Gallery

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, (TAMWA) kinaungana na Watanzania wote kuomboleza kifo cha Mwanadiplomasia Mkongwe, mwanahabri mahiri na Rais wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa.

TAMWA inakumbuka mchango wa Rais Mstaafu Hayati BWM katika kuijenga nchi hii kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni lakini hasa inaukumbuka mchango wake katika kujenga na kuhimiza usawa jinsia, kisheria, kisera na katika ngazi za maamuzi.

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 3, 2021. 
Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Siriel Mchembe kwa kusimamia kidete masuala ya ukatili wa kijinsia yanayotokea wilayani humo.
 Mchembe akitimiza majukumu yake ya kazi wilayani humo, ameweza kuibua ukatili unaofanywa na baadhi ya askari polisi wilayani humo, wanaodaiwa kuwashika sehemu za siri wasichana, kuwabaka, kuwapiga na kuwalazimisha kuwa na mahusiano ya kimapenzi. 
Mchembe ambaye pia kisheria ndiyo mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya, amenukuliwa akisema wazi katika mkutano huo kuwa; Mimi kama Mkuu wa wilaya, unyanyasaji wa kijinsia Handeni, Hapana.
Mkuu huyo wa Wilaya alichukua hatua za kuitisha mkutano baada ya kuwepo kwa madai ya  askari kuwapiga   na kuwajeruhi wasichana wawili katika ukumbi wa starehe wilayani humo kwa kile kinachodaiwa walikataa kuwa na mahusiano na askari hao. 
Katika mkutano huo walikuwepo wasichana ambao walitoa ushahidi wa wazi kuwa wanalazimishwa kuwa na mahusiano na askari na endapo wanawakataa basi wanawekwa mahabusu bila sababu ya msingi.
 Mashahidi wengine katika mkutano huo wamesema kuwa baadhi ya askari polisi huingia kwenye kumbi za starehe na kuwapiga wasichana bila sababu anuwai yenye mashiko.  
 Kadhalika, DC Mchembe alisimamia kidete tukio la mwezi Agosti mwaka huu, la mtoto wa miaka 10 kubakwa  mara kadhaa na kijana wa miaka 20 wilayani humo. 
TAMWA tunaamini kwamba utendaji kazi wa namna hii unaofanywa na Mheshimiwa Mchembe, utasaidia kupunguza matukio ya  ukatili wa kijinsia ambao umekuwa ukisababisha madhara makubwa ya kimwili na kiakili kwa watoto wa kike na wanawake. 
 Kadhalika, tunakemea vikali vitendo vya askari polisi kutumia madaraka yao vibaya  na kufanya ukatili wa kijinsi kama huu. 
Hakuna aliye juu ya sheria, na ndiyo maana askari wana dhamana ya kusimamia sheria hizi, lakini cha ajabu baadhi wamekuwa wa kwanza kuzivunja, Dkt Rose Reuben, Mkurugenzi Mtendaji, TAMWA.
Dkt Reuben amesema ukatili wa namna hii sio tu unavunja haki za binadamu lakini pia ndicho chanzo cha madhara mengi ikiwamo mimba zisizotarajiwa, mimba za mapema, magonjwa ya kuambukiza na wakati mwingine madhara ya kimwili kama majeraha. 
Polisi wasimamie maadili yao ya kulinda raia na mali zao, wasiwe washika bendera wa kuendeleza ukatili wa kijinsia, hakuna aliye juu ya sheria, amesema Dkt Reuben. 
TAMWA tunaomba askari watakaobainika kufanya ukatili huo wachukuliwe hatua huku tukiendelea kumtia moyo Mheshimiwa Mchembe kulinda na kutetea haki za wanawake na watoto wilayani humo. 
Dkt Rose  Reuben
Mkurugenzi Mtendaji
TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Dar es Salaam Agost 12, 2020. Wakati macho na masikio ya Watanzania yakiisubiri kwa hamu Oktoba 28 ambayo ni siku ya uchaguzi mkuu nchini, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF) pamoja na Global Peace Foundation (GPF) tunaoa mapendekezo kwa  vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi, kuondoa changamoto zote zinazochagiza ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
Uchaguzi Mkuu unafanyika wakati ambapo kati ya wagombea 16 waliochukua fomu kugombea urais, wapo wanawake wawili mpaka sasa ambao ni Queen Cathbert Sendinga wa Chama cha ADC, na Cecilia Augustino wa Demokrasia Makini walioteuliwa na vyama vyao kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi huo. Kadhalika, wapo wanawake watano wanaowania umakamu wa Rais, katika mchakato huu wa uchaguzi. 
Lakini TAMWA, WiLDAF  na GPF  taasisi ambazo malengo yake ni kuwepo kwa jamii yenye amani, inayoheshimu haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia, na amani zimeona ni vyema kuikumbusha jamii, wadau wa masuala ya siasa na ya jinsia  kuzifanyia kazi changamoto zinazochangia ushiriki duni wa wanawake katika siasa. 
 TAMWA WiLDAF  na GPF  chini ya ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake Afrika, (AWDF) kupitia mradi wa ‘Wanawake Sasa’ imeendesha midahalo mbalimbali ya wanawake kutoka  vyama vya siasa ,wakiwamo wanawake wanasiasa, viongozi wa dini na kubaini kuwa bado kuna changamoto  zinazopelekea ushiriki mdogo wa wanawake katika siasa.
Midahalo tuliyofanya  katika  kanda za Dodoma, Arusha, Zanzibar na Dar es Salaam, iliibua changamoto zinazowakabili wanawake katika siasa ikiwamo lugha dhalilishi  zinazowavunja moyo wanawake  wanaogombea au walio katika nafasi za uongozi pamoja na familia zao kuwania nafasi mbali mbali za uongozi.
Wanawake wanaogombea nafasi za uongozi, hukutana na changamoto  ya lugha dhalilishi wakati wa kampeni, na hata wakati wa utendaji wao wa kazi ili tu kuwakatisha tamaa na kuwarudisha nyuma. Kama tunataka uchaguzi wa haki na wa kidemokrasia, ni muhimu kwa tume ya uchaguzi na vyombo vya usalama kupiga marufuku na kutoa adhabu kali kwa wanasiasa watakaotoa lugha hizi dhidi ya wanawake, Rose Reuben, Mkurugenzi TAMWA.
Katika midahalo hiyo, TAMWA , WiLDAF  na GPF  tumebaini kuwepo kwa rushwa ya kifedha katika shughuli za kawaida za siasa na hasa wakati wa chaguzi mbali mbali za ndani ya vyama, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu. Hii ni pamoja na tabia za wajumbe wanaotegemewa kupiga kura kuwa na hulka ya kudai au kujenga mazingira ya kupewa kitu kidogo ili waweze kutoa ushirikiano kwa mgombea. Hii inaathiri  wanawake ambao wengi wao hawana kipato cha kutosha hasa wanawake vijana. 
 
Pia tumebaini uwepo wa vitendo vya kuomba au kutengeneza mazingira ya rushwa ya ngono kwa baadhi ya wanaume wenye dhamana za kusimamia michakato ya chaguzi au mamlaka ndani ya vyama vya siasa.Changamoto hiyo husababisha wanawake kudhalilishwa na kuharibiwa ndoto zao za kisiasa na wakati mwingine familia au wenzi wao kuwazuia kushiriki katika siasa. 
Hayo na mengine mengi, yanachangia wanawake, kuvunjika moyo na hivyo kutoshiriki shughuli za siasa au kukosa nafasi za uongozi pale wanapokuwa na msimamo wa kutotoa rushwa.
Katika hili tunapenda kutoa rai kwa wanawake wenzetu kukataa kabisa kudhalilishwa na kutojihusisha na vitendo vya rushwa ya fedha au ngono na pia tunashauri jumuiya za wanawake ndani ya vyama vya sisasa kuvunja ukimya na kuhakikisha hoja za rushwa katika siasa inazungumzwa katika kila vikao vya jumuiya na vikao vingine muhimu. 
Pia tunaviomba vyama vya siasa viweke utaratibu madhubuti na wa siri wa kutoa taarifa za vitendo hivi na kuwe na kamati huru ndani ya vyama zisizofungamana na yeyote zitakazoratibu upokeaji, ufuatiliaji na utoaji adhabu kwa wale ambao bado wanaendekeza vitendo hivi vya kuwadhalilisha wanawake.   
Changamoto nyingine zilizoibuliwa katika midahalo hiyo,  ni Ilani za vyama vya siasa ambazo hazitoi nafasi kwa wanawake kuwa viongozi na kupata nafasi ya kugombea katika majimbo. Tumebaini wanawake wengi wanashindwa kushiriki uchaguzi kwa kutopata baraka hii kuanzia ndani ya vyama.
Wakati huo huo tunavitaka, vyama hivyo viwachague wanawake wenye uwezo wa kisiasa na wa uongozi.
Tunapenda kuvipongeza vyama vya siasa ambavyo vimetoa nafasi za wanawake kugombea nafasi za udiwani na ubunge na hata urais katika kura za maoni. 
“Mwaka huu wanawake wengi wamejitokeza. Tungependa kuviomba vyama vya siasa kuhakikisha kuwa wale wanawake wenye uwezo wasimamishwe kugombea nafasi hizo na tunawaomba wananchi wote kuwachagua wanawake waliosimamishwa kugombea nafasi za ubunge na udiwani, na wengine wapewe nafasi za teuzi mbalimbali Mkurugenzi wa GPF , Martha Nghambi. 
Tunavikumbusha vyama kuendelea kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wanawake ambao hawakupata nafasi mwaka huu ili waweze kusimama na kugombea chaguzi zijazo ndani ya vyama vyao, serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
Kadhalika tunapenda kuwaasa wanawake kuepuka kugawanywa na zile kauli kuwa, hawapendani badala yake waendelee kushirikiana na kupeana fursa mbalimbali za kisiasa, kiuchumi na masuala ya kijamii.
Kauli hizi za kuwa wanawake hatupendani si za kweli bali zimekuwa zikitumika katika jamii kuwagawa wanawake kuwania nafasi mbalimbali za uongozi, Reuben 
Tunatarajia kuwa serikali, wadau wa siasa, vyombo vya usalama vitazingatia kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, DK John   Pombe Magufuli ya kuwepo kwa mazingira wezeshi kwa wanawake katika uchaguzi mkuu na katika nafasi za uongozi na maamuzi. Pia tunampongeza kwa kuendelea kumchagua Mama Samia Suluhu kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao. 
 
Tungependa kumalizia kwa kusisitiza kauli zilizotolewa na Rais, viongozi wa vyama mbali mbali na tume ya taifa ya uchaguzi kuwa uchaguzi wa mwaka huu utakuwa ni  huru, haki na wa amani. 
Tunawakumbusha wagombea wote kuhakikisha kuwa hawatoi kauli zozote za uvunjifu wa Amani, kuchochea vurugu, kuwagawa watu kwa dini au makabila yao au matusi na udhalilishaji wa kijinsia kwa wagombea wengine. 
Wakati huo, TAMWA, WiLDAF na GPF  inaiomba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuendelea kuhimiza uchaguzi huru, wa haki na usawa na kutengenezwa kwa mazingira sawa ya ushindani kwa wagombea wote.
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ubariki Uchaguzi Mkuu wa Octoba 2020. 
 
Rose Reuben Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA
Anna Kulaya Mkurugenzi - WILDAF
Martha Nghambi Mkurugenzi - GPF

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Septemba 13, 2021. Dar Es Salaam. Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kinampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa kuteua wanawake wawili katika Baraza la Mawaziri.
 
Uteuzi huo umefanyika jana ambapo Dkt Ashatu Kijaji ameteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na  Teknolojia ya Habari, wakati Dkt Stergomena Tax ameteuliwa kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
Uteuzi huu unafanya idadi ya mawaziri wanawake kufikia saba, kutoka watano walioteuliwa awali. 
 
TAMWA tunampongeza Rais Samia pia kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kumteua mwanamke kushika wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. 
 
"Uteuzi alioufanya Rais, wa kuongeza mawaziri wawili katika baraza unaonyesha dhahiri kuwa wanawake wanaaminika na wana uwezo wa kuleta mabadiliko katika Nyanja zote, kisiasa, kiuchumi na kijamii" Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk Rose Reuben. 
 
TAMWA tunaamini kuwa ushiriki wa wanawake katika siasa na uongozi ndiyo nguzo muhimu ya kuleta usawa na ndicho chanzo cha kuleta mabadiliko chanya katika jamii ambayo yataletwa katika usawa, haki na uwajibikaji. 
 
"Rais Samia, ameweza kuonyesha lile ambalo lilidhaniwa haliwezekani kwa kuwaweka mawaziri wanawake katika wizara nyeti  kama ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa, pia kwa kuendelea kuteua mawaziri wanawake, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na makatibu tawala" amesema Dkt Reuben
 
Kadhalika tunampongeza Rais kwa ile kauli yake wakati akiwaapisha mawaziri hao aliposema: Nimeamua kuvunja taboo (mwiko), iliyoaminika kwamba wizara ya ulinzi lazima akae mwanaume mwenye misuli yake, kazi ya wizara ile si kupiga mizinga au kushika bunduki,  nimevunja taboo(mwiko) hiyo na kumteua dada yetu Tax kutokana na upeo wake mkubwa alioupata akiwa Jumuiya ya Nchi zilizo kusini mwa Jangwa la Sahara
 
“Hakika Rais amevunja dhana ya kuwa wanaume pekee ndiyo wenye uwezo wa kushika wizara hii, na kwa hili tunategemea Dkt Tax hatatuangusha, bali atasimamia vyema nafasi hiyo na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika masuala ya ulinzi na usalama,kwa kuwa ana uwezo na upeo" Dk Reuben 
Kadhalika TAMWA tunampongeza Rais Samia kwa kusikiliza kilio cha wanahabari na kuunganisha Wizara ya Habari, Mawasiliano na ile ya Teknolojia ya Mawasiliano, kuwa moja. 
Hatua hiyo itawafanya wadau wa habari kufanya kazi kwa ufanisi na wepesi zaidi kuliko hapo awali. 
TAMWA tunaamini kuwa Ushiriki wa Wanawake katika Siasa na Uongozi na katika ngazi za maamuzi ndicho chanzo cha haki, usawa na uwajibikaji na maendeleo  ya nchi. 
Wanawake Wanaweza! Kazi Iendelee!
Dkt Rose Reuben
Mkurugenzi Mtendaji - TAMWA

Star InactiveStar InactiveStar InactiveStar InactiveStar Inactive
Machi 8th 2022, Dar es Salaam. Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania, kinalazimika kutupia jicho lake kwenye usalama wa wanahabari wanawake katika vyumba vya habari nchini Tanzania.
 
Ulazima huu umekuja baada ya kuwepo kwa mwendelezo wa matukio, ushahidi, na ripoti za kitafiti zinazoonyesha kuwa wanahabari wanawake siyo tu Tanzania bado wanapitia unyanyasaji wa kingono katika vyumba vya habari. 
 
Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kwa mwaka huu, yamebebwa na Kauli mbiu isemayo; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu. Kauli hii inatupeleka zaidi kutaka kuweka usawa katika vyumba vya habari baada ya kubaini kuna mdudu anayetafuna tasnia ya habari kimya kimya. 
 
 Utafiti uliofanywa na Asasi ya Wanawake katika Habari Africa (WIN) mwaka 2022 ulibaini kuwa, asilimia 41 ya wanawake wanahabari waliwahi kufanyiwa unyanyasaji wa kingono wakiwa katika maeneo ya kazi. 
 
Hivyo basi wakati tukiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, TAMWA inahimiza Wamiliki wa vyombo vya habari, watunga sera, serikali na wanahabari wote kwa ujumla kutupia jicho unyanyasaji na ukatili wa kingono unaofanywa ndani ya vyumba vya habari.
 
Unyanyasaji wa kingono kwa wanahabari iwe ndani au nje ya vyumba vya habari, una madhara makubwa katika chombo cha habari, taaluma ya habari, aina ya habari zitakazoandikwa na hata katika maendeleo ya nchi yenyewe. Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dk  Rose Reuben.
 
Udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari wanawake, unachagiza wanahabari wengi wa kike kuikimbia tasnia  na hilo limesababisha kupoteza vipaji lukuki ambavyo vingekuzwa iwapo kusingekuwa na bughudha hiyo.
 
 
Kadhalika udhalilishaji wa kingono kwa wanahabari unashusha hadhi ya chombo cha habari, kwani pindi mwanahabari anapotoa shutuma kuwa mhariri au kiongozi wa chombo cha habari kamdhalilisha kingono, basi ni dhahiri chombo hicho hutazamwa vibaya. Kadhalika vivyo hivyo anapotoa taarifa kuwa amedhalilishwa na chanzo cha habari.
 
Kaika utafiti uliofanywa na TAMWA kwa kushirikiana na Mfuko wa Wanawake Tanzania (WFT) mwaka 2021, kuhusu hali ya rushwa ya ngono ndani ya vyumba vya habari, ilibainika kuwa wanahabari wanawake wamewahi kukutana na udhalilishaji huu, kimwili, kimaneno na hata baadhi walifukuzwa kazi. 
 
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyoiona TAMWA katika tafiti hizo ni ukimya. Wanahabari wengi wanawake hawataki kusema pindi wanapodhalilishwa, hivyo wanaishi katika msongo, maumivu, fedheha na wengine kuacha kabisa tasnia, kwa sababu ya udhalilishaji wa aina hii.  Dk Rose Reuben.
 
Utafiti wa TAMWA ulibaini kuwa wanafunzi wengi wa tasnia ya habari wa vyuo vikuu wanaokwenda kujifunza kwa vitendo  katika vyumba vya habari wamekutana na udhalilishaji huo na kujikuta wakiikimbia tasnia hiyo mara tu wanapomaliza masomo yao. 
 
Hata utafiti wa WIN uliofanyika Afrika nzima kuangalia ukubwa  wa tatizo hilo, ulibaini kuwa ni asilimia 4 tu ya wanahabari wanawake wanaopaza sauti zao pindi wanapofanyiwa ukatili huu.
 
Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka huu, kwanza tunawaasa wanahabari kupaza sauti zao na kueleza bayana madhila wanayopitia katika kazi zao ikiwamo udhalilishaji wa kingono.
 
Imetosha sasa wanahabari kuwa kipaza sauti cha kusemea matatizo ya wengine  katika jamii, ilhali tatizo lao wamelinyamazia kimya, Dk Rose Reuben.
 
Kadhalika tunaviomba vyombo vya habari kuhakikisha vinaweka na ketekeleza sera ya jinsia ndani ya vyumba vya habari, na sera ya kupinga unyanyasaji na rushwa ya ngono na sera hizi zijulikane na wote ndani ya vyumba vya habari. 
 
Katika utafiti wa TAMWA tulibaini kuwa vyumba vingi vya habari havina sera ya jinsia wala sera za kupinga rushwa na unyanyasaji wa kingono, na vile vyenye sera hizi hazitumiki au hazijulikani na wanahabari/ wafanyakazi wengine, Dk Rose Reuben.
 
Lakini zaidi tunaiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kushirikiana na wadau kutoa elimu kuhusu sheria ya mwaka 2017 inayoangalia rushwa ya ngono mahala pa kazi. Hii itasaidia wanawake na wasichana kuifahamu  kujua kuwa uwepo wa sheria hii na namna ya kukusanya ushahidi wa madhila hayo. 
 
Lakini wakati huo huo serikali ione umuhimu wa kupeleka ajenda ya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu na hata mashuleni, ili kuwajengea uelewa watoto wa Tanzania uelewa na athari ya rushwa hii. 
 
Kwa mfano, hivi karibuni yamekuwapo matukio kadhaa ya wahadhiri kwa vyuo vikuu kuwadhalilisha kingono wanafunzi na huku video zao za utupu zikivuja. Haya na mengine mengi yapo pia katika vyombo vya habari na mahala pa kazi ikiwamo serikalini. 
 
Kwetu sisi TAMWA hili ni janga na ni muuaji wa kimya kimya wa utu wa wanawake,  endapo lisipochukuliwa hatua basi mabinti zetu vyuoni na wanataaluma katika uandishi watapoteza mwelekeo na hivyo tutapoteza vipaji na nguvu kazi, Dk Rose Reuben.
 
 
Kama kauli mbiu ya mwaka huu isemavyo, Haki Sawa kwa maendeleo Endelevu ndivyo tunavyotaka wanahabari wanawake waheshimiwe na wathaminiwe, watimize wajibu wao bila kulazimishwa au kurubuniwa kutoa rushwa ya ngono. 
 
Tunachoweza kusema TAMWA ni; Mwanahabari mwanamke anaweza kuripoti habari za uchunguzi kama mwanaume, anaweza kuripoti michezo kama mwanaume, anaweza kuripoti katika vita kama ilivyo kwa wanaume. Uanamke wake, hauondoi ujasiri, utimamu na umakini katika taaluma  yake. 
 
Kadhalika, Mwanahabari mwanamke hapimwi kwa sura wala sauti yake, bali ujuzi na kipaji katika taaluma yake ya uanahabari. 
 
TAMWA tunasisitiza kuwa hiki ni; Kizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu kama kauli mbiu  ya mwaka huu isemavyo. 
 
 
Mkurugenzi Mtendaji
 
Dk Rose Reuben
TAMWA
 

User Rating: 5 / 5

Star ActiveStar ActiveStar ActiveStar ActiveStar Active

Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimewataka wazazi, walezi, jamii hasa wanahabari kuchukua hatua na kulinda haki za wahanga wa ukatili wa jinsia na usalama wao katika mitandao ya jamii ili kuepusha udhalilishaji zaidi unaoweza kujitokeza.


TAMWA inachukua hatua hii baada ya kuendelea kusambaa kwa video fupi na maudhui, ya binti wa kidato cha tano wa shule ya Panda Hill mkoani Mbeya, aliyetoroka shule na kisha kudaiwa kukimbilia kwa mwanaume aitwaye Baba Jose.


Baada ya kusambaa kwa maudhui hayo, kumeendelea kusambaa video fupi na taarifa mbalimbali zikimuonyesha binti huyo akijieleza na kwenda mbali zaidi kuwa alifanyiwa ukatili wa kijinsia yaani kubakwa na mwalimu wake wa nidhamu, jambo lililovuta maoni mengi dhalili.


Hofu ya TAMWA inajikita zaidi katika utu, usalama, na hatma ya baadaye ya binti huyu ambaye mahojiano yake yanaendelea kusambaa huku wasambazaji na waandaji wa maudhui hayo wakiacha sura yake ionekane wazi wazi, jambo ambalo linavuta hisia na maneno dhalili yanayoweza kuweka usalama wake na afya yake ya akili hatarini.


TAMWA tunaamini kuwa binti huyu bado anayo nafasi ya kujenga hatma yake, hata kuendelea na masomo na baade kuwa mwanajamii mwenye mchango mkubwa kwa taifa.
Pia vyombo vya dola vilivyochukua maelezo yake ya awali vinauwezo wa kuhakikisha haki yake inapatikana vizuri zaidi kuliko mijadala inayozuka baada ya mahojiano yake na waandishi wasiofuata maadili na kusambaza mitandaoni.
Binti huyu bado ana haki ya kulindwa na wazazi, walezi, jamii, serikali na waandishi wa habari na ndio maana TAMWA tunapata wasiwasi anavyoendelea kuhojiwa na kusambazwa mitandaoni ambako kunazua hisia na mijadala dhalili, kutukanwa na kutuhumiwa.


Lakini pia, mpaka sasa inatushangaza kwani hatujaona wazazi au walezi wake wakisimama moja kwa moja kuzungumzia suala hilo na badala yake binti huyo ameachwa kujieleza peke yake kwa wanahabari ambao nao wameshindwa kulinda utu wa muathirika kwa mujibu wa maadili ya uandishi. Maadili ya uanahabari yanasisitiza kuficha sura ya waathrika wa ukatili hata ikiwezekana wazazi wa mtu/mtoto aliyefanyiwa udhalilishaji, ili kumlinda na kulinda utu wake na kumpunguzia maumivu ya ukatili aliopitia na katika hili binti huyu anastahili kulindwa.

Kwa mujibu wa kanuni zilizotengenezwa Baraza la Habari Tanzania (MCT,2020) ni kinyume cha maadili kuwabainisha watoto walionyanyaswa, kutumika vibaya au walioshtakiwa na kupatikana na hatia ya jinai. Kanuni hizo zinawataka waandishi wa habari kuchukua tahadhari katika kutumia picha na majina na waepuke kuchapisha taarifa kunapokuwa na uwezekano wa kuwaathiri wahusika.


Inaelezwa kuwa baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kutoa amri ya kutafutwa kwa binti huyo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera naye alitoa amri ya kusakwa. Alipopatikana taarifa zinaeleza kuwa, mwanamke aliyejitambulisha kama mama Abdul, ambaye naye alisema, binti huyo alipelekwa kwake na mwanaume mmoja aitwaye baba Jose, ambaye naye alisema: “Ni mke wake ...” Na baada ya hapo vyombo vya dola vilikusanya maelezo.

Katika hali hiyo TAMWA, kama wadau wa habari na watetezi haki za wanawake, wasichana na watoto, tunawataka wazazi, walezi , jamii na wanahabari kuwajibika na kulinda haki za wanawake na watoto, waliopitia ukatili wa kijinsia, ili kuepusha madhara ya kudumu na makubwa zaidi, ya kimwili na kisaikolojia kwa muathirika.


Imetolewa na


Dkt Rose Reuben

Mkurugenzi Mtendaji.

Search