inatoa wito kwa serikali na asasi za kiraia  kuzungumzia madhara ya vitendo vya ukatili wa mitandaoni na kutoa elimu kwa jamii na kwa kizazi cha sasa, kuhusiana na madhara ya kutumia mitandao ya kijamii kama njia ya  kufanya vitendo vya ukatili ya kijinsia.
 “Wito wetu kwa jamii ni kuwa masuala ya ukatili wa kijinsi ni jukumu la kila mmoja wetu,  Asasi za kiraia, madawati ya kijinsia,Serikali, jeshi la polisi,Wasaidizi wa kisheria pamoja na watu maarufu kama wasanii katika  fani mbalimbali  tushirikiane  kwa vitendo kukemea vitendo hivyo.”
Kwa taarifa zaidi,
Rose Reuben.
E-mail:  This email address is being protected from spambots. You need JavaScript enabled to view it.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar Es Salaam, Machi, 19, 2021. Bodi ya wanachama, wanachama na Sekretariati ya Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuapishwa kuwa Rais wa awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
Rais Samia Suluhu Hassan aliyekuwa Makamu wa Rais, ameapishwa leo, Machi 19, 2021 baada ya kifo cha Hayati Rais John Magufuli ikiwa ni utekelezaji wa hatua za kikatiba na kisheria inayoeleza kuwa, Makamu wa Rais ataapishwa kuwa Rais, endapo Rais aliyeko madarakani atafariki dunia. 
 
TAMWA tunampongeza Rais huyu wa awamu ya sita, tukiamini kuwa ni kiongozi amestahili, makini na  anayekwenda kusimamia maadili, kusimamia katiba na kuzisimamia haki za wanawake na watoto. 
 
Tunaamini Rais wetu mpya ni muumini wa usawa wa kijinsia na hivyo atakwenda kuwa mstari wa mbele kusimamia sheria na haki zinazolinda watu wote, ikiwa ni pamoja na mwanamke hakika hatuna shaka na utendaji wake, TAMWA inaamini   ‘Wanawake Wanaweza  na sio kwa kuwezeshwa pekee bali waliaminika tangu enzi kwa kupewa madaraka ya kuwa  wasimamizi wakuu wa familia, kuanzia ngazi ya malezi,  jambo ambalo linawafanya kuwa imara, wanyenyekevu, wavumilivu na makini  zaidi hata katika nafasi za kisiasa na uongozi katika maeneo mengine.
 
Tangu akiwa Makamu wa Rais, amekuwa chachu kwa watoto wa kike na wanawake wa Tanzania katika kuwaza makubwa kwenye kuleta mabadiliko katika jamii ya kijinsia.
 
Hatuna  shaka na  utendaji kazi wa Rais wetu mpya na  historia yake ya kufanya kazi katika taasisi zisizo za kiserikali, kwa zaidi ya miaka kumi ambapo alijikita zaidi katika harakati za usawa kijinsia. 
Hivyo basi tunaamini kuwa atakwenda kusimamia ajenda hizo akiwa anaelewa kwa kina umuhimu wa usawa wa kijinsia na umuhimu wa kumaliza ukatili wa kijinsia,
 
Rais Samia Suluhu Hassan ameweka historia Afrika Mashariki  kwa kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Rais, jambo ambalo  litaacha alama kwa vizazi vijavyo na kisha kuulinda  na kuuheshimisha mfumo wa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi. 
Wakati tukiendelea kuomboleza msiba wa Hayati Rais John Magufuli, TAMWA ina imani kuwa, Rais Mama Samia Suluhu ataendelea kusimamia kauli yake  ile ya kuitaka jamii  kupinga na kupambana na vitendo vya ukatili katika maeneno yao.
 
Hongera Rais Samia Suluhu Hassan! Hongera Tanzania!
 
Rose Reuben,
Mkurugenzi Mtendaji,
TAMWA.

Search